WANAFUNZI JIFUNZENI KUSEMA ‘NO’ MSIDHALILISHWE

 



 NA MWANDISHI WETU, PEMBA@@@@

WANAFUNZI wa skuli ya msingi na sekondari ya kiislamu ya Amini, iliyopo Wesha wilaya ya Chake chake, wametakiwa kujifunza kusema hapana, wanapoona kuna ishara za wao kutaka kudhalilishwa.

Ushauri huo, umetolewa leo Julai 14, 2025 na Askari shehia Khamis Ali Khamis, wakati akizungumza na wanafunzi hao, kwenye shamra shamra za wiki na jukwaa la msaada wa kisheria, mkutano ulioandaliwa na Jumuiya ya wa saidizi wa sheria wilaya ya Chake chake ‘CHAPO’ na kufanyika skulini hapo.



Alisema, wasiwe rahisi mno wanapoona kuna viashiria vya udhalilishaji, hivyo wajifunze kwa vitendo neno la kukataa, ili kujikinga na madhara makuwa zaidi.

‘’Niwaombe leo mkutano huu wa wazi ulioandaliwa na wenzetu CHAPO, na tukiwa ndani ya wiki na jukwaa la msaada wa kisheria, ninawaomba mjifundishe kusema hapana, mkihisi mazingira hayako salama,’’alisema.

Aidha, aliwataka wanafunzi hao, kuchukua muda mkubwa wa kujisomea, kuliko jambo jingine lolote.

Nae Msaidizi wa sheria wa shehia ya Wesha Khadija Said Khalfan, aliewataka wanafunzi hao, wanapokuwa na changamoto za kisheria, wasisite kuwatumia wasaidizi wa sheria, kupata ufumbuzi bila ya malipo.



Alisema, karibu kila shehia, anakuwepo msadizi wa sheria mmoja, na kwa kuanzia unaweza kumfika sheha na kurahisisha upatikanaji wa watu hao.

‘’Sisi tupo kishehia, na tuko chini ya sheha, sasa wewe mwanafunzi ukiwa umekumbana na mgogoro hata wa udhalilishaji, tutafute tusaidiane,’’alisema.

Mapema Msaidizi wa sheria mwalika kutoka shehia ya Wawi Haji Nassor, aliwataka wanafunzi hao, kuwauliza wazazi wao, ikiwa wanavyeti vya kuzaliwa ama laa.

‘’Ikiwa mzazi atakuambia huna, mwambie anzie kwa sheha na kisha atafika wilayani, kwa ajili ya kupata haki yako hiyo ya lazima,’’alisema.



Hata hivyo, alisema cheti cha kuzaliwa, kwa sasa ni jambo la lazima, kutokana na umuhimu wake, hasa kwa wanafunzi, ikiwemo kuombea mikopo.

Akifunga mkutano huo, Mwalimu Mkuu wa skuli hiyo Juma Jumbe, aliishukuru ‘CHAPO’, kwa kuamua kuwafikia skulini hapo.



Alieleza kuwa, mikutano kama hiyo, inasaidia kuwapa uwelewa wanafunzi, juu ya haki, wajibu wao kisheria.


Wakati huo huo Msaidizi wa sheria jimbo la Chake chake Riziki Hamad Ali, aliwasisitiza wanafunzi wa skuli ya msingi ya Alswadiq, kutojihusisha na vitendo viovu, kwani havina mwisho mwema kwao.


CHAPO, kwa sasa imo kwenye shamra shamra za jukwaa na wiki ya msaada wa kisheria, baada ya kuzinduliwa na Julai 14, 2025 na Waziri wa Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman.

                     Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’