BONANZA: WATOTO YARIPOTINI MAJANGA MNAYOFANYIWA
NA HASINA KHAMIS, OUT- PEMBA@@@@
MKURUGENZI Mtendaji wa Jumuiya ya Tumaini Jipya Pemba ‘TUJIPE’ Tatu
Abdalla Msellem, amesema watoto wana haki ya kulindwa na kulijinda
wenyewe, kutokana na majanga mbali mbali, yakiwemo ya udhalilishaji kwa kuyaripoti
kwa wazazi na Serikali pale awapofanyiwa vitendo hivyo.
Alisema, kulingana na mazingira ya sasa baadhi ya wazazi
wamekuwa mbali na watoto wao, na ndio chanzo cha udhalilishaji na ukatili
wanaofanyiwa watoto hao.
Aliyasema hayo jana Julai 21, 2024 katika bonanza la Mabaranza ya watoto lililofanyika
skuli ya Istikama Mkanjuni wilaya ya Chake Chake, lilioandaliwa kwa ushirikiano
na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’.
Aidha aliwataka kujilinda, kusimamia na kujitetea katika suala la
udhalilishaji na mazingira yao wanayoishi, ili kuepukana na vitendo hivyo.
"Kumekuwa na mtindo wa watoto kudhalilishana, hivyo
ninawaomba kuacha mara moja kufanya vitendo hivyo, na ikitokezea, karipotini
kwa waratibu wa mabaranza pamoja na wazazi wenu,"aliwashauri.
Aidha Mkurugenzi huyo wa TUJIPE, alisema uwepo wa waratibu
katika mabaranza ya watoto, wanasaidia kupunguza woga na hofu kwa wahanga wa
vitendo hivyo.
Alisema mabaraza hayo yanasaidia kupunguza changamoto
zinazowakabili watoto na familia, kwani bado baadhi ya watoto hawako salama,
kwenye familia zao.
Nae Afisa Mradi Jumuishi kutoka Taasisi ya Save the Children, Maftah
John Yohaness, alisema ni vyema kuwashirikisha watoto wenye mahitaji
maalum, katika masuala yote ya kijamii na kielimu.
‘’Watoto wenyemahitaji maalum, wana haki sawa kama wingine,
hivyo kuwapenda, kuwashirikisha, kuwajali na kuwalinda ni jukumu letu sote,"alifafanua.
Aidha aliwakumbusha watoto hao, kuwa wazalendo wa taifa lao, kwa
kuweka maslahi mbele ya taifa lao, wakijua kuwa wanao wajibu huo, ili baadae
wawe viongozi wema.
Akisoma risala ya baranza la watoto wa mkoa wa kusini, Katibu
mkuu wa Baraza hilo, shehia ya Msingini, Yunus Ali Mussa, aliwataka wazazi, walezi,
wadau, serikali na jamii, kuwapatia haki ya elimu ya msingi, kwa kuwaandikishwa
watoto wote wenye sifa.
Alieleza kuwa, wapo watoto hasa wenye mahitaji maalum, wamekuwa
wakifungiwa ndani na kukoseshwa haki yao ya msingi, jambo linaloongeza ufinyu
wa ufahamu wao.
‘’Sisi tunazochangamoto nyingi za kiafya, zinazosababisha
maendeleo duni ya ukuaji wetu na kusababisha vifo, hivyo tunaomba wazazi
kutekeleza majukumu yao ya msingi kwetu, ili tupate afya njema,’’alieleza.
Hata hivyo, aliishukuru wizara ya Afya Zanzibar, kwa kuendelea
kuwapatia kinga za maradhi mbali mbali ikiwemo kichocho, minyoo pamoja na saratani
ya shingo ya kizazi.
Mkurugenzi wa ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, katika hutuba yake
iliyosmwa na Mratibu wa ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Ali, aliwaasa watoto kuachana na
tamaa za kifedha na mali, ikiwa ni njia sahihi ya kushawishika kuingia katika
mitengo ya watu waovu hasa wabakaji.
Hata hivyo Mkurugenzi huyo, alisema wataendelea kukutana na mabaraza
ya watoto katika shehiz zote, 32 za wilaya ya Chake chake, ili kuwaelimisha na
majanga yaliopo.
Katika hatua nyingine, aliwasisitiza wazazi na walezi, kuacha
utamaduni wa kuzisuluhisha kesi za jinai zikiwemo za udhalilishaji, kwani
kufanya hivyo ni kukiuka sheria.
‘’Kwanza tujilinde na udhalilishaji, lakini tunapoona kuna
viashiria tunao wasaidizi wa sheria kwenye shehia zetu, tuwatumieni ili kupata
elimu, msaada na ushauri wa kisheria bila ya malipo,’’alisisitiza.
Bonanza hilo, linalofanyika kila mwaka, limetayarishwa kwa
pamoja kati ya Idara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na watoto kwa
kushirikisna na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba
CHAPO.
Ambapo, kauli mbiu ya mwaka huu 'Mlinde, Mpende na
Mshirikishe Mtoto kwa Maendeleo ya Taifa.’
MWISHO





Comments
Post a Comment