ALIYEUPASUA MPIRA WA WATOTO WESHA ULIOTOLEWA NA CHAPO AAHIDI KUULIPA
MWANAMKASI
Mikidadi Maeda (38) wa shehia ya Wesha wilaya ya Chake chake, amekubali ushauri
wa wasaidizi wa sheria wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilayani humo, ‘CHAPO’
kulipa gharama za mpira mmoja wa miguu, alioupasua baada ya kumgonga kwa bahati mbaya, wakati
timu ya ‘kaza buti’ inyomilikiwa na baraza la watoto la shehia hiyo, walipokuwa
wakifanya mazoezi.
Mpira huo
awali, ulikabidhiwa kwa uongozi wa baraza hilo ukitoka CHAPO, Machi 20, mwaka
huu, kwa ajili ya timu hiyo, ikiwa ni ahadi ya wasaidizi wa sheria, walioitoa
kwa watoto hao, mwishoni mwa mwaka jana.
Kwenye kikao
cha sulhu kilichofanyika nyumbani kwa sheha wa shehia ya Wesha, mwananchi huyo
alikiri kosa la kujichukulia sheria mikononi, mara baada ya tukio hilo la yeye
kugongwa mpira wa uso.
Alisema siku
ya tukio hilo, alikuwa nyumbani kwake, kando kando ya uwanja huo, wakati akiwa
kwenye harakati zake, alishtukia mpira ukienda usoni mwake, na kumsababisha
maumivu, jambo ambalo lilimsababishia kujawa na hasira.
‘’Baada ya
kunipiga mpira, wachezaji wengine walinizomea na mimi kutokana na maumivu
niliyopata nilichukua uamuzi ambao sio sahihi wa kuuchana mpira kwa kisu, ingawa
nakiri kosa,’’alisema.
Aidha
mwananchi huyo alikiri kuwa, nyumba yake iko kando kando ya uwanja mpira unaotumika
na hata kwa mashindani ya wilaya, na upo zaidi ya miaka 100 kwa sasa.
‘’Mimi
pamoja na maumivu niliyoyapata, lakini nakiri kuwa, nilitakiwa niwafuate wazazi
wa watoto ama niripoti kwa sheha, kwa kosa walilonifanya, lakini nilijichukulia
sheria mikononi, sasa naahidi kuwa Arpili 28, mwaka huu nitawasilisha fedha
hizo kwa sheha,’’alifafanua.
Katika hatua
nyingine, mwananchi huyo, alishauri kuwa ni vyema michezo inapofanyika katika
uwanja huo, wachezaji wawe na tahadhari, ya hali ya juu, kwani kwa eneo ulipo
uwanja wanaweza kusababisha maafa kwa wazee na watoto.
Akizungumza kwa
niaba ya baraza la watoto, Mratibu wa baraza hilo Waride Seif Mohamed, aliwataka
wananchi kujenga utamaduni wa kuripoti kwa sheha, wanapokoseana katika jamii.
Alieleza kuwa,
hakuna kinga ya kuwa na hasira na kujichukulia sheria mikononi, kwani kwa sasa
vipo vyombo kdhaa ngazi ya shehia ikiwemo wasaidizi wa sheria, askari shehia,
mratibu wa wanawake na watoto na sheha mwenyewe, kwa ajili ya kupokea malalamiko
mbali mbali.
‘’Mimi
niwashukuru wasaidizi wa sheria kutoka ‘CHAPO’ kwa kufanikisha kikao cha sulhu,
maana kwa upande wa baraza, lilikuwa limeshashindwa juu ya mgogoro huo,’’alieleza.
Kwa upande
wake Msaidizi wa sheria wa shehia ya Wesha, Khadija Said Khalfan, alisema
watoto au kundi jingine lolote linapokosea, ni vyema taratibu za kisheria
zifuatwe.
‘’Sisi wasaidizi
wa sheria kutoka CHAPO, kila siku tunaelimisha jamii, juu ya namna ya kuvitumia
vyombo vya kisheria, inapotokezea shida yoyote, lakini sio kujichukulia sheria
mikononi,’’alifafanua.
Hata hivyo amewataka wachezaji wa klabu hiyo ya ‘kaza buti’ ya baraza la watoto la shehia ya Wesha, kuwa waangalifu wanapokuwa mazoezini, kwani uwanja wao, uko katikati ya makaazi ya wananchi.
‘’Ni kweli
wananchi ndio waliofuata uwanja hapa, lakini hiyo haiwi sababu ya kutoangalia
watu wanapopita, maana kila mmoja ana haki yake katika nchi,’’alieleza.
Sheha wa
shehia ya Wesha Haji Mohamed Ali, alimtaka mwananchi huyo kuhakikisha analipa
fedha hiyo kwa siku aliyoahidi mwenyewe, ili kuepussha mingine ya kisheria.
Alieleza kuwa,
shehia yake inavyombo tofauti kama waratibu, kamati ya maadili, watu maarufu, wasaidizi
wa sheria ambapo mote humo unaweza kuwasilisha malalamiko.
‘’Hakuna
sheria yoyote hata kama watoto walikuzomea na kisha ukapandwa na hasiri juu ya
suala la kujichukulia sheria mkononi, hapo ukifanya unanunua kosa jingine
kisheria,’’alifafanua.
Katika hatua
nyingine, sheha huyo, alisema watoto wanazo haki zao mbali mbali ikiwemo
kucheza, kusoma, kupewa majina mazuri, matibabu, chakula na mavazi.
Hata hivyo,
ameutaka uongozi wa timu hiyo ya kaza buti, kuwa makini wanapokuwa kwenye
michezo yao, kujenga heshima kwa watu wote pamoja kuwathimini wapiti njia.
Mapema kiongozi
wa timu ya Kaza buti ya baraza la watoto shehia ya Wesha, Ahmed Issa Adam,
alisema baada ya tukio hilo, walimuomba radhi mwananchi huyo, ingawa alikataa.
Hata hivyo,
aliwapongeza wasaidizi wa sheria kutoka ‘CHAPO’ kwa kuumaliza mgogoro huo, na
kuahidi kuwaangalifu wanapokuwa kwenye mazoezi yao.
Timu ya
baraza la watoto la shehia ya Wesha wilaya ya Chake chake, itarejea tena uwanjani
kuanzia Aprili, 28 mwaka huu, kuendelea na mazoezi, baada ya kusita kufanya
mazoezi, kufuatia mpira waliokuwa wakitumia kupasuliwa wiki tatu zilizopita.
Mwisho






Comments
Post a Comment