CHAPO: 'WANAFUNZI WAIBUWENI WANAOTAKA KUWADHALILISHA'

 



NA MWANDISHI MAALUM, CHAPO

WANAFUNZI wa chuo cha Qur-an cha kijiji cha Vikutani shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake Pemba, wametakiwa kuwaibua ndugu na jamaa zao, wanaoashiria kutaka kuwafanyia vitendo vya udhalilishaji.

Ushauri huo umetolewa Januari 29, 2023 na Msaidizi wa sheria Jimbo la Wawi Haji Nassor, wakati akitoa elimu ya kupambana na matukio ya ukatili na udhalilishaji, hasa kwa watu wao wa karibu, kwenye mkutano uliofanyika chuoni hapo.

Alisema, tafiti kadhaa zinaonesha kuwa, sasa watoto wamekuwa wakifanyiwa vitendo hivyo na watu wao wa karibu, na kushindwa kutoa taarifa hizo, katika maeneo husika.

Alieleza kuwa, wakati umefika sasa kutowafumbia macho watu hao, kwani wamekuwa wakishindwa kuonesha upendo wa kweli kwao, jambo ambalo linaweza kusababisha kupoteza mwelekeo wa maisha yao.

‘’Wanafunzi niwasihi sana kuwa, iwapo kuna kaka, baba, ami, mjombo ameanza kukufanyia vitendo vya udhalilishaji, mseme kwa wenzako au wetu wengine wa karibu,’’alifafanua.

Aidha Msaidizi huyo wa sheria alisema, eneo moja ya kuripoti matukio hayo ni kwa mratibu wa wanawake na watoto, katibu wa sheha, wajumbe wake au kwa msaidizi wa sheria katika eneo wanaloishi.

Mapema Afisa sheria kutoka Idara ya Katiba na Msaada wa kisheria Unguja Ali Haji Hassan, aliwataka wazazi na walezi kukataa kufanya sulhu kwa makosa ya ukatili na udhalilishaji.

‘’Haiwezekani, mtoto ameshaharibiwa kwa ubakaji au ulawiti, kisha wazazi wakubali kukaa chini, eti kuyamaliza kienyeji, kwani makosa haya uamuzi wake ni mahakamani,’’alieleza.



Hata hivyo amewataka wanachi Wawi, kuendelea kuwatumia wasaidizi wa sheria waliomo, kwa ajili ya kupata elimu, ushauri na msaada wa kisheria.

Nae Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, alisema kama jamii haijaamua kuyakataa matendo hayo, watoto wataendelea kudhalilika.






Alieleza kuwa, watoto wanaofanyiwa ukatili na udhalilishaji, wanawategemea mno wazazi na walezi wao wawasimamie katika vyombo vya sheria, hivyo wakishindwa kufanya hivyo ni kuwaumiza mara mbili.

‘’Wazazi sote tuungane katika kupiga vita matendo haya, maana wanaowaumiza kiakili, mwili ni watoto wetu sasa kama hatuko makini, tutawavunjia ndoto zao za baadae,’’alieleza.



Mapema mjumbe wa sheha wa shehia ya Wawi Nassor Rashid, aliwataka wasaidizi hao wa sheria, kuendelea kukutana na jamii ya Wawi, kwani kumekuwa na shida ya elimu ya kutosha.



Baadhi ya wanafunzi walisema, elimu walioyoipata imewaongezea maarifa katika kupambana na matukio ya ukatili na udhalilishaji.

  

                    Mwisho   

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’