AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

 

NA HAJI NASSOR, PEMBA @@@@

AFISA Mdhamini wizara ya Nchi Afisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Pemba, Halima Ali Khamis, ameitaka Afisi ya Mwanasheria Mkuu Zanzibar ‘AGCZ’ kurudi tena kwa wadau, baada ya kuyachakata maoani ya sheria nambari 13 ya mwaka 2018 ya Msaada wa Kisheria Zanzibar.

 Mdhamini huyo aliyasema hayo leo Novemba 13, 2025, ukumbi wa wizara ya Fedha Pemba, alipokuwa akifungua kikao kazi, cha kukusanya maoni ya sheria ya Msaada wa Kisheria, mbele ya wadau wakiwemo wasaidizi wa sheria, Polisi, Masheha na wadau wa haki za binaadamu.

Alisema itapendeza zaidi, baada ya kukusanya maoni hayo kwa Afisi ya Mwanasheria Mkuu kurudi tena kwa wadau, ili kujadiliana kabla ya kuandikwa, kama sheria ya msaada wa kisheria.



Alieleza kuwa, wadau wanataka kuona maoni yao, ikiwa yamezingatiwa kwa kiasi gani, kwenye uandikwaji wa sheria hiyo upya hapo baadae.

‘’Niwaombe sana wenzetu wa ofisi ya 'AGCZ', mkumbuke kurudi tena kwa wadau, baada ya kukusanya maoni, ili kabla haijapelekwa hatua nyingine, kwanza wajiridhishe,’’alifafanua.

Katika hatua nyingine Afisa Mdhamini huyo, alisema, msingi wa usaidizi wa sheria, utaendelea kuwa mwarubaini wa upatikanaji wa haki kwa wananchi wasiokuwa na uwezo wa kifedha wala uwelewa wa sheria.

Alieleza kuwa, kazi hiyo kwa sasa, inasisimiwa na Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, na hasa ndani ya awamu ya nane, inayoongozwa na Dk. Hussein Ali Mwinyi.


Alieleza kuwa, mazingira ya upatikanaji wa msaada wa kisheria bila ya malipo, umesaidia ndani ya uongozi wa Dk. Mwinyi, kuimarisha utawala bora na utawala wa sheria.

‘’Msingi wa usaidizi wa sheria kwa wananchi, imekuwa ni sehemu ya kuimarisha utawala bora, na leo tunajivunia kwa kazi kubwa iliyofanywa na Mkurugenzi wa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar,’’alifafanua.

Wakati huo huo, Afisa Mdhamini huyo, alitumia nafasi hiyo, kumpongeza Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ali Mwinyi, kwa kuchaguliwa tena, kuiongoza Zanzibar kwa awamu ya pili.

Aidha, aliwataka wadau wa kikao hicho kazi, kuwa huru kutoa maoni yao kwa maslahi mapana ya taifa, ili kuwa na sheria rafiki kwa watoa msaada wa kisheria, na wasimamizi wa haki jinai na madai.

‘’Kwa mfano ndani ya mapendekezo ya sheria hiyo, limo, suala la kuanzishwa kwa mfuko wa msaada wa kisheria ‘Legal Aid Fund’, ili kuonesha umuhimu wa kuwepo kwake ama kutokuwepo,’’alishauri.

Mapema Wakili wa serikali kutoka Afisi ya Mwanasheria Mkuu Zanzibar Mbarouk Suleiman Omar, alisema ofisi iliamua kuifanyia mapitio sheria hiyo, ili iendane na mazingira yaliopo.

Alisema, wamekuwa na utaratibu wa kuzipitia sheria kadhaa, ambapo kwa sasa ni hiyo ya Msaada wa Kisheria Nambari 13 ya mwaka 2018.

Akiwasilisha mapendekezo ya sheria hiyo, Wakili wa serikali kutoka ofisi ya AGCZ, Sumaiya Awadhi Hassan alisema, wameona kuangalia, kuna uwezekano wa kupatikana msaada wa kisheria kwa makosa ya madai, ikiwa mtu ameishtaka serikali.



Alisema jingine ni kuanzishwa kwa vituo vya msaada wa kisheria ‘legal aid clic’, ambapo sheria ya sasa haijaeleza kuhusu kuvitambua hivyo, jambo ambalo kama wadau watahisi linauhimu watalisemea.

Akichangia kwenye sheria hiyo, mjumbe kutoka Mwemvuli wa Asasi za Kiraia Pemba ‘PACSO’ Mohamed Najim Omar, alisema kuwa, suala la kukosekana kwa mfuko wa wasaidizi wa sheria ni tatizo.










Nae Said Rashid Hassan, kutoka Shirika la Msaada wa Kisheria na Haki za Binaadamu Zanzibar ‘ZALHO’ alishauri kuwa, makosa ya dawa za kulevya na yanayofanana na hayo, yasiingizwe kwenye makosa yanayopewa msaada wa kisheria.

Afisi ya Mwanasheria Mkuu Zanzibar ambayo imeanzishwa chini ya sheria nambari  6 ya mwaka 2013 ambapo miongoni mwa majukumu yake makuu ni kuzifanyia marekebisho sheria mbali mbali.

                       Mwisho  

Comments

Popular posts from this blog

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’