MJANE AIPA TANO ‘CHAPO’ KUMPA MTAJI
MJANE wa
watoto watatu mkaazi wa shehia ya Uwandani wilaya ya Chake chake, ameishukuru
Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilayani humo ‘CHAPO, kumuwezesha kwa mtaji wa
shilingi 70,000 na kuanza biashara.
Alisema
hakutarajia kua, ombi lake la shilingi 70,000 kwa uongozi wa ‘CHAPO’
lingejibiwa kwa haraka, ambalo alitamani kuanzisha biashara ya uji na mandazi,
akiamini ndio itakayomsadia kimaisha.
Mama huyo
aliyasema hayo, jana wakati akizungumza na mwandishi wa habari hizi, kufuatia
kutekelezewa ombi lake kwa CHAPO alilolitoa Juni 25, mwaka huu kwenye shamra
shamra ya wiki ya msaada wa kisheria.
Alisema, tokea
akabidhiwe mtaji wa shilingi 70,000 Juni 27, sasa anaendelea vizuri na
kujipatia faida, kati ya shilingi 3,500 hadi shilingi 4,000 kwa biashara ya uji
na mandazi kwa siku.
‘’Kwa hali
yangu ya kipato, mimi nikipata shilingi 4,000 huwa shilingi 2,000 nazihifadhi
na hadi sasa nimeshatimiza shilingi 32,000 kama faida, sio jambo dogo kwangu,’’alifafanua.
Aidha mama
huyo mwenye watoto watatu, aliyeachika mwaka mmoja uliopita, akidai kutekelezwa
kihuduma na aliyekua muumewake, alisema sasa anafikiria kuongeza biashara
nyingine.
‘’Nimeshawishika
kununua nazi mjini na kuja kuuza hapa nyumbani Uwandani, maana biashara ya uji
na maandazi imeshanikubali,’’alifafanua.
Katika hatua
nyingine, mama huyo alisema kama wanaume wataendelea kuyaacha majukumu yao,
wanawake na watoto wataendelea kudhalilika.
‘’Mimi huyu aliyekuwa
muume wangu, hadi sasa ni mwaka simjui alipo na wala kwa njia ya simu hapatikani,
lakini sitoisahau ‘CHAPO’ kwa msaada wa mtaji na sasa nashukuru,’’alieleza.
Mkurugenzi wa
‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, alisema walipokuwa Uwandani kwenye mkutano wa wiki
ya msaada ya kisheria, waliibuka wanawake kadhaa, wakilalamika ukosefu wa
huduma kwa waliokuwa, waume zao.
‘’Wengi wao
walitaka msaada na ushauri wa kisheria, lakini mmoja, alitupa mpango wake kazi,
na tukamsaidia shilingi 70,000 na sasa anaendelea vizuri,’’alisema.
Hata hivyo
alisema waliokwishawapa msaada unaofanana na huo, wapo wengi katika wilaya ya
Chake chake, kwani ndio jukumu lao la msingi.
‘’Moja ya
jukumu letu la msingi ni kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria tena bila
ya malipo, ndio maana huwataka wananchi tunapokuwa na mikutano, wahudhurie,’’alifafanua.
Akizungumza
kwenye kikao cha tathmini hivi karibuni, Mkuu wa divisheni ya Katiba na Msaada
wa Kisheria Pemba Bakar Omar Ali, alisema mfano kama huo ni miongoni mwa mrejesho
mzuri kwa jamii.
Alieleza kuwa,
mikutano inayowafikia wananchi moja kwa moja, mara zote huzaa matunda, maana watu
wamezungumkwa na changamoto na hawajui nani wamfikishie.
Mwisho

Comments
Post a Comment