CHAPO: YAWAPA MBINU WANAFUNZI WESHA KUKOMESHA UDHALILISHAJI

 


NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

 WANAFUNZI wa Almadrssatul Fatuhu-l-khair ya kijiji cha Mchochani shehia ya Wesha, wilaya ya Chake chake Pemba, wametakiwa kuwaripoti waalimu, wazazi, kaka, wajomba na watu wengine maarufu, ikiwa watawagundua  wameanza mchezo wa kutaka kuwadhalilisha.

 

Ushauri huo umetolewa leo Mei 19, 2024 na wasaidizi wa sheria shehia ya Wara Sabahi Mohamed Abdalla na mwenzake wa Wesha Khadija Said Khalfan, wakati wakitoa elimu ya kisheria, kuhusu viashiria vya udhalilishaji kwa wanafunzi hao, kwenye mkutano wa wazi ulioandaliwa na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake ‘CHAPO’.

 

Walisema, wasijaribu kuwaficha watu wa aina yoyote, ikiwa watawabaini wameanza tabia ambayo, sio ya kawaida, kama vile kuwachezea sehemu zao za siri, hivyo wasisite kutoa taarifa.

 

Walieleza kuwa, katika hilo waondowe woga na wasiwasi, kwani sheria zipo kwa ajili ya kuwalinda, hivyo kama watahisi kuna mchezo wanachezewa, wasisite kutoa taarifa haraka.

 



Msaidizi wa sheria shehia ya Wara Sabahi Mohamed Abdalla, alisema wakiendelea kuwaficha watu hao, wanaweza kuwadhalilisha nyumba nzima, wakijua kuwa hakuna hatua yoyote inayochukuliwa.

 

‘’Wanafunzi, mkihisi kunadalili za kutaka kudhalilishwa, hata awe mwalimu au baba, tuweni taarifa kwa mtu mwingine au kwa msaidizi wa sheria na sheha, ili hatua zichukuliwe,’’alieleza.

 

Nae Msaidizi wa sheria shehia hiyo, Khadija Said Khalfan, amewakumbusha wazazi na walezi hao, kuwa karibu na watoto, ili kuwagundua mapema, ikiwa wameanza ama laa, kufanyiwa vitendo vya udhalilishaji.

 



‘’Njia moja nzuri ya kumfuatilia mtoto, ni kujua marafiki zake, maeneo anayopenda kucheza, aina ya michezo, muda wake wa kulala na kuamka, na hata suala la matumizi yake,’’alishauri.

 

Mapema Askari wa Jeshi la Polisi kutoka wilya ya Chake chake anaefanyakazi shehia za Wesha, Ndagoni na Michungwani Khamis Ali Khamis, aliwakumbusha wazazi na walezi, kuwaripoti waingizaji, wasambaazaji na watumiaji wa dawa za kulevya, ili hatua zichukuliwe.

 

Alieleza kuwa, kwa miaka ya hivi karibuni, watu hao waovu huwatumia watoto katika kazi hiyo, kwa kuwalaghai kwa fedha au zawadi, jambo ni hatari zaidi.

 



Aliongeza kuwa, sasa ni wakati wa jamii kuwapiga vita watu wa aina hiyo, kwani madhara ya utumiaji wa dawa za kulevya, haumuathiri mtu mmoja pekee, bali jamii kwa ujumla.

 

Akifungua mkutano huo, Sheha wa shehia ya Wesha Haji Mohamed Ali, aliwataka wananchi hao, wasisite kuwaripoti kwake au kwa Jeshi la Polisi, wahalifu mbali mbali.

 



‘’Sisi jamii tuungane, kuukataa kwa vitendo uhalifu, ukiwemo udhalilishaji na dawa za kulevya, maana athari ya haraka hutukumba sisi wakaazi wa eneo husika,’’alifafanua.

 

Mwalimu mkuu wa Almadrasatu Fatuhu-l- khaira ya kijiji cha Mchochani shehiani humo, sheikh Kassim Bakar Yussuf, aliutaka uongozi wa ‘CHAPO’ kuongeza juhudi zaidi za utoaji, elimu. 



Wanafunzi Asma Kassim Bakar na mwenzake Ibrahim Mohamed Rashid, walisema uamuzi wa ‘CHAPO’ kuwafuata kijijini kwao ni hatua nzuri, kwani wamepata kuuliza na kujibiwa maswali yao.

 

Mzazi Aziza Omar Khamis, alisema ni vyema, ulinzi ukawepo kwa wananchi wanaotoa taarifa ya uwepo wa vitendo vya kihalifu, ili nao wapate ari na kasi ya kushirikiana na jeshi la Polisi. 


Mkutano huu, ni muendelezo wa mikutano ya wazi, inayofanywa cha ‘CHAPO’ kwa kushirikiana na masheha na askari shehia, kwa lengo la kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria bila ya malipo.

                                        Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’