SHEHIA YA MVUMONI YAPATA MSAIDIZI MPYA WA SHERIA
NA SAIDA ALI, PEMBA@@@@
MSAIDIZI mpya wa sheria shehia ya Mvumoni wilaya ya Chake chake Pemba, Haji
Nassor Mohamed, ameuomba uongozi wa shehia hiyo, kumpa kila aina ya uhirikiano,
ili kufanikisha majukumu yake.
Ameyasema hayo Novemba 29, 2025 alipokuwa akijitambulisha kwa wajumbe wa
sheha, mara baada ya kuhamishiwa shehia hiyo akitokea Wawi, kwa lengo la kutoa
elimu, ushauri na msaada wa kisheria bila ya malipo.
Alisema kuwa, kubwa analohitaji ni ushirikiano kuanzia kwa
sheha, wajumbe na wananchi wa Mvumoni, ili lengo la kuwahudumia wananchi
lifikiwe.
Alieleza kua, ataendelea kuwa tegemeo kwa wananchi wa
Mvumoni, kwani anaamini wapo ambao hawana uwelewa mpana, wa masuala ya kisheria.
‘’Kwanza nishukuru kwa kupokelewa, na ninachotaka kubwa zaidi
ni umoja, mshikamano na ushirikiano miongoni mwenu,’’alieleza.
Aidha Msaidizi huyo wa sheria, aliwakumbusha wajumbe hao wa
sheha, kutokubali kuzifanyia sulhu kesi za jinai na hasa za udhalilishaji, na
badala yake wawaelekeze wananchi kwenda mbele ya vyombo vya sheria.
Wakati huo huo Msaidizi huyo mpya wa sheria, alitumia fursa
hiyo, kuwaelezea wajumbe hao kuwa, kesi za jinai na madai, zinatofauti kubwa,
katika uendeshaji wake.
‘’Kwa kesi za madai, huwa baina ya mtu mmoja na mwingine, na
lazima anaelalamika aandike madai yake, ingawa kwenye jinai husimamiwa na ofisi
ya Mwendesha Mashtaka,’’alifafanua.
Mapema Kaimu sheha wa
Mvumoni Fatma Ali Khamis ameishukuru Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya
Chake chake ‘CHAPO’, kwa kuwapelekea msaidizi wa sheria, kwani ilikuwa ndio kilio
chao cha muda mrefu.
"Kuwepo kwa msaidizi huyu wa sheria shehiani mwetu, ni
jambo kubwa kwetu, kwani utatuzi wa migogoro sasa utakuwa wa kisheria, ni
tofauti na zamani tukitumia uzoefu tu,’’alisema.
Kwa upande wake Katibu wa sheha Khamis Mohamed na mjumbe wa shehiani humo Khamis Juma Mohamed walisema kuwa, ni jambo jema na faraja kupatiwa msaidizi huyo wa sheria.
Wakati huo huo, uongozi wa shehia hiyo, umekubaliana na
Msaidizi huyo wa sheria, kuendesha mafunzo wa siku moja, ya kuijengea uwezo kamati
hiyo, yanayotarajiwa kufanyika mwishoni mwa wiki hii.
Ambapo mada tatu zilizopendekezwa ni haki za binaadamu, nani
Msaidizi wa sheria pamoja na namna bora ya utatuzi wa migogoro ya mdai nje ya
mahkama.
MWISHO.





Comments
Post a Comment