‘WANAWAKE MSIONGOZE VIKAO VYA SULHU KESI ZA UDHALILISHAJI’

 


NA ALI KHAMIS, PEMBA@@@@

MJUMBE wa sheha wa shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake, Mwanajuma Bakar Mohamed, amewataka wanawake wa kijiji cha Mchekeweni, wasikubali kuongoza vikao vya sulhu, inapotokeza changamoto ya udhalilishaji wa watoto.

Alisema, imebainika wapo baadhi ya wanawake wamekuwa ndio watandikaji majamvi na mikeka, ili kuandaa mchakato wa sulhu, kwenye kesi za udhalilishaji.

Mjumbe huyo, aliyasema hayo jana kwenye madrassa ya wanawake iliyopo kijijini hapo, wakati wa mkutano wa wazi, ulioandaliwa na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake ‘CHAPO’, ikiwa ni mkutano wa kawaida wa utoaji wa elimu.

Alieleza kuwa, ni vyema sasa wakakimbilia vituo vya kisheria, ili kutoa taarifa haraka, mara tu inapotokeza changamoto ya ukatili na udhalilishaji.

‘Sisi akinamama, ni kweli tumeumbwa na huruma kubwa, lakini sio katika eneo hilo, na wala tusijihusishe na sulhu, kwani kufanya hivyo, ni kumuuza mtoto wako kwa thamani ndogo,''alieleza.

Katika hatua nyingine, Mjumbe huyo wa sheha, aliwataka wananchi wake, kuwatumia wasaidizi wa sheria waliomo shehia ya Wawi, ili kupata ushauri na msaada wa kisheria bila ya malipo.

Hata hivyo alisisitiza haja, kwa wananchi kuhudhuria kwenye mikutano kadhaa, inayoitishwa na wasaidizi wa sheria, ili kuongeza uwelewa wao.

Mwalimu wa Madrassa hiyo ya wanawake kijijini hapo Snei Hamad Khamis, alisema kazi inayofanywa na CHAPO, inasaidia kuibua changamoto za ukatili na udhalilishaji kwa watoto.

Mapema Msaidizi wa sheria, shehia ya Wawi Haji Nassor Mohamed, aliwakumbusha wananchi, kuacha kununua ardhi kiholela, ili kuepusha miogoro.



‘’Huwezi kununua ardhi kama muuzaji, hujajiridhisha yeye aliipataje ardhi husika na kama ana hati zinazokubalika za matumizi, vyenginevyo unaweza kucheza mchezo wa kubahatisha,’’alifafanua.

Aidha, aliwaeleza wanawake hao kuwa, kuendelea kuwachunga watoto wao wa kiume, kwani dunia ya sasa imakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwemo ukatili na udhalilishaji.

‘’Hapa niwakumbushe kuwa, kisheria mtoto ni mtu yeyote aliyechini ya miaka 18, sasa ni wajibu wa wazazi kisheria, kuhakikisha hakumbwi na janga lolote,’’alisisitiza.

Hata hivyo Msaidizi huyo wa sheria, aliwakumbusha wanawake hao, kuwatumia wasaidizi wa sheria wanapokumbwa na kesi za madai, kabla ya kufika mbele ya vyombo ya sheria.

Akiufunga mkutano huo, Sheha wa shehia ya Wawi Sharifa Abdalla Waziri, aliwaeleza wanawake hao, kuwa mfano bora ndani ya jamii yao, kimaadili.

Aidha, aliwataka vijana wanaoishi shehia ya Wawi, kutoa taarifa kwa wenzao, wanaotumia dawa za kulevya, au kuingiza na kusafirisha.

Baadhi ya wanawake hao, walisema bado migogoro ya ardhi inawaumizwa kichwa, kwa kuwepo wavamizi wa maeneo yao, pasi na nyaraka zinazotambulika.

‘’Inawezekana unalima sehemu kwa zaidi ya miaka 40, kisha anakujia mtu ana karatasi, ambazo hazitambulika anakunyang’anya eneo lako,’’alifafanua mwananchi Asha Ali Khamis.

Nae Saada Haroun Ali, alisema kama serikali haikuwalegeza masharti ya usajili wa ardhi, wananchi wengi ambao ni wanyonge, watazikosa ardhi zao.

                  Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’