MAMIA WAMZIKA MKURUGENZI 'CHAPO' SALAMU KILA KONA ZAMIMINIKA
NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
WASAIDIZI
wa sheria wilaya ya Chake chake, wamesema wamepokea salamu za pole kutoka,
maeneo kadhaa hapa nchini, kufuatia kifo cha aliyekuwa Mkurugenzi wao, Nassor
Bilali Ali, kilichotokea Augost 7, kisiwani Pemba.
Akizugumza na
waandishi wa habari, Mratibu wa Jumuiya hiyo Mohamed Hassan, alisema miongoni
mwa salamu hizo ni kutoka Afisi ya Rais, Katiba, Sheria na Utawala Bora Zanzibar.
Salamu
nyingine, ni kutoka wafanyakazi wa Idara ya Katiba na Msaada wa kisheria wa
Unguja na Pemba, kupitia Mkurugenzi wao Hanifa Ramadhan Said, taasisi za haki
za binadamu za Tanzania bara na Zanzibar.
Maratibu
huyo wa CHAPO alieleza kuwa, salamu nyingine za kuwatakia moyo wa ustahamilivu,
zimetolewa na wakurugenzi na wajumbe wa bodi za jumuiya za wasaidizi wa sheria za
Unguja na Pemba.
Aidha Hassan
alisema kuwa, kufuatia kifo hicho, watetezi wa haki za binadamu Pemba, kutoka
jumuia za PACSO, TAMWA, ZALHO, Jeshi la Polisi, Mahkama, Mawakili wa kujitegemea
na wale wa serikalini, nao wametuma salamu zao.
Akizungumzia
kifo cha marehemu Nassor Bilali Ali, alisema juzi alipata taarifa ya kuugua kwake
na kukimbizwa hospitali ya wilaya ya Chake chake, iliyopo Vitongoji.
Alifafanua kuwa,
baada ya hali kuwa mbaya, alipata uhamisho na kufikishwa hospitali ya Abdalla
Mzee Mkoani kwa matibabu zaidi, na kulazwa usiku mmoja.
Siku ya pili
yake, (Augost 7), alipatiwa rufaa ya kimatibabu kwenda hospitali ya Mnazi mmoja
Unguja, na wakati akiwa uwanja wa ndege wa Pemba, majira ya saa 3:50 hali
ilibadilika na kufariki dunia.
Akizungumza kwa
njia ya simu, Mkuu wa Divisheni ya Katiba na Msaada wa Kisheria ofisi ya Pemba
Bakar Omar Ali, alimtaja marehemu kuwa, alikuwa mchapakazi kwa saa 24.
Alisema,
moja ya wakurugenzi waliofanikiwa kuiinua jumuia ya wasaidizi wa sheria,
alikuwa na Nassor wakati wa uhai wake, jambo lililochangia kupata tunzo kadhaa.
Mjumbe wa Bodi
ya ‘CHAPO’ Zuwena Hamad Ali, alisema ni pengo kubwa, kifo hicho ingawa ni kazi
Muumba, siku zote huwa haina makosa.
Mkurugenzi
wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Mkoani ‘MIDIPAO’ Nassor Hakim Haji,
akizungumza kwa niaba ya wakurugenzi wenzake, alisema marehemu alikuwa tegemeo
sio tu kwenye ‘CHAPO’ lakini kwa jumuiya zote.
‘’Alikuwa
mwenyeji, anaejiamini, anaejua mambo, aliyekuwa akipenda kujitolea na siku zote
alikuwa anatuusia umoja, mshikamano, ukweli na ushirikiano,’’alifafanua.
Mtandao wa Watetezi
wa Haki za Binaadamu Tanzania (THRDC), nao umesema umepokea kwa mshtuko kifo
hicho cha mwanachama wao, na kuitaka familia, ndugu, wana CHAPO kuwa wavumilivu
katika kipindi hichi kigumu.
Mwenyekiti
wa taifa wa Mtandao wa utetezi wa haki za watoto Tanzania’ MUHUWATA’, John Joseph
Malale, wamewataka wanacha CHAPO na familia yake, kuwa wavumilivu katika
kipindi.
‘Nassor alikuwa
zaidi ya mwanaharakati wa haki za
watoto, alikuwa zaidi ya msaidizi wa sheria, daima alikuwa anatuongoza
hata sisi viongozi na unapomka kazi hakuwa tayari kumshinda,’’inafafanua
taarifa hiyo.
Marehemu Nassor
Bilali Ali, alizikwa siku hiyo hiyo kijiji kwao Vikunguni wilaya ya Chake chake
Pemba, ambapo viongozi kadhaa na watu maarufu, wasaidizi wa sheria, wanasheria
na mawakili walishiriki kwenye mazishi hayo.
Kabla ya
kukumbwa na umauti huo, Nassor alipata elimu ya usaidizi wa kisheria baina ya mwaka
2012/2013, na kisha baada ya kuanzishwa kwa CHAPO, alichaguliwa nafasi ya Mkurugenzi,
kwa vipindi tofauti, kuanzia mwaka 2016 hadi umauti unamkuta.
Mwisho



Comments
Post a Comment