'CHAPO' YAZINDUA VILABU VYA KUPINGA UDHALILISHAJI MABARAZA YA WATOTO

 

 
NA HAJI NASSSOR, PEMBA@@@@

AFISA Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto wilaya ya Chake chake Salma Khamis Haji, amewataka watoto wilayani humo, kutoa taarifa, pindi wanakapoona viashiria vya ukatili na udalilishaji dhidi yao, ikiwemo kuanza kuchezewa sehemu zao za siri.

Hayo ameyasema leo April 28, 2024, skuli ya Maandalizi Madungu, wakati akieleza wajibu wa mabaraza hayo, kwenye mkutano wa uzinduzi wa vilabu vya kupinga ukatili na udhalilishaji wa kijinsia, kupitia mradi wa upatikanaji haki, unaoendesha na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake ‘CHAPO’.

Alisema moja ya malengo ya vilabu hivyo, ni kuwawezesha watoto hao, kutetea mambo yanayohusu, huku jambo la mwanzo likiwa ni kutokukaa kimnya wanapoona viashiria vibaya kwao.


Alieleza kuwa, kiashiria kimoja wapo ambacho wanatakiwa kukiripoti ni kuanza kuchezewa sehemu za miili yao, kupewa zawadi na fedha zisizo na sababu maalum, pamoja na kuitwa maeneo yasio rasmi (vichakani).

Alieleza kuwa, wapo watu ambayo wanatabia mbaya, na wanaweza kuwatengenezea mazingira ya kuwaharibu, ikiwemo kuanza kuwapa fedha na kuwashika shika miili yao.

Alifafanua, wakiona kuna mtu wa kando, au wa ndani ya familia na hata mwalimu wake, ameanza na tabia hizo haraka sana watoe taarifa iwe kwa familia, mratibu wa wanawake na watoto  au mwalimu wao.

“Watoto mkiona kuna mtu ameanza kukuita, kukupa fedha, zawadi anza kutoa taarifa nyumbani au skuli, kwani wapo wengine huwa huo ndio mwanzo wa kutaka kuwadhalilishaji,’’aliwatahadharisha.



Akizungumzia vilabu hivyo, Afisa huyo aliesema kuwa, jambo lililoibuliwa na ‘CHAPO’ ni jema, maana litawasaidia watoto hao kuwa na sehemu muhimu, ya kutoa malalamiko yao.

Alieleza kuwa, wapo watoto wamekuwa wakikumbana na vitendo mbali mbali, lakini wakati mwingine hawajui pa kukimbilia, ingawa anaamini vilabu hivyo vitakuwa sehemu sahihi kwao.

Katika hatua nyingine, Afisa huyo, alisema hivi karibuni wizara itayapitia upya mabaraza yote ya watoto, ili kuyaendeleza upya, ikiwemo kufanya chaguzi, baada ya wajumbe wa awali, wengi wao, kupindukia umri wa utoto.

Akifungua mkutano huo, Mkurugenzi wa CHAPO, Nassor Bilali Ali alisema ‘CHAPO’ imeamua kuanzisha vilabu vya kupinga ukatili na udhalilishaji, kupitia mabaraza hayo, kwani watoto ndio waathirika wakubwa.




Alieleza kuwa, ili kuhakikisha vilabu hivyo vinakuwa endelevu, kila msaidizi wa sheria hapo baadae, atakuwa ndio msimamizi mkuu wa vilabu hivyo.

‘’Wasaidizi hawa wa sheria pamoja na majukumu yao ya kila siku, lakini watakwenda kuwajengea uwezo wa kielimu watoto hao, ili wazidi kujitambua kwa lengo la kuibua chamgamoto zinazowakabili,’’alifafanua.

Akitoa mada ya njia za kujikinga na vitendo vya ukatili na udhalilishaji, Mratibu kutoka ‘CHAPO’, Mohamed Hassan Abdalla, alisema moja wapo ni kwa watoto hao, kufuatana kwa makundi wanapokwenda na kurudi masomoni.

Njia nyingine alisema, ni kwa wazazi na walezi, kukubali kuleleana watoto, ili kila mmoja awe na nguvu ya kuripoti matendo atakayoyaona ya mtoto wa jirani yake.





Wakizungumza kwenye mkutano huo, watoto hao wamesema kupitia vilabu hivyo, watapata jukwaa sahihi la kuelezea kero na changamoto wanazopitia katika maisha yao.

Mwenyekiti wa baraza la watoto shehia ya Msingini Said Hassan Khamis, aliwashauri wazazi na walezi, kupunguza matumizi ya nguvu kwa watoto wanapowaadabisha, kwani kufanya hivyo kunaweza kukasababisha ukatili.



‘’Lakini pia niwashauri wazazi na walezi wasiwe wakali kupindukia pale wanapotaka taarifa kutoka kwa watoto, kwani wengine wanaweza wasitowe ushirikiano na kukosekana kwa taarifa sahihi,’’alifafanua.

Msaidizi wa sheria Jimbo la Chake chake Riziki Hamad Ali, amewasihi watoto hao, kuhakikisha wanakaa na wenzao wasiopata elimu hiyo, ili kuwaelekeza.

 Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ katika utekelezaji wa mradi huo wa upatikanaji haki, unaofadhiliwa na taasisi ya ‘LSF’ unafanyakazi katika shehia tano za Wesha, Ng’ambwa, Kibokoni, Msingi na Matale.

                          mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’