WAGOMBEA CCM JIMBO LA CHAKE CHAKE, KUANZISHA WIKI YA MSAADA WA KISHERIA
NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
MGOMBEA Ubunge na Uwakilishi
jimbo la Chake chake, wamesema kama wakipata ridhaa ya wananchi, wataanzisha wiki
ya msaada wa kisheria jimboni humo, ili kuwasaidia wananchi, wenye changamoto
za kisheria.
Walisema, wanayodhamira ya dhati
kuhakikisha wananchi wa jimbo hilo, wanaondokana na changamoto za kisheria, kwa
kuanzisha wiki ya msaada wa kisheria, kila baada ya muda.
Wakizungumza na baadhi ya
watendaji wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’,
wakati walipofika ofisini hapo, walisema wanachosubiri ni ridhaa tu ya wananchi.
Wagombea hao walisema,
wamebaini kuwa, ipo haja ya kuongeza nguvu ya kutoa elimu, msaada na ushauri wa
kisheria kwa wananchi, na hilo litawezekana kwa kuanzisha wiki ya msaada wa
kisheria.
Mgombea Uwakilishi
Abdulla-wahabi Said Abubakar, alisema kwa kushirikiana na viongozi wenzake, na
baada ya kukaa na uongozi wa ‘CHAPO’, azma hiyo wanayo.
Alieleza kuwa, kama Idara ya
Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, inayo wiki ya msaada wa kisheria kila
mwaka, nalo jimbo la Chake chake, litaanzisha ya kwake kwa madhumuni yanayofanana.
Alisema, wapo wananchi wenye
changamoto za kisheria kama vile watu wenye ulemavu, wazee, wanawake na hata vijana,
hivyo kupitia wiki ya msaada wa kisheria, watapata ufumbuzi.
‘’Leo (jana), tuliseme tuitembelee
‘CHAPO’ na kufanya mazungumzo na baadhi ya watendaji na kisha kuonesha hisia
zetu za kufanyakazi nao hapo baadae, kwa lengo lile lile la kuwasaidia
wananchi,’’alifafanua.
Katika hatua nyingine, Mgombea
huyo uwakilishi, alisema atakaa na viongozi wenzake, kuona CHAPO wanaisaidia
baadhi ya vitendea kazi, ili iwahudumie wananchi kwa ufanisi.
Nae Mgombea Ubunge wa Jimbo
hilo Nassor Said Nassor ‘Maro’, alisema hataki kusikia hapo baadae, kuwa kuna
mwananchi ndani ya jimbo hilo, analalamikia kukuosa msaada wa kisheria.
Alisema, anaifahamu vyema ‘CHAPO’
na utendaji wake wa kazi katika sheria za jimbo la Chake chake, hivyo kama
akipata ridhaa, ataiunga mkono.
‘’Lengo letu ni kuona
wananchi wale ambao wameshakata tamaa ya kukosa haki zao, waliomo jimbo la
Chake chake, sasa wanasimama wima na kuzipata,’’alisema.
Aidha ‘Maro’, aliwaomba
watendaji hao wa CHAPO kuhakikisha, wanakuwa waalimu kwa wingine, katika namna
ya kutunza amani, iliyopo.
‘’Amani ndio yetu, kabla,
wakati na baada ya uchaguzi, hivyo wasaidizi wa sheria, hilo endeleeni
kulihubiri na muwafikishie na wingine,’’alifafanua.
Mapema Mkurugenzi wa ‘CHAPO’ Mwalimu
Mohamed Hassan Abdalla, aliwaahidi wagombea hao, kuendelea kufanya nao kazi,
kwa maslahi mapana ya wananchi.
Alisema, hata wasaidizi wa
sheria wanahitaji amani katika kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria,
hivyo atahakikisha, ujumbe huo anawafikishia na wingine.
Nao wasadizi wa sheria Jimbo
la Chake chake, Wahida Kombo Khamis na Abeda Adi Seif, waliwatakia kila la
kheir wagombea, hao na kurudi tena ofisini hapo.
Kwa upande wake, msaidizi wa
sheria shehia ya Wesha Khadija Said Khalfan, aliwashauri wagombea, hao kuendelea
kuhubiri amani, ili uchaguzi ufanyike kwa utulivu.
Mwisho

Comments
Post a Comment