‘YALETENI MALALAMIKO YA KUVUNJIWA HAKI ZENU TUME’
NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WANANCHI
wa shehia ya Mjananza wilaya ya Wete Pemba, wameshauriwa kuyafikisha malalamiko
yao ya kisheria, yanayohusu uvunjwaji wa haki zao, kwa Tume ya Haki za
Binaadamu na Utawala Bora, ili kupata ufafanuzi.
Hayo yalieleza
leo August 14, 2025 kijiji cha Mlalashi shehiani humo, na Mwanasheria
kutoka Tume hiyo Pemba, Mohamed Massoud, wakati akielezea majukumu ya taasisi
hiyo, kwenye mkutano wa wazi, ulioandaliwa na Idara ya Katiba na Msaada wa kisheria
Zanzibar.
Alisema,
moja ya jukumu la tume hiyo, ambayo ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni
kupokea, kusikiliza malalamiko mbali mbali ya uvunjifu wa haki wa binaadamu,
tena bila ya malipo.
Alieleza kuwa,
ofisi yao ambayo kwa sasa ipo Chake chake, inawakaribisha wananchi hao na wingine,
ili kufika na kulalamikia, ikiwa wanaona kuna haki yao, iliyovunjwa.
‘’Kwa mfano
umevunjiwa nyumba yako, kwa kupisha mradi wa kijamii kama barabara au ujenzi wa
skuli na hakuna dalili ya kulipwa fidia, njoo na tutashirikiana,’’alisema.
Katika hatua
nyingine, Mwanasheria huyo, aliwataka wananchi hao, wasiwe chanzo za kuvunjiana
haki miongoni mwao, ikiwemo kuzifanyia sulhu kesi za jinai.
‘’Imekuwa ni
kawaida, ikiwa kumetokezea ubakaji, hapo familia hukaa na kuanza kutafuta
sulhu, ikiwemo kuwafungisha ndoa waliodhalilishana, jambo ambalo ni kosa jingine,’’aliafafanua.
Hata hivyo,
aliipongeza Idara ya Katiba na Msaada wa kisheria kwa kushirikiana na UNDP,
kufanikisha mikutano hiyo katika baadhi ya shehia teule.
Kwa upande
wake, Afisa sheria kutoka Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar Salma Bakar
Abdulla, alisema mikutano hiyo ya wazi, lengo kuu ni kuwafikia wananchi na
kuwafundish maana, chimbuko na zilikoanzia haki za binaadamu.
Alisema,
imebainika kuwa, wananchi wamekuwa wakivunjiana haki za binaadamu, iwe kwa
kujua ama kutokuelewa, na ndio maana, Idara hii na mshirika wake UNDP, imeamua
kuwafikia wananchi moja kwa moja.
‘’Wananchi
ni vyema fursa za mikutano kama hii, mkazitumia kwa kuuliza, kutaka ufafanuzi
juu yao, ikiwa ni nachangamoto kadhaa, ikiwemo vyeti vya kuzaliwa, migogoro ya
ardhi na suala la fidia,’’alifafanua.
Mkuu wa
divisheni ya Katiba na Msaada wa Kisheria Pemba, Bakari Ali Omar, alisema hata
baada ya kumalizika kwa mikutano hiyo, wananchi wanatakiwa kuyafikisha malalamiko
yao kwa wasaidizi wa sheria, ambao wamo katika shehia zao.
Alisema,
kupitia kwa masheha unaweza kuwapata watendaji hao, ambao moja ya jukumu lao ni
kutoa elimu, ushauri na msaada wa sheria bila la malipo.
Akifungua mkutano
huo, sheha wa Mjananza Hamad Said Ali, alisema ujio wa wanasheria hao katika
shehia yake, ni jambo jema, maana uwelewa wa sheria ni mdogo.
‘’Wananchi
wa shehia hii, wingi wao uwelewa wa haki zao za kisheria uko chini, ingawa
naamini mikutano kama hii, huwaamsha na kuwapa uwelewa zaidi,’’alifafanua.
Akitolea ufafanuzi
suala lililoulizwa na wananchi, sheha huyo alisema ili mwananchi aingie kwenye
mpango pensheni jamii, sio kwa ukongwe wake, bali vitambulishi vionyeshe
amefikia miaka 70.
Idara ya
Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, ikishirikiana na ofisi ya Mwanasheria mkuu,
Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora, pamoja na wasaidizi wa sheria, wameshawafikia
wananchi wa shehia nane.
Mwisho
Comments
Post a Comment