KILELE WIKI YA MSAADA WA KISHERIA: MAKAMU WA PILI AAGIZA JUMUIYA ZA WASAIDIZI WA SHERIA ZIPATIWE OFISI
NA HAJI
NASSOR, UNGUJA@@@@
MAKAMU wa
Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdull, amesema nia yake ni kuona
jumuiya zote za wasaidizi wa sheria, zinakuwa na ofisi ambazo hazitolipa kodi,
kwani msingi wa kazi zao, ni wa kujitolea.
Makamu huyo
wa Pili, aliyasema hayo leo Juni 28, 2024 kwenye kilele cha maadhimisho
ya wiki ya msaada wa kisheria, kilichofanyika ukumbi wa Idrisaa Abdull-wakil
mjini Unguja.
Alisema,
kama hatua zimeshachukuliwa kwa jumuiya za wasaidizi wa sheria wilaya ya Kusini
na Kaskazini ‘A’ kuwa ofisi na jumuiya nyingine tisa zilizobaki, lazima hilo
lifanyike.
Alieleza kuwa,
kwa vile msingi mkuu wa wasaidizi wa sheria ni wa kujitolea, hakuna budi kwa
serikali, kuhakikisha inajitolea na kuwapatia ofisi, ili wafanye kazi zao kwa
ufanisi.
‘’Nitawatuma
wasaidizi wangu, kukutana na uongozi wa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria
Zanzibar, ili kukaa pamoja na kuona kila wilaya, imetoa jengo kwa ajili ya ofisi
za wasaidizi wa sheria,’’alieleza.
Katika hatua
nyingine, Makamu huyo wa Pili wa rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdulla, alieleza
kuwa, watoaji wa msaada wa kisheria wamekuwa wakombozi kwa jamii ya Zanzibar,
na kuhakikisha wanapata haki zao.
Alieleza kuwa,
ndani yake wamo ambao waliokwishakata tamaa kupata haki zao na sasa wanaendelea
kupata faraja, baada ya elimu, ushauri na kupata msaada wa kisheria.
Aidha Makamu
huyo wa Pili, alifahamisha kuwa ni jambo la faraja kuona uratibu, usimamizi na
uendeshaji wa masuala ya msaada wa kisheria hapa Zanzibar, yanaendeshwa katika ubora
wa hali ya juu.
Wakati huo huo, Makamu huyo wa Pili wa Rais, akiabidhi bajaji saba, kwa ajili ya Jumuiya za wasaidizi wa sheria ikiwa ni ahadi ya Rais wa Zanzibar Dk. Husseinn Ali Mwinyi.
Aidha Makamu huyo wa Pili alizindua nambari ya simu ya bure 800710230 kwa ajili ya wataka huduma za kisheria, ambapo nambari hiyo hapo baadae, itawekewa kifaa maalum kitakachoruhusu kuweza kutumiwa na watu 15 kwa wakati mmoja
Mapema Waziri
wa Nchi Afisi, Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Zanzibar Haroun
Ali Suleiman, aliiagiza Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar,
kuangalia katika bajeti yake ijayo, kupatiwa sabuni kwa wasaidizi wa sheria.
Alieleza kuwa,
wamekuwa wakifanyakazi kubwa ya kuwasaidia wananchi kwa njia ya kujitolea,
hivyo ni vyema kwa sasa kuangaliwa, ili kupata sabuni kwa lengo la kuwapa hamasa
na kujenga ari kwao.
‘’Kwa vile
wasaidizi wa sheria, wamekuwa wakifanyakazi kubwa, natoa agizo kwa Idara ya
Katiba na Msaada wa Kisheria, katika bajeti ijayo, kufikiria mara mbili jambo
hilo,’’alifafanua.
Aidha Waziri
Haroun, aliwashauri washirika wa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria wakimo
LSF, UNDP na wengine kuangalia uwezekano wa kusaidia, jambo hilo.
Mkurugenzi Idara
ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar Hanifa Ramadhan Said, alisema kabla ya
kilele cha maadhimisho ya wiki ya msaada wa kisheria, shughuli kadhaa ikiwemo
makongamano ya vyuo vikuu, yalifanyika.
‘’Kwa shughuli
zilizofanywa na Idara yetu pekee, wananchi 816, walifikiwa na elimu ya kisheria,
ambapo kwa waliofikiwa na watoaji wa msaada wa kisheria kwa Unguja na Pemba ni
wananchi 1,690,’’alieleza.
Aidha Mkurugenzi
huyo, alisema ushirikiano uliopo kwa taasisi kama za skuli ya sheria, ofisi ya
Mkurugenzi wa mashtaka, Jeshi la Polisi, Chuo cha mafunzo, Mahkama na wasaidizi
wa sheria, wamekuwa wakifanikisha malengo yao.
‘’Hata hivyo
kipekee, niwapongeze wenzetu wa LSF na UNDP kwa kuendelea kutushika mkono,
katika mradi wa upatikanaji haki Zanzibar, jambo ambalo linawapa faraja watu
wasio kuwa na uwezo,’’alieleza.
Akiwasilisha
salam za LSF, Meneja Mawasiliano na Ushirikiano wa tasisi hiyo Jane Matinde,
alisema kwa muda wa miaka mitano sasa, wamekuwa wakisaidia kufanyika kwa wiki
ya msaada wa kisheria.
Aidha Meneja
huyo, alisema kwa Tanzania bara na Zanzibar, wastani wa wananchi milioni 10,
wameshafikiwa na elimu ya msaada wa kisheria kwa mwaka jana pekee.
Alifafanua kuwa,
hilo linasaidia kupunguza kesi mahkamani na kupunguza migogoro ndani ya jamii,
jambo ambalo linaimarisha utawala bora na utawala wa sheria.
‘’Hadi sasa
tunaendelea kuyasaidia mashirika 184 Tanzania nzima, ambapo wanawafikia
wananchi kuwapa elimu bure, na wastani wa mashauri 100,000 na asilimia 70
hutatuliwa na wasaidizi wa sheria,’’alifafanua.
Wakitoa salamu
zilizosomwa na Time Asaa Khamis, wasaidizi wa sheria Zanzibar, walimpongeza Waziri
Haroun, kwa kufuta ada ya usajili ya shilingi 20,000 kwa wasaidizi wa sheria.
Aidha, alisema
wamefarajika kuona, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein
Ali Mwinyi kutimiza ahadi yake ya
kuwapatia bajaji.
Alieleza kuwa,
kati ya bajaji zilizoombwa za jumuia za wasaidizi wa sheria 11 kwa Unguja na
Pemba, tayari bajaji saba zimeshapatikana na kuamini kuwa kwa wilaya nyingine
zitapatiwa hapo baadae.
Katika hafla
hiyo, wasaidizi wa sheria kadhaa walikabidhiwa tunzo kwa utendaji wao bora pamoja
na jumuiya bora ya wasaidizi wa sheria kwa mwaka huu.
Waliopata tunzo
hizo ni Nassor Bilali Ali kutoka Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake
chake CHAPO, kuwa masaidizi wa sheria bora wa mwaka.
Wengine ni
Mwaka Mzee Mohamed, aliyeibuka msaidizi wa sheria bora kwa Unguja, katika haki
za binaadamu ni masaidizi washeria kutoka Mkoani ‘MDIPAO’ Massoud Abdalla
Massoud.
Aidha Omar
Abdalla Nassor, alipata tunzo ya mazingira kutoka Jumuiya ya wasaidizi wa
sheria wilaya ya Wete ‘WEPO’ Nassor Bilali Ali, alipata tena kwa upande wa kupinga
ukatili na udhalilishaji, wakati jumuiya bora ya wasaidizi wa sherua ni ya
Magharibi ‘A’
Wiki ya msaada
wa kisheria Zanzibar ilizinduliwa Juni 24, 2024 na Waziri
wa Nchi Afisi, Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Zanzibar Haroun
Ali Suleiman.
Hii ni wiki
ya tano wa Msaada wa Kisheria Zanzibar, ambapo ujumbe wa mwaka huu ni ‘tumia
teknologia kurahisisha upatikanaji wa haki.
Mwisho








.jpg)




Comments
Post a Comment