CHAPO YAPOKEA WASAIDIZI WA SHERIA WAPYA, YAWAPA NENO

 

NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

JUMUIYA ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba CHAPO, imewapokea wasaidizi wa sheria wapya na kuwahakikishia ushirikiano wa hali ya juu, ili kufikia malengo ya kuihudumia jamii, wilayani humo.

Hayo yalielezwa leo Machi 30, 2024 na Mkurugenzi wa ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, wakati wa ukaribisho na mapokezi ya wasaidizi wapya watatu wa sheria, kutoka shehia za Michungwani, Kibokoni na Mgelema, hafla iliyofanyika ofisi ya CHAPO, mjini Chake chake.

Alisema, C HAPO inafarajika mno kuona sasa inaongeza idadi ya wasaidizi wa sheria 21, kutoka 18 wa awali, jambo ambalo linaendelea kupunguza ukakasi kwa shehia 11, zitakazobakia bila ya kuwa na wasaidizi wa sheria, kati ya zote 32 za wilaya hiyo.

Alieleza kuwa, wasaidizi hao wa sheria wapya, watapewa kila aina ya ushirikiano, wakati huu wa miezi mitatu wakiwa kwenye majaribio na hata baada ya kumaliza na kuanza kazi rasmi shehiani mwao.



Mkurugenzi Nassor alifafanua kuwa, wananchi wa vijiji wanavyotoka wasaidizi hao wa sheria, kwa sasa wakae mkao wa kula kwa kuwatumia, kwani wapo baadhi ya wananchi, wameshakata tamaa katika kuzipata haki zao.

‘’Kwanza nyinyi wasaidizi wa sheria karibuni ‘CHAPO’ kwenye kazi ya kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria kwa njia ya kujitolea, na tumefarajika kwa Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, kutupatia watendaji hawa,’’alieleza.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi huyo wa CHAPO, aliwataka wasaidizi hao wa sheria wapya, kuhakikisha wanajenga ngome imara ya ushirikiano na wenzao, kabla na wakati wanapotaka kutoa elimu ya kisheria.

Hata hivyo, aliwakumbusha kuongeza elimu ya sheria hatua kwa hatua, kwani changamoto za kisheria na mabadiliko yake, yanakuja kila kila siku hapa Zanzibar.

Akizungumzia kuhusu kuhudhuria kwenye vikao, aliwataka wasaidizi hao wa sheria wapya na wingine, kuhakikisha wanafuatilia vikao hivyo, kwani ni muhimu kwa maendeleo ya CHAPO na wananchi wa Chake chake kwa ujumla.

Wakati huo huo Mkurugenzi huyo, aliipongeza taasisi ya LSF kwa kuendelea kuwabeba na kuwawezesha katika mradi maalum wa miezi tisa wa upatikanaji haki, ambao umeshaanza mwezi Fubauri, mwaka huu.

Mapema Mratibu wa ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdalla, alisema mbinu ya kufikia malengo ya utoaji wa msaada wa kisheria, inachangiwa na mambo kadhaa ikiwemo ubunifu, ushirikiano, kujituma na kukubali kujifunza kila siku.



Akizungumzia suala la usajili kwa wasaidizi wa sheria, aliwataka ambao bado, kuharikisha kufanya hivyo, hasa kwa vile ada ya mwaka ya shilingi 20,000 ilishaondolewa na Waziri husika, tokea mwaka jana.

Mkurugenzi fedha wa ‘CHAPO’ Riziki Hamad Ali, aliwakumbusha wasaidizi wa sheria, kuendelea kuihudumia jamii, katika kushughulikia changamoto zao, wakijua kuwa hiyo ni kazi ya kujitolea.

Msaidizi wa sheria, shehia za Wawi, Mgogoni na Ziwani Fatma Hilali Salim, alisema ikiwa kuna upangwaji wa makundi ya wasaidizi wa sheria, ni vyema kukaangaliwa jiografia, baina ya msaidizi wa sheria mmoja na mwingine.





Nae Msaidizi wa sheria Abeda Abdi Seif, alisema moja ya mafanikio ya msaidizi wa sheria, ni kuhakikisha anafanyakazi kwa karibu mno na sheha wake, ili kuona anapata nguvu ya kushirikishwa.

‘’Inawezekana Msaidizi wa sheria anamlalamikia sheha wake, kwamba hamshirikishi, lakini pengine mwenyewe anakuwa ametingwa na kazi zake, kisha akamuangushia sheha lawama,’’alieleza.

Kwa upande wake msaidizi wa sheria mpya kutoka shehia ya Mgelema Asha Juma Ali, alisema atahakikisha anayafanyia kazi kwa vitendo, mafunzo aliyopewa hivi karibuni.

Nae Msaidizi wa sheria kutoka shehia ya Kibokoni Haitham Hamad Khamis, alisema anachoomba ni ushirikiano wa hali ya juu, kwa wale wenzake, waliomtangulia katika kazi hiyo.



Mkutano huo ambao ni wa kawaida kila mwisho wa mwezi, kwa leo uliambatana na mafunzo ya ujazaji wa fomu za elimu na msaada wa kisheria, kutambulishwa kwa wasaidizi wa sheria wapya waliomaliza mafunzo hivi karibuni na utambuzi wa mradi wa upatikanaji haki.

                                      Mwisho  

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’