CHAPO YAANZA MAANDALIZI WAWI UANZISHWAJIA KLABU YA KUPINGA UDHALILISHAJI BARAZA LA WATOTO
NA ASHA ABDALLA, PEMBA@@@@
JUMUIYA ya wasaidizi washeria wilaya ya Chake
chake Pemba, ‘CHAPO’ imesema inampango wa kuanzisha klabu maalum ya kupinga vitendo
vya ukatili na udhalilishaji ndani ya baraza la watoto la shehia ya Wawi, kwa
lengo la kulijengea uwezo, ili kutambua viashiria ya vitendo hivyo.
Hayo yameelezwa wasaidizi washeria wa shehia
za Wawi, Wesha, Waram Mgogoni na Kibikoni wilayani humo, wakati wakizungumza na
wajumbe wa baraza hilo, kwenye mkutano maalum wa wazi, wenye lengo la kupanga
mikakati ya kutokeza vitendo hivyo.
Walisema kuwa CHAPO, inalojukumu kubwa la
kuhakikisha kila shehia ya wilaya ya Chake chake, imefikiwa na elimu inayostahiki
katika kupinga vitendo vya ukatili na udhalilishaji kwa watoto, ikiwemo
kuanzisha klabu hizo.
Mmoja kati ya wasaidizi wa sheria hao kutoka
shehia ya Wesha, Khadija Said Khalfan, alisema kuwa, wasaidizi wa sheria kazi
yao ya msingi ni kutoa elimu na msaada wa kisheria bure, ikiwemo kuyapitia
makundi kama ya mabaraza ya watoto.
Alieleza kuwa, suala la uanzishwaji wa klabu
ndani ya mabaraza ya watoto, itakuwa rahisi sasa kwa watoto hao, kupata jukwaa
la kuelezea matendo wanayofanyiwa katika maisha yao.
‘’Chapo kupitia wasaidizi wa sheria, na
kupitia mabaraza ya watoto tutaanzisha klabu maalum, zenye lengo la kupinga
ukatili na udhalilishaji, na kisha watoto watajengewe uwezo wa kuzungumza na
kuibua viashiria vya ukatili na udhalilishaji,’’alieleza.
Mapema Msaidizi wa sheria wa shehiya ya Wawi Haji
Nassor Mohamed alisema kuwa, watoto wawe tayari kupinga udhalilishaji kwa njia
moja ama nyingine, pale tu wanakapoona viashiria ambavyo watafanyiwa.
"Watoto mnatakiwa kuwa makini, wakati
munapoona viashiria vya ukatili na udhalilishaji, ikiwemo kupewa zawadi ovyo
ovyo, kuoneshwa picha chafu kwa simu, kuitwa vichochoroni au hata kuchezewa
miili yenu na kila mtu,’’alifafanua.
Hata hivyo aliwataka watoto hao, kuawa tayari
kutoa taarifa, pale wanapofanyiwa udhalilishaji au kutoa ushahidi popote hata
kama mtendaji huyo ni baba mzazi, kaka au kiongozi wowote kutoka katika taasisi
au serikalini.
Katika hatua nyingine, aliwaomba watoto hao
kua mabalozi kwa wenzao ambao hawakuhudhuria katika mkutano huo, kuwapa elimu, ili
kujua mambo muhimu ambayo waweze kujitenga nayo.
Akizungumzia umuhimu wa kuanzishwa kwa klabu
ya kupinga vitendo vya ukatili na udhalilishaji, alisema vitakuwa ndio jukwaa
kwa watoto hao la kupashana habari na kuelezana madhila wanayopitia.
Kwa upande wake Msaidizi wa sheria wa shehiya
ya Wawi Fatma Hilali Salim, alisema kua watoto wanapodhalilishwa kwa njia
yoyote ile, iwe ni kuadhibiwa, kulawitiwa, kubakwa, kupewa majina wasiyoyataka,
wahakikishe hawakai kimnya.
Nae Msaidizi
wa sheria wa shehiya ya Kibokoni Haitham Hamad Khamis, aliwaomba watoto wasisite
kutoa taarifa kwa wale ambao wanafanyiwa udhalilishaji, kwa kuhofia
vitisho.
Wakizungumza kwenye mkutano huo, Mratibu wa
wanawake na watoto ambae ni mratibu wa baraza la watoto shehia ya Wawi Fatama
Kassim Mohamed na Mwenyekiti wa baraza hilo Abuubakar Masoud Juma, walipongeza hatua
ya Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ kwa kuonesha nia ya kupinga vitendo hivyo.
Walisema, mabaraza hayo yamekuwa wakati
mwingine yakikosa msaada kama wa elimu, ingawa aanamini baada ya ujio wa
wasaidizi wa sheria, sasa watoto watatambua haki na wajibu wao kwa jamii.
‘’Sisi hiyo klabu tunahamu nayo mno, maana
hata watoto wa shehia ya Wawi, nao hawako salama na vitendo vya ukatili na
udhalilishaji, njooni tusaidiane kuwalinda watoto wetu,’’alisema Mwenyekiti.
CHAPO
kwa sasa imo katika utekelezaji wa mradi wa upatikanaji haki, unaofadhiliwa na
taasisi ya LSF, ambapo moja ya shughuli katika mradi huo, ni kuanzishwa klabu
za kupinga udhalilishaji kupitia mabaraza ya watoto, katika shehia teule za
Kibokoni, Wesha, Ng’ambwa, Matale na Msingini.
MWISHO














Comments
Post a Comment