JUMUIYA ZA WASAIDIZI WA SHERIA PEMBA: 'WIKI YA MSAADA YA KISHERIA ILICHAPUZA KAZI ZETU'
WAKURUGENZI wa Jumuiya za wasaidizi wa sheria
kisiwani Pemba, wamesema wiki ya msaada wa kisheria iliyomalizika mwezi uliopita
kisiwani Unguja, ilichapuza utendaji wao wa kazi, kwa jamii.
Wakizungumza kwenye kikao cha tathmini kilichofanyika leo
Julai 5, 2024 ukumbi wa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Chake chake,
walisema waliongeza hamasa ya kutoa elimu kwa jamii.
Walieleza kuwa, ijapokuwa hilo ni jukumu lao la msingi,
lakini kuanzia Juni 25 hadi 27, mwaka huu, waliwafikia wananchi wengi zaidi,
kuliko ilivyozoeleka.
Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria Micheweni ‘MIDIPAO’
Saleh Hamad alisema kwa kushirikiana na Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria,
walilifikia kundi la walengwa wa mpango wa kunusuru kaya maskini, Micheweni.
Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya
Mkoani ‘MDIPAO’ Nassor Hakim Haji, alisema walipanga kuwafikia wandesha boda
boda 65, ingawa walivuuka lengo hilo.
‘’Kwa mfano, sisi tulitarajia kukutana na waendesha boda
boda 65, lakini kwa nguvu ya Idara, kwa kushirikiana na wadau wengine
tuliwafikia 113, jambo ambalo lilikuwa kubwa,’’alieleza.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria
wilaya ya Chake chake CHAPO, Nassor Bilali Ali, alisema hata wao walifikia
wananchi 378 wa Uwandani, kuwapa elimu.
‘’Tulichagua wale waliomo kwenye mpango wa kunusuru kaya
maskini, na kwa hakika kwenye mkutano huo tulivuuka malengo yetu,’’alifafanua.
Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria Wete WEPO,
Hemed Ali Hemed, alisema pamoja na changamoto ya bajeti, lakini wanafunzi wa vyuo
vikuu walifikiwa kwa wingi wa aina yake.
Akiwasilisha ripoti ya utekelezaji wa shughuli za wiki ya
msaada wa kisheria, Mkuu wa Divisheni ya Katiba na Msaada wa Kisheria Pemba
Bakar Omar Ali, alisema mafanikio makubwa yamefikiwa.
‘’Moja ni kufanikisha wiki ya tano ya msaada wa kisheria,
kupatikana kwa bajaji kwa Jumuiya saba za wasaidizi wa sheria, pamoja na
kuongeza idadi ya wasaidizi wa sheria wapya,’’alifafanua.
Aidha alieleza kuwa, jingine ni kufikiwa kwa wanafunzi wa
vyuo vikuu 805 kwa Unguja na Pemba pamoja na waendesha boda boda 508, ambao
baadhi yao wamefikiwa kwa ushirikiano baina yao na Jumuiya za wasaidizi wa
sheria.
Akizungumzia changamoto za wiki ya tano ya msaada wa kisheria,
alisema ni pamoja na ufinyu wa bajeti, uliosababisha uhaba wa washiriki kwenye
kilele cha maadhimisho hayo kutoka kisiwani Pemba.
Hata hivyo, amewakumbusha wasaidizi wa sheria kuwatumia
waandishi wa habari, wakati wanapotekeleza majukumu yao, ili na wengine
waelewa wanachokifanya.
‘’Kama mkishindwa kuwatumia waandishi, basi hata mpige
picha mziweke kwenye mitandao ya kijamii, ili watu wengine wajue, kwanza uwepo wenu
pili kazi mnazozifanya,’’alifafanua.
Baadhi ya washiriki wakitoa maoni yao, akiwemo Safia
Saleh Sultan, alisema kazi zinayofanywa na wasaidizi wa sheria ni kubwa, hivyo
waendelee nazo kwa maslahi ya jamii yao.
‘’Msingi mkubwa wa kazi zenu ni wa kujitolea, sasa
msivunjike moyo, maana jamii inawategemea mno katika kufanikisha hilo, mkirudi
nyuma mmewapoteza,’’alieleza.
Wiki
ya tano ya msaada wa kisheria Zanzibar, ilizinduliwa Juni 24, 2024 na Waziri wa
Nchi Afisi, Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Zanzibar, Haroun Ali
Suleiman na kilele kufanyika Juni 28 mwaka huu na Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar Hemed
Suleiman Abdulla, alikuwa mgeni rasmi, katika ukumbi wa Idrissa Abdull Wakil na
ujumbe wa mwaka huu, ulikuwa ni ‘tumia teknologia kurahisisha upatikanaji wa
haki’’.
Mwisho
Comments
Post a Comment