MRAJISI WA NGOs: ‘ZAPONET’ JIPANGENI KUJITEGEMEA WENYEWE

 


 NA HAJI NASSOR, UNGUJA@@@@


MRAJISI wa asasi za kiraia Zanzibar Ahmed Khalid Abdulla, amesema mtandao wa wasaidizi wa sheria Zanzibar ‘ZAPONET’ ianze sasa kujipanga vyema kuhakikisha wanajiendesha wenyewe, na sio kutegemea wafadhili.

Mrajisi huyo aliyasema hayo leo Januari 25, 2026 ukumbi wa Malaria Mwanakwerekwe Unguja, wakati akiufungua mkutano mkuu wa kwanza wa mwaka ‘ZAPONET’, uliokuwa na malengo kadhaa, ikiwemo mapatio ya katiba na uwasilishaji wa ripoti za wanachama wao.

Alisema, ZAPONET ni muhimili muhimu kwa jumuia za wasaidizi wa sheria, lakini kikubwa kwa sasa ni kujipanga mapema, ili kujiendesha yenyewe na kutoa usaidizi kwa wanachama wao.

Alieleza kuwa, msingi wa wasaidizi wa sheria kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria kwa jamii bila ya malipo, inazingalia sana jumuia zao pamoja na mtandao huo, katika kuwajengea uwezo.

Alifafanua kuwa, ingawa kwa sasa wanaendelea kushikwa mkono na taasisi ya LSF, na kufanya vizuri katika utendaji wao wa kazi.

‘’Lazima niwapongeze sana wenzetu wa ‘LSF’ katika kuushika mkono mtandao wa ZAPONET, na kuwaomba kufanya hivyo, kwani wanufaika wakubwa ni jamii hasa wanyonge,’’alifafanua.

Katika hatua nyingine Mrajisi huyo, aliwataka viongozi wa ZAPONET kuendelea kushirikiana kwa karibu na jumuia zote 11 za wasaidizi wa sheria za Unguja na Pemba, ili jamii iendelee kunufaika na msaada wa kisheria.

Alieleza kuwa, haitoshi kwa wananchi kujua ofizi zao zilipo, bali kubwa waelewe nafasi yao, wakati wanapotafuta haki zao mbali mbali za kisheria.

Hata hivyo, aliziagiza jumuia za wasaidizi wa sheria, kuwa na mpango kazi ngazi ya shehia, katika kutoa elimu, msaada na ushauri wa kisheria kwa wananchi.

Hata hivyo, aliahidi kuendelea kuwa karibu na ‘ZAPONET’, ili kutatua baadhi ya changamoto zinazowakabili, ili kuhakikisha wanafikia malengo yao.

Wakati huo huo, alizipongeza asasi za kirai Zanzibar, kwa kuhubiri amani na mshikamano, kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka 2025.

Mapema Mwenyekiti wa ‘ZAPONET’ Nassor Hakim Haji, alisema uwepo wa mtandao huo, ni faraja kwa jumuiya hizo, kwani sasa wamekuwa na mfumo wa sauti moja.

Alifahamisha, jumuia hizo ambazo nyingi zao zimeanzishwa mwaka 2016, zilikuwa hazina pakukimbilia wanapokuwa na changamoto zao, ingawa uwepo wa ‘ZAPONET’ sasa kama zimezaliwa upya.

‘’ZAPONET ni mkombozi wa jumuiya za wasaidizi wa sheria za Unguja na Pemba, maana dira yetu ni kuwa chombo cha kuwaunganisha na kuwaweka pamoja wasaidizi wa sheria wote wa Zanzibar,’’alifafanua.

Nae Mkurugenzi wa ZAPONET Asia Abdul-salaam Hussein, amesifu kazi inayofanywa na jumuia za wasaidizi wa sheria, na kwamba inawapa nguvu wao kuendelea kuwajengea uwezo.

Aidha kuwa mkutani huo mkuu wa kwanza, pamoja na mambo mingine utaipitia na kuifanyia marekebisho katiba ya ZAPONET ili iwe na miundombiu rafiki.



Mwakilishi mwandamizi wa taasisi ya LSF amesema kwa Tanzania yote, wanafanyakazi na jumuia za wasaidizi wa sheria 184, ambapo kati ya hizo zipo 30 kwa Tanznania zilipoingia kwenye mradi huo wa majaribio na mbili zikiwa ni kutoka Zanzibar.

Alisema, kupitia mradi huo, wametengeneza fungu ambalo litaipa nguvu ZAPONET ili ifanyekazi zake kwa ufanisi, tokea kuanzishwa kwake mwaka 2019.

‘’Kwa Zanzibar zipo jumuiya ya wasaidizi wa sheria ya wilaya ya Kaskazini ‘A’ NAPAC na jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Micheweni ‘MDIPAO’ ambao ndio wanaoendesha mradi wa ‘Sauti ya mwanamke’ kwa majaribio,’’alifafanua.

Hata hivyo alisema anatamani kuona siku moja, jumuiya za wasaidizi wa sheria, inajiendesha wenyewe kuanzia vifaa, majengo na rasilimali fedha.

Akiwasilisha ripoti ya utendaji kazi, Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdalla, alisema kwa upande wa elimu waliwafikia wananchi 25,972, wakiwemo wanawake 11,741, wanaume 12,462, watoto 1474 na watu wenye ulemavu 294.

Ambapo kwa upande wa  msaada wa kisheria kwa mwaka huo wa 2025, walifanikiwa kuwapa watu 100, na waliwaandikia watu hati za kisheria 20 ambapo hati  za madai zilikuwa 16 na hati za majibu ni nne.



Kwa upande wake Asia Fadhil Makame kutoka Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Kaskazini ‘A’ NAPAC alisema, bado changamoto ni kuongezeka kwa matendo ya udhalilishaji ndani ya jamii.

                   Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’