ZIARA YA ‘CHAPO’ YAFUFUA BARAZA LA WATOTO CHANJAANI
UONGOZI wa shehia
ya Chanjaani wilaya ya Chake chake Pemba, umesema ujio wa wasaidizi wa sheria
kutoka Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilayani humo, umewasaidia kutambua dhana
ya baraza la watoto kisheria, kinyume na hapo awali.
Hayo yameelezwa juzi
na Sheha wa Chanjaani Khatib Ali Vuai, wakati akizungumza na mwandishi wa
habari hizi, baada ya kumalizika kwa kikao, kilichojumuisha wasaidizi wa
sheria, wajumbe wa sheha na askari shehia na kufanyika Chanjaani Gereji.
Alisema, hapo awali
hakuwa na uwelewa mpana, wa nini maana ya baraza la watoto, utataratibu wake,
aina ya wajumbe, idadi, kazi zao, utambuzi wake kisheria, ingawa ujio wa
wasaidizi wa sheria umemfungua macho.
Alieleza kuwa,
alikuwa anasikia tu ndani ya shehia yake, kuwa kuna baraza la watoto, ingawa
alidhani ni suala lisilotambuliwa kisheria, na hakuwa na hamu ya kulifuatilia kwa
undani.
Alifahamisha kuwa,
kikao hicho cha wasaidizi wa sheria kutoka ‘CHAPO’, kimempa mwanga mpana, na
sasa amepanga kukutana na Mratibu wa baraza hilo na wajumbe wake, ili
kujitambulisha rasmi.
‘’Ziara yenu wasaidizi
wa sheria, imenisaidia mno mimi sheha na wajumbe wangu, juu ya dhana ya kisheria
ya uwepo wa baraza hili, na sasa tunatamani kukutana na Mratibu na wajumbe
wake, ili kulifahamu kwa upana,’’alisema.
Katika hatua nyingine
sheha huyo, aliupongeza uongozi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya
Chake chake ‘CHAPO’ kwa kuandaa ziara hiyo, ambayo imewasaidia mambo kadhaa.
‘’Nimefurahishwa
niliposikia kuwa, kupitia mabaraza hayo, sheria inakubali kwa watoto wenyewe,
kuanzisha klabu kama za mazingira, kupinga udhalilishaji na ile ya maadili,’’alieleza.
Nae mjumbe wa sheha
eneo la Vijijini Khadija Said Abdall, alisema ndio kwanza anasikia kutoka kwa wasaidizi
hao wa sheria, kuwa kuna baraza la watoto, katika kila shehia za Unguja na
Pemba.
Alisema, awali hakuwa
na taarifa sahihi juu ya uwepo wa baraza hilo, hasa kwa vile katika kijiji
anachokiongoza, hakuna mwanachama wala mjumbe.
‘’Kama lipo baraza
la watoto hapa shehia ya Chanjaani, basi ni kwa baadhi ya watoto na kwenye
baadhi ya vijiji, maana mimi ni mjumbe wa shehia, lakini sina taarifa, mpaka
mlipokuja kutueleza.’’alifafanua.
Nae mjumbe wa sheha
Rehema Juma Faki, alisema ziara hiyo ya wasaidizi wa sheria, imeamsha uwelewa
kwao na sheha wao kwa ujumla, na kinachofuata, sasa ni kulifufua baraza hilo.
‘’Kwa Zaira yenu
hii, inatubidi sasa tumfuatilie Mratibu wa baraza la watoto la shehia yetu, na
kama baraza liko hai ni kuliendeleza na kama limefifia ni kulifufua,’’alisema.
Mapema Msaidizi wa
sheria shehi ya Chanjaani Wahida Kombo Khamis, alisema nia ya ziara yao hiyo,
ni kutaka uwelewa kwa sheha na wajumbe wake, juu ya uwepo wa baraza hilo.
Alisema, kisha
Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’, ni kutaka
kuanzisha klabu ya kupinga udhalilishaji ndani ya baraza hilo.
Alieleza kuwa,
maana watoto wamekuwa ndio waathirika wakubwa katika janga la ukatili na
udhalilishaji, sasa kupitia chombo chao cha baraza, wanalengo la kuanzisha
klabu hiyo.
‘’Zipo shehia kama
za Msingini, Wawi, Wesha mabaraza ya watoto yanafanyakazi vizuri, sasa lengo la
ziara hii, ni kutaka kulifufua au kuliendeleza baraza la watoto shehia ya
Chanjaani,’’alisema.
Mkurugenzi wa ‘CHAPO’
Nassor Bilali Ali, akizungumza na wasaidizi wa sheria hivi kaibuni, alisema wameanza
mpango madhubuti wa kuhakikisha kila shehia, inakuwa na klabu ya kupinga
ukatili na udhalilishaji.
Alieleza kuwa,
awali walikuwa na mpango wa kuzifikia shehia tano za Msingini, Kibokoni, Ng’ambwa,
Matale na Wesha, ingawa sasa mpango ni shehia zote 32 za wilaya ya Chake chake.
‘’Tunachoamini,
kila shehia inalo baraza la watoto, lakini tukibaini kuna shehia linalega lega,
kwanza nikulifufua na kulisimamia na kisha kuanzisha klabu ya kupinga ukatili
na udhalilishaji ndani yake,’’alisema.
Msaidizi wa sheria
jimbo la Chake chake Riziki Hamad Ali, alisema klabu hizo ambazo zitawezeshwa kielimu
na mbinu hapo baadae, ili kutambua viashiria vya ukatili na udhalilishaji.
Alieleza kuwa, kwa
vile wasaidizi wa sheria ni wadau wa haki za binaadamu, ndio maana wameamua kuanzisha
vilabu hivyo, na kisha kuvisimamia.
‘’Kama tunataka
viongozi wazuri wa baadae, au wasaidizi wa sheria, wakuu wa wilaya na mikoa waliosalama,
lazima tuchukue hatua sasa za kuwalinda watoto wetu,’’alieleza.
Msaidizi wa sheria
shehia ya Wawi Haji Nassor Mohamed, alisema tayari kwa upande wa shehia yake,
ameshakutana na uongozi wa baraza la watoto, na kutambua changamoto zao.
‘’Inaonekana haya
mabaraza yanafanyakazi kwa uwepo wa miradi tu, bila ya kujali kuwa, suala la
kutoa elimu na kusikiliza changamoto za watoto ni kazi ya kila siku,’’alisema.
Hata hivyo, amesema
amepata moyo kuona uongozi wa shehia ya Chanjaani, kutaka kukutana na Mratibu
wa baraza la watoto la shehia hiyo, kwa lengo la kutafuta namna ya kuliendeleza.
Tayari ziara hiyo
ya wasaidizi wa sheria, imeshazitembelea na kufanya mikutano katika shehia za
Wesha, Wawi, Chanjaani, Matale, Msingini, Ziwani kwa lengo la kuanzisha klabu za
kupinga ukatili na udhalilishaji kwa watoto.
MWISHO



.jpg)



Comments
Post a Comment