CHAPO: 'WAZAZI ONGEZENI ULINZI KWA WATOTO KIPINDI HICHI CHA MAPUMZIKO'

 

NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

MKURUGENZI wa Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdalla, amewataka wazazi na walezi, kuwa makini na kufuatilia nyenendo za watoto wao, kwa kukinga na majanga kama ya uudhalilishaji, hasa kipindi hiki cha mapunziko ya masomo.

Alisema, wahalifu waliowengi wamekuwa wakijisogeza na maeneo ya watoto wanamopenda kucheza cheza, hivyo ni vyema kwa wazazi na walezi wakaimarisha ulinzi mara dufu.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi leo Novemba 15, 2024, Mkurugenzi huyo, alisema wakati huu wa skuli zikiendelea na mitihani ya taifa, kundi kubwa la watoto wapo majumbani, hivyo ni vyema ulinzi ukaimarishwa.

Alieleza kuwa, wadhalilishaji wanaweza kujichanganya na watoto wakiwa kwenye michezo mbali mbali, hivyo ni wajibu ulinzi dhidi yao, ukaongezwa.

‘’Nitowe wito na tahadhari kwa wazazi na walezi, katika kipindi hiki wakiwa watoto hawaendi masomoni, na kutawanyika mtaani hovyo hovyo, ni kuongeza ulinzi, ili tusiwape nafasi wahalifu,’’alieleza.

Mkurugenzi huyo wa ‘CHAPO’ alifafanua kuwa, wazazi wasipendelee kuwaachia watoto kwa watoto wenzao, na badala yake, hali ikiruhusu awepo mtu mzima.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi huyo, alisema hata ndani ya majumba ni vyema kila mmoja, akawa mlinzi kwa mwenzake, maana zipo kesi za baba kumdhalilisha mtoto wake.

‘’Kesi hadi mahkamani zimeshafikishwa kwa baba, kaka, mjomba na ami kumdhalilisha mtoto wake, sasa ulinzi uimarishe ndani ya nje,''alishauri.



Hata hivyo aliwataka wasaidizi wa sheria wilayani humo, wanapokutana na jamii, kulieleza hilo ili tahadhari hiyo ichukuliwe kwa upana wake.

Sheha wa shehia ya Wesha Haji Mohamed Ali, aliwataka waratibu wa shehia, kukutana na watoto waliomo ndani ya shehia zao, ili kuwapa tahadhari hiyo.

Katibu wa sheha, shehia ya Wawi Sham Haroub Said, aliwakumbusha watoto, kwenda madrassa na kurudi kwa kundi, ili isiwe rahisi kwa mdhalilishaji, kutimiza malengo yake.

‘’Njia nyingine baada ya wazazi na walezi kuimarisha ulinzi, ni watoto wasipendelee kwenda mmoja mmoja, na wafuatane wanapokwenda na kurudi masomoni,’’alishauri.

 Kwa upande wake Katibu wa kamati ya kupambana na vitendo vya udhalilishaji wilaya ya Chake chake, Rashid Said Nassor, aliitaka jamii, kuendelea kuwalea watoto katika misingi yenye maadili, ili wajiepushe na kujiingiza kwenye vitendo vibaya.

‘’Ni kweli skulini nyingi zimeafungwa na watoto wako mtaani, lakini kwanza ni tahadhari kwao na wadhalilishaji, pili tuendelee kuwapa elimu ya kujitambua, ili wawe raia wema,’’alipendekeza.

Mkuu wa Mkoa wa kusini Pemba Mattar Zahor Massoud, aliendelea kuwataka masheha kutozitia mkono kesi za udhalilishaji, na badalayake wazifikishe mbele ya vyombo  vya sheria.

‘’Sheha yeyote atakaebainika kuziingilia kesi za udhalilishaji, kwanza hana kazi pili vyombo ya sheria vitakuwa vinamuhusu kwa njia moja ama nyingine,’’alieleza.

Mwanaharakati wa haki za wanawake na watoto Pemba Tatu Abdalla Msellem, aliwataka akinababa kusaidia malezi ya watoto, na sio kumuachia mwanamke kwa kisingizio cha kutafuta maisha.

Mjumbe wa baraza la watoto shehia ya Wawi Omar Mohamed Hassan na mwenzake wa Wesha Asha Taimur Hussein, walisema bado adhabu kwa wanaowadhalilisha watoto ni ndogo.

‘’Ndio maana kila siku, tunaripotiwa kubakwa, kulawitiwa na kufanyiwa ukatili wa kipigo, maana wanaotiwa hatiani, hawafungwi kifungo kirefu kama sheria ilivyo,’’walisema.

Akiwasilisha hutuba ya bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024 Wiziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Riziki Pemba Juma, alisema wameshaandaa mpango kazi mpya wa kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji kwa wanawake na watoto.

Alifahamisha kuwa, mpango huo (NPA-VAWC wa mwaka 2023/2028), unalengo la kuhamasisha na kuelimisha jamii, juu ya kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto katika ngazi zote.

Jingine alisema ni kuandaa Sera ya Maendeleo ya Jamii, pamoja na miongozo ya utoaji wa huduma za maendeleo ya jamii, kuratibu na kuhamasisha utekelezaji wa ahadi za nchi juu ya kizazi chenye usawa pamoja na kuhamasisha jamii kuimarisha malezi ya pamoja, yenye lengo la kuwatenga na vitendo viozuvu.

  Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’