BODI CHAPO YANG'AKA UTORO, UVIVU WA WASAIDIZI WA SHERIA
NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WAJUMBE wa Bodi wa Jumuiya ya Wasaidizi wa
sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’, wamesema hawataki kusikia tena
kuwa, wapo wasaidizi wa sheria, wamekuwa wavivu wa kufanya wajibu wao na kudharau
vikao vinavyoitwishwa.
Walisema, kila mmoja anajua kuwa, CHAPO kama ilivyo wa
jumuiya nyingine, ni eneo la kujitolea, sasa kama wako tayari kuendelea nayo,
wahakikishe wanaendelea kuwahudumia wananchi.
Mwenyekiti wa Bodi hiyo Safia Saleh Sultan, alisema wakati
wanaomba kuingia kwenye sekta ya wasaidizi wa sheria, suala la kujitolea na
kujitoa, ndio kigezo kikuu.
Alieleza kuwa, leo anashangaa kusikia kuwepo wasaidizi wa
sheria ndani ya ‘CHAPO’, wamekuwa wavivu wa kutoa elimu na msaada wa kisheria
kwa jamii.
Alifahamisha kuwa, uvivu wao wa kufanyakazi na jamii,
inaweza kupoteza mwelekeo kwa wananchi, na kuiangusha CHAPO, jambo ambalo akiwa
Mwenyekiti, hataki kulisikia.
‘’Kila mmoja kuanzia sasa afanye wajibu wake, ambao ni kutoa
elimu, ushauri na msaada wa kisheria, kama ilivyokuwa sehemu ya vigezo vya kuwa
msaidizi wa sheria hapo awali,’’alifafanua,
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo wa Bodi, aliwataka
wajumbe wa kamati tendaji ya CHAPO, kujenga ushirikiano wa utendaji miongoni mwao,
ili wanachama wasiyumbe.
‘’Kamati tendaji ikiwa kitu kimoja, katika kutekeleza maagizo
ya bodi pamoja na kuifuata katiba ya CHAPO, hata wale wanachama wenu watawaheshimu
na kutekeleza wajibu wao,’’alisema.
Hata hivyo, aliwataka watunza fedha, kuhakikisha wanaweka
ripoti zao sawa, na kufuatilia michango ya wanachama, ukiwemo ule wa kila mwisho
wa mwezi.
Nae mjumbe wa bodi hiyo Kassim Ali Omar, alisema umoja na
mshikamano wao, ndio utakaoifikisha mbali CHAPO, na kujenga uaminifu, kwa
wananchi wa Chake chake.
‘’Wananchi wa Chake chake, wanaitegemea mno CHAPO kufikisha
malalamiko yao ya kisheria, na kupatiwa ufumbuzi wa haraka,’’alifafanua.
Hata hivyo mjumbe huyo, nae aliwataka viongozi wa jumuiya
hiyo, kuhakikisha kila mwanachama anafanyakazi yake kwa nia njema, ili kuwasaidia
wananchi, hasa wasiokuwa na uwezo.
Kwa upande wake mjumbe Adam Abdalla, alisema hatojiskia
vyema, CHAPO kufa yeye akiwa mjumbe wa bodi ya wadhamani.
Alifafanua kuwa, kama kuna mwanachama anajiona hawezi
kuendelea na CHAPO akae pembeni, ingawa anaetaka kuendelea, afanye kazi zake bila
ya kusimamiwa.
‘’Inawezekanaje msaidizi wa sheria, anakaa ndani ya shehia,
mwezi mzima hajafanya kazi ya kutoa elimu wala msaada wa kisheria, lazima
ajitathmini,’’alifafanua.
Mapema Mkurugenzi wa ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdalla, alikiri
kuyapokea maagizo ya bodi na kuyafanyiakazi, ili jumuia hiyo iendelee kuwategemeo
kwa wananchi.
Aliwashukuru wajumbe hao, kwa kuwapa mwanga wa kufikia mafanikio
ya CHAPO, kwani alikiri kuwa, kulikuwa na baadhi ya wanachama, wamesinzia
kikazi.
Mkurugenzi Fedha wa CHAPO Riziki Hamad Ali, alisema amekuwa
akijitahidi kuweka kumbu kumbu sawa, hasa malipo, ingawa utoro wa wajumbe, ndio
changamoto.
Mratibu wa CHAPO Fatma Hilali Salum, alisema changamoto
kubwa, ni wanajumuia kudharau vikao, na kusababisha wingine, kukosa maagizo na
mipango inayoamuliwa.
‘’Wapo wanachama ni watoro, mnaweza kuamua jambo yeye hajui
na wala haulizi, wakati wa utekelezaji ndio anaanza kulalamika,’’alifafanua.
Msaidizi wa sheria shehia ya Wesha Khadija Said Khalfan,
alisema vikao kama hivyo, vinavyowahusisha wanachama na wajumbe wa bodi ni muhimu,
katika kuiendeleza CHAPO.
Hata hivyo, aliwakumbusha wenzake, kuendelea kutoa michango
yao, wanapokwenda kwenye mikutano na mafunzo, kupitia CHAPO.
CHAPO imekuwa na utaratibu wa kukutana na wanachama wake,
kila mwisho wa mwezi, ili kupokea ripoti za utendaji kazi, pamoja na
kuwasilisha ripoti ya fedha.
Mwisho
Comments
Post a Comment