MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU
MKURUGENZI wa Idara ya
Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, Hanifa Ramadhan Said, amewataka wananchi
wa shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake, kulindiana haki zao za binaadamu, ili
kujengeana heshima baina yao.
Hayo aliyasema leo August
11, 2025 eneo la Kwa Gerei shehiani humo, wakati akizungumza na wananchi
hao, kwenye mkutano wa wazi wa kutoa elimu ya haki za binaadamu.
Alisema kila mmoja anawajibu
wa kumlindia haki za binaadamu mwenzake, na kufanya hivyo kutajengeana heshima miongoni
mwao.
‘’Haki za binaadamu ni pamoja
na ile ya kuishi na kupata faragha, sasa kama kila mmoja atamlindiana mwenzake,
heshima kwa wananchi, itaongezeka,’’alisema.
Hata hivyo Mkurugenzi huyo wa
Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, amewakumbusha wananchi hao, kuwatumia wasaidizi
wa sheria, waliomo ndani ya shehia, ili kupata ufafanuzi wa changamoto zao za
kisheria.
Mapema Afisa sheria kutoka
Ofisi ya Mwanasheria Mkuu Pemba Safia Saleh Sultan, alisema haki za binaadamu ni
zile alizomwanadamu kwa sababu ya ubinaadamu wake.
‘’Kwa mfano haki za kisiasa,
uchumi, faragha, haki za kujikusanya na kwenda mtu atakapo bila ya kuvunja
sheria, ni sehemu ya haki za binaadamu,’’alifafanua.
Aidha, alisema kila mmoja ana
haki ya kuheshima haki za mwingine, na sio sahihi kuwa ni kwa mamla za serikali
pekee, ndio zinapaswa kuheshima haki za binaadamu.
Akijibu baadhi ya maswali
yalioulizwa na wananchi, alisema kisheria mtoto chini ya miaka 18 hana ridhaa,
hivyo hata kama kuna makubaliano, huitwa tendo la ubakaji.
‘’Kwa mfano mtoto ametoka
kilomita 100 na kumfuata mwanamme nyumbani kwake, bado kwa mujibu wa sheria huo
huitwa ubakaji, pindi likifanyika tendo,’’alifafanua.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji
Baraza la Vijana Zanzibar Ali Haji Hassan, aliwataka wananchi, kufuatilia
nyaraka kwa watoto wao, na sio kusubiri mpaka wakiwa wanazitaka kwa matumizi.
‘’Mtoto akizaliwa tu
afuatiliwe cheti chake, na akifia miaka 18 familia zifike ofisi za vitambulisho
ili taratibu zianze,’’alisema.
Mkuu wa Divisheni Idara ya
Katiba na Msaada wa kisheria Pemba Bakar Omar Ali, alisema mikutano hiyo ni kwa
ajili ya wananchi, kupata elimu ya sheria na hasa eneo la haki za binaadamu.
Akizungumza kwa niaba ya
wananchi wenzake, Nassor Said Rashid, alisema elimu zaidi ya kisheria
inahitajika kwa jamii.
Akifunga mkutano huo, sheha
wa Wawi Khamis Mohamed Khamis, aliwataka wananchi wasisite kuhudhuria wanapoitwa
kwenye mikutano mbali mbali.
Aidha aliipongeza Idara ya
Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, kwa uamuzi wake wa kuziacha shehia
nyingine na kuitisha mkutano huo, shehiani mwake.
Mwisho
Comments
Post a Comment