IDARA YA KATIBA NA MSAADA WA KISHERIA YAWAALIKA WANANCHI WAWI ELIMU YA KISHERIA LEO HII

 

 

NA HAJI NASSOR, PEMBA

WANANCHI wa shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake, wametakiwa kuitumia fursa ya kuhudhuria mkutano maalum wa elimu ya kisheria, ulioandaliwa na Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, unaotarajiwa kufanyika jioni hii ya leo shehiani humo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Mkuu wa Divisheni ya Idara hiyo Pemba Bakari Omar Ali, alisema mkutano huo, ni maalum kwa ajili ya wananchi hao, ili kuwapa elimu na msaada wa kisheria bila ya malipo.

Alisema, mkutano huo ambao utafanyika eneo la Kwa gerei Wawi (Kwa Ali Haji) majira ya saa10:00 jioni, ni sehemu ya utendaji wa kazi wa kawaida wa Idara hiyo, katika kuhakikisha jamii inapata muelekeo wa kutambua haki na wajibu wao kisheria.

Alieleza kuwa, zipo njia kadhaa za wananchi kujua haki zao za kisheria, moja wapo ni kuwapelekea wataalam wa sheria ndani ya shehia, na kuelezea changamoto zao za kisheria.

‘’Mkutano huu ambao unatarajiwa kufanyika jioni hii shehia ya Wawi ni maalum, ili kuona wanapata uwelewa, lakini pia kuuliza na kutoa changamoto zao za kisheria,’’alifafanua.

Mkuu huyo wa Divisheni ya Idara ya Katiba na Msaada wa kisheria, alisema watalamu kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, watendaji wa Tume ya Haki za Binaadamu na Utawala Bora pamoja na wasaidizi wa sheria wa Chake chake watajumika pamoja.


‘’Wataalamu hawa watahakikisha kila mwananchi atakaefika kwenye mkutano wa leo, na akiwa anajambo lolote la kisheria atauliza na kupata jawabu papo hapo,’’alisema.

Katika hatua nyingine, aliwahimiza wananchi hao, kuitumia fursa hiyo, kwani kinyume chake wakiwafuata baadhi ya wanasheria watahitaji fedha nyingi, ili kusikiliza na kuchambua changamoto zao.

Mapema sheha wa Wawi Khamis Mohamed Khamis, alisema matayarisho yote kwa ajili ya mkutano huo mkubwa wa wazi, yamekamilika.

Alisema, baada ya kupokea taarifa hiyo kutoka Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, alishakutana na kamati yake, na wameshatoa taarifa kwa wananchi.

‘’Niliwatumia wajumbe wangu kutoa taarifa kwa wananchi wa makundi kadhaa, kama ya watu wenye ulemavu, watumishi wa umma, wakulima, waalimu wa vyuo vya qur-an na wanamichezo,’’alifafanua.

Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdalla, alisema hiyo ni heshima kubwa kwa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria kuwapa fursa ya kuandaa mkutano huo.

Msaidizi wa sheria shehia ya Wawi, Fatma Hilali Salim, aliwakumbusha wananchi wa shehia hiyo, kufika kwa wingi kwenye mkutano huo, ili kupata ufafanuzi wa changamoto zao za kisheria.

Mjumbe wa sheha Nassor Rashid Said na Katiba wa sheha Sham Haroub Said, waliipongeza Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, kwa uamuzi wake wa kuandaa mkutano huo.

Mikutano kama hiyo, inatarajiwa kufanyika katika shehia za wilaya ya Mkoani, Wete na Micheweni.

                       Mwisho   

 

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’