CHAPO: 'WANANCHI UCHANGANI JENGENI URAFIKI NA WATOTO WENU MTAYAPATA MINGI '
WANANCHI
wa kijji cha Uchangani shehia ya Ndagoni wilaya ya Chake chake Pemba,
wametakiwa kujenga urafiki endelevu na watoto wao, ili kugundua kwa haraka,
ikiwa wanakumbana na changamoto zikiwemo za udhalilishaji.
Ushauri huo
umetolewa Augost 6, 2024 na Msaidizi wa sheria wa shehia za Wesha na Ndagoni, Khadija
Said Khalfan, wakati akizungumza na wananchi hao, kwenye mkutano wa wazi
ulioandaliwa na Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria ‘CHAPO’.
Alisema, mbinu
nzuri kwa wazazi na walezi, ya kugundua mazito wanayopitia watoto wao,
wanapokuwa skuli au madrassa, ni kujenga nao urafiki endelevu.
Alieleza kuwa,
kupitia mpango huo mzazi au mlezi, anaweza kumuuliza maswali kadhaa na majibu
yake, yanaweza kumpa mwanga na kujua aina ya marafiki na mwenendo wa mtoto wake kwa ujumla.
Alifahamisha
kuwa, sio kinga kwa wazazi na walezi, kulalamikia ugumu wa maisha na kuacha kuwatunza
watoto na kuwa nao karibu, kwani mazingira yasiorafiki yanazidi kutawala kwa sasa.
‘’Ni kweli,
wazazi sasa wako na harakati ngumu za maisha, lakini na watoto nao wanahitaji
kutunzwa, na njia moja wapo ni kujenga urafiki, ambao utakuwezesha mzazi
kugundua yaliojificha kwa mtoto wako,’’alifafanua.
Katika hatua
nyingine, Msaidizi huyo wa sheria, aliwashauri wazazi hao, kutowaruhusu watoto
wao kukogeshana wenyewe, bila ya mzazi kufanya kazi hiyo, kwa baadhi ya siku.
Mapema Askari
wa shehia za Wesha na Ndagoni Khamis Ali Khamis, aliwatahadharisha wazazi na
walezi, hao juu ya watoto wao kutumiwa na wasafirishaji, wauzaji na watumiaji wa
dawa za kulevya.
‘’Sasa wale
wanaotumia dawa za kulevya, wameanzisha ujanja wa kuwatumia watoto, wakijua
kuwa hata wakikamatwa nazo, hawawezi kutiwa hatiani, sisi wazazi tuwe makini na
hili,’’alifafanua.
Nae Msaidizi
wa sheria wa shehia ya Wawi Haji Nassor Mohamed, amewakumbusha wazazi kuwa,
hadi sasa kwa mujibu wa sheria, mtoto anatambulika ni mtu yeyote aliyechini ya
miaka 18.
‘’Kwa mantiki
hii, tunaendelea kutahadharisha kwa wale wadhalilishaji, hakuna kinga kwa eti mtoto
huyo, kaja mwenyewe kwenye nyumba, na kisha kufanya nae tendo la ngono, bado
kisheria inaitwa ni ubakaji,’’alifafanua.
Aidha Msaidizi
huyo wa sheria, amewatahadharisha wazazi na walezi, kutothubutu kuwafungisha
ndoa watoto wao waliobakwa, kama njia ya kuyatengeneza.
Wananchi wa
kijiji hicho, akiwemo Ali Sharif Khamis, alisema bado hukumu hazijakuwa kubwa,
kama sheria inavyoelekeza, na ndio maana, matendo ya udhalilishaji yanaendelea
kuripotiwa.
Nae ustadhi
Salim Khamis Salim, alisema kama jamii haikuyarejesha malezi ya pamoja, suala
la kupunguza majanga kwa watoto, litaendelea kuwa ndoto.
Mwananchi Fatma
Hamad Khamis, alisema bado njia za kupitishiwa dawa za kulevya, hazijalindwa
ipasavyo, na ndio maana vijana wanaendelea kuzitumia.
‘’Zanzibar
dawa za kulevya hazizalishwi wala hazilimwi, sasa inakuaje wanaofanya biashara
hii, wanatuletea, tusema ulinzi haupo vizuri katika bandari zetu na uwanja wa
ndege,’’alihoji.
Akiufunga mkutano
huo, Naibu sheha wa kijiji hicho Hazina Musheha Omar, alisema kazi zinazofanywa
na wasaidizi wa sheria, na kama zitaungwa mkono, jamii inaweza kuondokana na changamoto
mbali mbali.
Aidha aliwahakikishia
wasaidizi hao wa sheria, kuyafanyia kazi maagizo walioyoyatoa, ikiwa ni njia
moja wapo ya kuwalinda watoto wao na ukatili na udhalilishaji.
Mwisho











Comments
Post a Comment