‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’
NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WANANCHI wa shehia ya Mchakwe na Mwambe wilaya ya
Mkoani, wamekumbushwa kuwa, ni kosa la kisheria, kujichukulia sheria mikononi, kwa
kuondoa uhai wa mtu, kwani kufanya hivyo, ni kuzipokonya kazi mamlaka zilizopo
kisheria.
Hayo yalielezwa jana August 12, 2025 na Wakili wa
serikali kutoka ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa serikali Safia Saleh Sultan,
wakati akizungumza na wanachi hao, kwenye mkutano wa wazi, ulioandaliwa kwa
pamoja na Idara ya Katiba na Msaada wa kisheria Zanzibar na kufanyika shehiani
humo.
Alisema, zipo mamlaka ikiwemo mahakama, ndio ambayo
inaweza kutoa adhabu ya kifo, ikiwa mshitakiwa atatiwa hatiani.
Alieleza kuwa, imezoeleka kuona wananchi
wanajichukulia sheria mikononi, mara wanapomkamata mtuhumiwa, jambo ambalo,
wajibu wao ni kumfikisha mbele ya vyombo vya sheria.
Wakili huyo wa serikali, alisema mahkama pekee
ndio ambayo kisheria imepewa nguvu za kisheria, kuondoa uhai wa mtu, ikiwa nae
amebainika kuua kwa maksudi.
‘’Imekuwa ni rahisi siku hizi, kuvunjwa kwa haki
za binaadamu ikiwemo mtuhumiwa kuuawa, jambo ambalo kisheria ni kosa la jinai,’’alifafanua.
Katika hatua
nyingine Wakili huyo wa serikali, alisema
kuwa chimbuko la haki za binaadamu, lilikuja baada ya vita vya kwanza na vya
pili vya dunia, ambapo haki nyingi zilivunjwa ikiwemo watu kuuliwa na kunyang’anywa
mali zao mbali mbali.
Alieleza kuwa baada ya hapo, mataifa yalikutana na kuunda tamko la haki za
binaadamu duniani, ili kila nchi iunge mkono kwa nafasi yake.
Aidha alifafanuwa kuwa, kwa upande wa Zanzibar kulikuwa na katiba ya kwanza 1963 ndani yake kulikuwa na haki za binaadamu, na kisha kuendelezwa kuingizwa kwa ile ya mwaka 1984, zikiwekwa kwenye sehemu ya tatu.
Nae Afisa
sheria kutoka Idara ya Katiba na Msaada wa
kisheria Zanzibar Salma Suleiman Abdulla, amesema mikutano hiyo ni muendelezo wa majukumu
ya Idara, katika kuifikia jamii yenye uwelewa wa sheria.
Alieleza
kuwa, kwa kushirikiana na wasaidizi wa sheria waliomo ndani ya shehia zao,
wanaweza kupata ufafanuzi wa changamoto zao, bila ya malipo.
Sheha wa
Mchakwe Fatma Khamis, alisema ziara ya watendaji wa Idara ya Katiba na Msaada
wa kisheria, ni muhimu kwa wananchi wake, katika kupata uwelewa.
Wananchi
wa Mwambe akiwemo Haku Mossi Haji, alisema wanakabiliwa na uvamizi wa ardhi,
hasa zinapokuja kampuni kwa uchukuaji wa rasilimali za ujenzi wa barabara.
Nae Kheir
Sheha Ali, alisema ipo mgogoro ya ardhi, ambayo inaweza kuepukika, ingawa
changamoto ni uwelewa wa jinsi gani ya kuidhibiti kisheria.
‘’Huku Mwambe
sisi tunavamiwa ardhi zetu, kisa hatuna nyaraka, ingawa tumeshaendesha kilimo
kwa zaidi ya miaka 50, jambo linalotupa wasi wasi,’’alisema.
Wakati huo
huo Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, imewataka wanafunzi wa skuli ya
sekondari ya Dk. Samia Suluh Hassan, kuhakikisha wanawahimiza wazazi wao, kuwapatia vyeti vya kuzaliwa.
Mikutano
hiyo ya wazi kwa wananchi, ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa upatikanaji
haki Zanzibar unaotekelezwa na Idara hiyo, ambapo kesho ni zamu za shehia zilizomo ndani
ya wilaya za Micheweni na Wete.
Mwisho







Comments
Post a Comment