CHAPO: 'WAPENI ELIMU YA KINGA WAZAZI WIZI WA WATOTO'
JUMUIYA ya wasaidizi wa sheria wilaya ya
Chake chake Pemba ‘CHAPO’ imewakumbusha wasaidizi wa sheria wilayani humo,
kutilia maanani, elimu kwa jamii, juu ya wimbi la wizi wa watoto lililoibuka
hivi karibuni.
Kauli hiyo imetolewa leo Julai 27, 2024 na Afisa Ufuatiliani na Tathmini
kutoka ‘CHAPO’ Wahida Kombo Khamis, kwenye kikao cha mwezi cha kuwasilisha
ripoti za elimu na msaada wa kisheria, kilichofanyika ofisini kwao mjini Chake
chake.
Alisema, pamoja na kuwaelimisha wananchi juu ya
udhalilishaji, migogoro ya ardhi, ndoa, wizi, dawa za kulevya pamoja na
kuhubiri amani, lakini watilie mkazo, juu ya elimu ya tahadhari ya wizi wa
watoto.
Alieleza kuwa, ijapokuwa kwa wilaya ya Chake chake
halijakua la kutisha jambo hilo, kama ilivyo kwa baadhi ya mikoa ya Tanzania
bara, lakini ni vyema, kinga ikaanza kuwekwa.
Alifahamisha kuwa, hilo ni miongoni mwa majukumu ya
wasaidizi wa sheria, hivyo ni wakati sasa kulieleza kwa upana, ili jamii
ifahamu na izidishe ulinzi kwa watoto wao.
‘’Tukianza kutoa elimu kwa jamii, kuanzia mwezi Augost
mwaka huu, tusisahau kuwaeleza kwa upana, juu wizi wa watoto, ambao kwa mikoa
ya Tanzania limekuwa maarufu,’’alieleza.
Katika hatua nyingine, Afisa huyo Ufuatiliaji na Tathmini
Wahida Kombo Khamis, aliwataka wasaidizi hao wa sheria, kuwasilisha mapema
ripoti zao za kutoa elimu na msaada wa kisheria.
Mapema Mkurugenzi wa ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali,
alisema kuanzia sasa, ripoti zote za wasaidizi wa sheria za mwezi, siwasilishwe
sio zaidi ya tarehe 3 ya mwezi mpya.
‘’Imekuwa uletaja wa ripoti haupewi kipaumbele, sasa
ili kuhakikusha tunakwenda vizuri, kila msaidizi wa sheria, awasilishe ripoti
na iwe mwisho wa mwezi husika na sio vyenginevyo,’’alifafanua.
Katika hatua nyingine, aliwataka wasaidizi wa sheria
wakongwe, kuzidisha ushirikiano wao wa karibu na wale wapya, ili lengo la kutoa
elimu, ushauri na msaada wa kisheria, litimie.
Aidha Mkurugenzi huyo, amewakumbusha wasaidizi hao
wa sheria, wanapopata mafunzo, kuhakikisha wanakuwa na mrejesho kwa kuwasomesha
na wingine.
Mratibu wa CHAPO Mohamed Hassan, aliwakumbusha
wasaidizi hao wa sheria, kuendelea kufanya kazi za kuwaelimisha wananchi, juu
ya sheria mbali mbali.
Alieleza kuwa, zipo sheria kadhaa zimeshafanyiwa
marekebisho na nyingine ni mpya, hivyo ni nafasi yao, kuhakikisha wanawaelisha
wananchi katika shehia zao.
Mkurugenzi fedha wa ‘CHAPO’ Riziki Hamad Ali, aliwakumbusha
wanachama hao, kuhudhuria katika shughuli zote wanazoalikwa, bila ya kujali
nauli.
Masaidizi wa sheria kutoka Wesha Khadija Said
Khalfan, alisema ushirikiano ndio njia pekee, utakayofanikisha kazi zao za
kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria, kwa jamii.
Msaidizi wa sheria Jimbo la Chonga Asha Hamad Faki,
aliwasisitizia wenzake, kuendelea kuwa karibu na wasaidizi wa sheria wapya, ili
kuwajenga kiuwezo.
Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake
Pemba ‘CHAPO’ imekuwa na utaratibu wa kukutana na wanachama wake kila mwishoni
mwa mwezi, kwa ajili ya kuwasilisha ripoti na kuibua changamoto, zinazokwaza
katika shughuli zao.
Mwisho









Comments
Post a Comment