WANANCHI 422,908 WAFIKIWA KAMPENI YA MSAADA WA KISHERIA YA MAMA SAMIA

 




NA HAJI NASSOR, UNGUJA@@@@

WANANCHI 422,908 wakiwemo wanawake 209,185 na wanaume 213,723 wamefikiwa na elimu na msaada wa kisheria, kupitia kampeni ya msaada wa kisheria ya Mama Samia, iliyomalizika hivi karibuni Zanzibar.

Kampeni hiyo, iliendeshwa katika mikoa yote mitano ya Zanzibar, inayojumuisha wilaya 11, ambapo miongoni mwao kati ya waliofikiwa, ni wanawake, watu wenye ulemavu, vijana, wazee na wanafunzi.

Hayo yalielezwa leo Julai 16, 2025 na Mwanasheria Mkuu wa serikali ya Zanzubar, Mwinyi Talib Haji, kwenye hutuba yake, iliyosomwa kwa niaba yake na Naibu Mwanasheria mkuu Shaaban Ramadhan Abdalla, kwenye kilele cha maadhimisho ya jukwaa la tano, kilichofanyika Michenzani Mall.

Alisema, kwa takwimu hiyo na kazi iliyofanywa, inadhahirisha umoja na mshikamano, unaosababishwa na uwepo wa Muungano wa Tangayika na Zanzibar.

Alieleza kuwa, serikali inafurahishwa mno kuona wananchi walio wengi na wanyonge, wanaendelea kupata msaada, ushauri na elimu ya kisheria bila ya malipo.

‘’Kwa hakika, uwepo wa kampeni hii, ni faraja kwa serikali zote mbili, maana wananchi walio wengi wamekuwa wakikata tamaa, kupata haki zao, ingawa kampeni kama hizi, husaidia kwa wananchi hao kupata haki zao,’’alieleza.



Katika hatua nyingine, Mwanasheria huyo Mkuu wa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, alisema wakati wa kampeni hiyo, ipo migogoro 749 ilipokelewa na 259 ikiwemo ya ardhi, mirathi, ndoa, ajira na talaka ilipatiwa ufumbuzi papo hapo.

Aidha, aliipongeza Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar, chini ya Mkurugenzi wake Hanifa Ramadhan Said, kwa kuendelea kusimamia vyema upatikanaji wa haki.

Hata hivyo, aliipongeza UNDP na taasisi ya LSF, kwa kuendelea kusaidia upatikanaji wa haki Zanzibar, jambo linaloleta faraja.

Mapema Mkurugenzi wa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar Hanifa Ramadhann Said, akiwasilisha maazimio ya jukwaa hilo kwa mwaka jana, alisema yapo ambayo yameshaanza kutekelezwa, ikiwemo azma ya kuanzishwa kwa mfuko wa wasaidizi wa sheria.



Azimio jingime alisema, ni serikali na wadau wingine, kutenga bajeti maalum kwa ajili ya kuendelea majukwaa na wiki ya msaada wa kisheria, jambo ambalo linaendelea kutekelezwa.

Alifahamisha kuwa, azimio jingine ni kuweka mazingira rafiki ya upatikanaji wa elimu, kwa jumuiya, taasisi za msaada wa kisheria hasa suala la uandishi wa miradi, ili kurahisisha upatikanaji wa fedha za kujiendesha.

‘’Lakini kupitia azma hii, niziombea hata jumuiya ya wasaidizi wa sheria zote kutoka wilaya 11, zihakikishe zinawasilisha hadithi za mafanikio kwetu, kwa ajili ya kuziingiza kwenye kitabu maalum,’’alifafanua.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka taasisi ya LSF ambae ni Afisa Miradi Mwandamizi Bakar Hamadi, alisema wataendelea kuinga mkono Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, katika kuhakikisha jamii, inapata uwelewa na haki zao.




Alieleza kuwa, kwa sasa ‘LSF’ inaendesha mradi wa ‘sauti ya mwanamke’ ambao umejikita katika mapambano dhidi ya ukatili wa wanawake, watoto na watu wenye ulemavu.

‘’Kwa mradi huu, kwa sasa unaendeshwa kwenye taasisi mbili za Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Kaskazini Unguja ‘NAPAC’ na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Micheweni ‘MIDIPAO’, kama eneo la majaribio, ili baadaae inaweza kuzifikia taasisi zote.







Mapema akiwasilisha mada ya nafasi ya ufuatiliaji na tathmini katika kuimarisha upatikanaji wa haki,  Dk. Skujua Omar Hamdani, alisema moja ni kujua mafanikio na changamoto za mradi husika.

Baadhi ya wachangiaji mada hiyo, walisema ufuatiliaji na tathmini ndio kioo cha mradi, ili kujua kuwa wamefanikiwa wapi, na wamekosea eneo gani.

Katika jukwaa hili la tano la mwaka la msaada wa kisheria Zanzibar, ujumbe wa mwaka huu ni ‘Ufuatiliaji na Tathimini husaidia kuimarisha ubora na ufanisi na huduma za msaada wa kisheria Zanzibar’.

                 Mwisho    

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’