WASAIDIZI WA SHERIA WAWAREJESHA WANAFUNZI WATORO MASOMONI

 


NA MWANDISHI WETU, CHAPO@@@@

FAMILIA mbili za shehia za Gombani na Ziwani wilaya ya Chake chake, wamewashukuru wasaidizi wa sheria wilayani humo, kwa kufanikiwa kuwarejesha watoto wao masomoni, baada ya kukatisha kwa zaidi ya miezi minne.

Walisema tayari walishashindwa kuwanasihi na kuwatisha watoto wao ili kurejea masomoni, ingawa hawakufanikiwa, na kuamua kuwatafuta wasaidizi hao wa sheria.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti wazazi hao, walisema walitumia mbinu kadhaa ikiwemo kuwapeleka kwa askari wa ulinzi shirikishi, ingawa hakuwafanikiwa.

Walisema, waliwatumia askari wa shehia ili kuwanasihi na kisha kuwatisha, ingawa walikuwa wanarejea masomoni kwa muda, kisha kuatisha tena.

Mzazi Hassina Khamis Said, alisema aliamuwa kuwatafua wasaidizi wa sheria na haraka walifika kijijini kwao Semeweni, shehia ya Ziwani na kuwakabidhi kijana wake.

Alisema, walifika na kuzungumza nae, na sasa kijana wake amerejea masomoni skuli ya Mbuzini kwa ajili ya kujiandaa na mitihani ya darasa la saba.

‘’Mtoto wangu alishakaa nyumbani kwa zaidi ya miezi mitatu, alikuwa anaendelea kuvuna zao la karafuu na tayari alishanunua simu, na ameshaniambia zaidi ya mara moja kuwa hatorudi skuli, ingawa sasa nashukuru,’’alisema.

Mzazi huyo, alisema kwanza anawashukuru wasaidizi hao wa sheria, kwa kufuata wito wake wa haraka na kisha, kufanikiwa kumrejesga kijana wake masomoni.

‘’Kwa sasa anaamka na kijihimiza mwenyewe kwenda masomoni, lazima niwashukuru wasaidizi wa sheria kutoka CHAPO, kwa kazi hii,’’alisema.



Nae mzazi Saada Abdalla Nassor wa shehia ya Gombani, alisema mtoto wake, aliacha masomo ya darasa la 10, kwa zaidi ya miezi sita.

‘’Baada ya kusikia kuwa, kuna wasaidizi wa sheria, niliwatafuta na niliwakabidhi mtoto wangu na sasa amesharejea skuli ya Ng’ambwa,’’alieleza.

Mama huyo, alisema kwa sasa ataendelea kuwa karibu na wasaidizi hao wa sheria hadi hapo, mtoto wake atakapomaliza elimu yake ya lazima.

Msaidizi wa sheria Fatma Hilali Salum, aliyefanikiwa kumrejesha mwanafunzi wa darasa la saba skuli ya Mbuzini, alikiri kutumia mbinu za hali ya juu.

Alieleza kuwa, baada ya kupata taarifa na wito ya mzazi huyo, jioni yake akiwa na baadhi ya wasaidizi wa sheria walifika nyumbani kwa mtoto huyo, na kumnasihi na sasa amerejea masomoni.

‘’Watoto wingi ambao wamekatisha masomo ni wale ambao ndo za wazai wao, zimekatika, jambo ambalo mzigo wa malezi humuangukia mama pekee,’’alisema.





Nae msadizi wa sheria Haji Nassor Mohamed, aliyemrejesha mwanafunzi wa kidato cha pili skuli ya Ng’ambwa, alisema nao wazazi wake, wameshaachana, na mama pekee kushindwa malezi.

‘’Wajomba wake wameshaingia kwenye nasaha, waalimu, Polisi na majirani lakini mtoto alishindikana, hadi nilipofika na sasa amerejea skuli,’’alieleza.

Aidha Msaidizi huyo wa sheria, alipofika skuli ya Ng’ambwa alioneshwa orodha ya wanafunzi zaidi ya 35 wa madarasa tofauti, waliokatisha masomo skulini hapo.

Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdalla, aliwataka wasaidizi hao wa sheria, kuendelea kuisaidia jamii, kwani ndio tegemeo lao.

Mkuu wa wilaya ya Chake chake Mgeni Khatib Yahya, aliwataka wazazi na masheha kuendelea kushirikiana na wasaidizi wa sheria, ili kutatua changamoto kadhaa.

   Wakati hayo yakifanyika, upande mwingine wizara ya Elim una Mafunzo ya Amali, imeongeza shilingi bilioni 11.5 kwa mwaka 2021/2022 hadi kufikia shilingi bilioni 33.4 kwa mwaka 2024/2025.

Aidha ufaulu wa wanafunzi vipawa na mchepuo kwa mitihani ya darasa la saba, umeongezeka kutoka asilimia 5.5 mwaka 2020 hadi asilimia 27.5. kwa mwaka 2023.

                   Mwisho   

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’