WAJUMBE SHEHIA MVUMONI WAPIGWA MSASA ELIMU YA KISHERIA

 

 

NA MWANDISHI WETU, PEMBA

 WAJUMBE wa sheha wa shehia ya Mvumoni wilaya ya Chake chake, wameelezwa kuwa, suala la haki za binaadamu sio la kuomba, bali ni haki ya kila mmoja, kwa ubinaadamu wake.

 

Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilayani humo ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdall, aliyasema hayo leo Disemba 7, 2025 wakati akiwasilisha mada ya haki za binaadamu, kwa wajumbe hao, kwenye mafunzo ya siku moja.

 



Alisema, haki za binaadamu, ni haki zote anazostahiki mtu, kwa sababu ya kuwepo kwake duniani, ikiwemo uhai, matibabu, afya, elimu, utaifa na uzalendo.

 

‘’Niwaombe sana wajumbe wetu wa shehia ya Mvumoni, kwanza elimu hii mkawafikishie na wingine, maana haki za binaadamu ni zote,’’alieleza.



 


Akizungumzia faida za kufanya sulhu kwa kesi za madai kama vile, huduma za mke, watoto, migogoro ya ardhi, mirathi na madeni, alisema inaondosha visasi.

Alifahamisha, kuwa ndio maana, wamempeleka msaidizi wa sheria katika eneo lao, ili migogoro hiyo kabla haijafikishwa mbele ya vyombo vya sheria, kwanza wakutane na kuangalia ufumbuzi.

 

‘’Hapa tukumbushane kuwa, kesi za jinai kama udhalilishaji, wizi, dawa za kulevya, utoroshaji wa watoto na yanayofanana na hayo, yapelekwe Polisi moja kwa moja,’alifafanua.

 

Nae Msaidizi wa sheria shehiani humo, Haji Nassor Mohamed, ambae amehamishiwa hapo, akitokea shehia ya Wawi, alisema suala la msaada wa kisheria ni haki ya kikatiba.

 


Alieleza kuwa, sasa serikali inawatambua wasaidizi wa sheria, kupitia Sheria nambari 13 ya mwaka 2018, na kwamba wapo kwa ajili ya kuwahudumia wananchi bila ya malipo.

 

‘’Sisi wasaidizi wa sheria, tunaisaidia jamii, iwe ni elimu ya kisheria, msaada na ushauri wa kisheria tena bila ya malipo, na hasa kwa wale wasiokuwa na uwezo,’’alieleza.

 


Akifungua mafunzo hayo, Kaimu Mkuu wa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Pemba, Ali Salum Hamad, alisifu juhudi za ‘CHAPO’ katika kusambaaza elimu ya kisheria kwa jamii.

 

Alieleza kuwa, mfano uliooneshwa na Msaidizi wa sheria wa Mvumoni, ni vyema ukaenea katika shehia nyingine za Pemba, kwa mafunzo ya aina hiyo.

 


‘’Mafunzo haya naamini ni matunda ya kufanyakazi vyema kwa pamoja, baina ya uongozi wa shehia ya Mvumoni na CHAPO, jambo ambalo Idara inajivunia nalo mno,’’alifafanua.

 

Katika hatua nyingine, amewakumbusha wananchi wa Mvumoni na maeneo mingine, kuendelea kuwatumia wasaidizi wa sheria, kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa changamoto zao, za kisheria.

 



Wakichangia mada kwenye mafunzo, mmoja wa wajumbe hao Khamis Juma Mohamed, alisema mafunzo hayo yamewasaidia, kujua baadhi ya mambo ya kisheria.

 

‘’Kwa mfano nimeshajua tofauti baina ya Msaidizi wa sheria na Mwanasheria, kupata faida ya kufanya sulhu nje ya mahkama kwa kesi za majadi,’’alifafanua.

 

 Nae Asia Juma Khamis, alisema watamtumia vyema Msaidizi huyo wa sheria, ili kujua haki na wajibu wao kisheria.

 


Kwenye mafunzo hayo ya siku moja, mada tatu, ziliwasilishwa ikiwemo dhana ya msaada wa kisheria, haki za binaadamu na namna ya utatuzi wa migogoro wa ya madai nje ya mahkama.

                              MWISHO.

 

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’