CHAPO YAMALIZA SIUTAFAHAMU MATUMIZI UWANJA WA SOKA WESHA
NA ABDALLA
MBAROUK, PEMBA @@@@
WASAIDIZI
wa sheria kutoka wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ wamemaliza siutafahamu ya
matumizi ya uwanja wa mpira wa miguu, baina ya timu ya watoto ya Baraza la
watoto la shehia ya Wesha na wachezaji wa vilabu vikubwa shehiani humo.
Itakumbukwa kuwa,
Disemba 17, mwaka 2023, wasaidizi hao wa sheria, walipokea lalamiko la kusitishwa
kwa matumizi ya uwanja uliopo Wesha kwa sheha, timu ya kazabuti inayomilikiwa
na baraza la watoto la shehia hiyo, wakielezwa kuwa, hawana haki ya matumizi ya
uwanja huo.
Ambapo baada
ya malalamiko hayo, wasaidizi wa sheria kutoka CHAPO, wakiongozwa na Msaidizi
wa sheria mwenyeji wa shehia ya Wesha, Khadija Said Khalfan, waliahidi kulitafutia
ufumbuzi lalamiko hilo.
Msaidizi wa
sheria huyo akiwa na wenzake watatu, waliahidi kukutana na uongozi wa vilabu
vikubwa vinavyotumiwa uwanja huo, ili kuona na timu ya kaza buti ya baraza la
watoto la shehia ya Wesha, nao wanautumia uwanja huo kufanya mazoezi.
Ndipo leo
Machi 16, 2024, wasaidizi hao wa sheria, walikuwa na kikao cha wazi kati ya uongozi
wa baraza la watoto, mwakilishi wa timu wanaotumia uwanja huo, askari shehia na
wananchi wengine, na kukubaliana juu ya matumizi ya uwanjua huo.
Akizungumza kabla
ya kufikia makubaliano hayo, Msaidizi wa sheria wa shehia Wawi Haji Nassor
Mohamed, alisema moja ya haki ya msingi za mtoto, ni kucheza michezo kadhaa.
Alieleza kuwa,
kama uwanja uliopo shehia ya Wesha ni mmoja, ni vyema kwa timu kubwa kupangiana
zamu, ili na timu ya watoto ya Kaza buti, nayo ipate haki ya matumizi ya uwanja
huo.
‘’Hii timu
kubwa ya Wesha, ambayo sasa inaendelea kufanya vizuri, chanzo chake ilikuwa
kama ilivyo hii ya watoto, ambapo kwa wakati huo, ililelewa na watu wazima
waliokuwepo, na sasa ndio inatamba,’’alieleza.
Hivyo amewanasihi
wachezaji wa timu kubwa, kuangalia uwezekano wa haraka, ili kuvilea vipaji vya
watoto wao, kwani ndio wanapoanzia kutoka kwa wachezaji wa vilabu vya timu za
Simba, Yanga na kisha timu ya taifa.
Awali Msaidizi
wa sheria kutoka shehia ya Wara Sabah Abdalla Mohamed, alisema, watoto wanazo
haki nyingi, moja wapo ni kusoma, kulindwa na kucheza.
‘’Sisi
wasaidizi wa sheria, leo tumeshawakabishi mpira mmoja na filimbi, sasa ni
wajibu wazazi, walezi, wamiliki wa uwanja na wachezaji wa timu kubwa, kupanga
nao ratiba, ili wakuze vipaji vyao kupitia uwanja huo,’’alieleza.
Kwa upande
wake Mkagauzi wa Polisi, anayeshughulikia shehia hiyo, Khamis Ali Khamis
alisema, kukabidhiwa kwa mpira huo na ruhusa ya kucheza kwao, isiwe chanzo cha
kukatisha masomo.
‘’Wakati
mnautumia uwanja huu kukuza vipaji vyenu, mkumbuke kuwa, bado wajibu wenu wa
kutafuta elimu na kusoma kwa bidii, ipo pale pale, sasa michezo isiwe chanzo
cha kuacha masomo,’’alifafanua.
Mapema kiongozi
wa timu ya Kaza buti ya baraza la watoto shehia ya Wesha, Ahmed Issa Adam,
alisema watautumia muda wa ziada kufanya mazoezi katika uwanja huo.
Hata hivyo,
aliwapongeza wasaidizi wa sheria kutoka CHAPO, kwanza kwa kutimiza ahadi ya kuwanunulia
mpira na filimbi, kama ambavyo waliwaahidi wakati walipokutana nao mwishoni mwa
mwaka, jana.
‘’Lakini
tuendelee kuwashukuru kwa kulipatia ufumbuzi suala la matumizi ya uwanja, kwani
timu kubwa, walidhani sisi hatuna haki ya matumizi ya uwanja, lakini leo,
tunashukuru wameshakubali,’’alisema.
Mwakilishi wa
vilabu vikubwa wanaotumia uwanja wa Wesha Kassim Yussuf Ali, alisema kuanzia
sasa uwanja huo, utatumiwa na rika zote, ikiwa ni njia moja yapo ya kuibua,
kukuza na kuendeleza vipaji.
‘’Ni kweli
hata sisi ambao leo tunaitwa timu kubwa, miaka 25 iliyopita tulikuwa wadogo na
kuruhusiwa kucheza, na ndio maana sasa tunaiwakilisha hata Pemba, kwenye mpira
wa miguu,’’alieleza.
Mratibu wa
Baraza la watoto shehia ya Wesha Waride Seif Mohamed, alisema atahakikisha timu
hiyo inafika mbali, kwani kwa sasa michezo imekuwa ikizaa ajira na kujenga
uhusiano mwema.
Hata hivyo,
alisema watajipanga vyema ili kuhakikisha wanalifanyia kazi wazo la kutafuta fedha
nusu na kisha kuziwasilisha kwa wasaidizi wa sheria, kwa ajili ya ununuzi wa jezi
kwa timu hiyo.
Wasaidizi wa
sheria kutoka Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba CHAPO,
wanaendelea na kutekeleza mpango wao kazi, wa kukutana na makundi mbali mbali,
ili kusikiliza changamoto zao za kisheria.
Mwisho











.jpg)


Comments
Post a Comment