CHAPO: NA MIAKA SABA YA MAPAMBANO YA UKATILI, UDHALILISAJI CHAKE CHAKE
NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@
CHAPO, ni kifupi cha Jumuiya ya Wasaidizi
wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba.
Ukiwa mtaalamu wa lugha sema ‘Chake chake
Paralega Organization’ kwa ufupi ni CHAPO.
CHAPO, sio neno geni masikioni mwa wakaazi
wa wilaya ya Chake chake, wanaoishi ndani ya shehia 32, ikiwemo za Vitongoji,
Wesha na Chanjaani, inayobebwa na majimbo ya Chake chake, Ole, Ziwani, Chonga
na Wawi.
Kwamba, humu ndio eneo la CHAPO
inapofanyakazi, tena kupitia wanachama wake, ambao ni wasiaidizi wa sheria tena
waliosajiliwa na kutambuliwa.
Kwa sasa, si haba kuanzia mwaka 2018, serikali
imeshapitisha sheria rasmi, iliyokuja kuweka mambo yawe ‘shega’
mazuri ya wasaidizi wa sheria.
Maana, ipo sheria maarufu ya Msaada wa Kisheria
Zanzibar nambari 13 ya mwaka 2018, ambayo awali ilitanguliwa na sera ya mwaka
2017, ambayio imekuja kumueleza nani Msadizi wa sheria?
Kwamb, ni yeyote aliyepata mafunzo ya awali
ya sheria, na kisha kusajiliwa, na Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria
Zanzibar, na kuanza kufanyakazi.
Kwani kazi zake zilizotajwa na sheria hiyo,
ni kutoa elimu, ushauri na msaada lakini wa kisheria, tena bila ya malipo ya
aina yoyote, kutoka kwa mwananchi.
Mkuu wa Idara ya Katiba na Msaada wa
Kisheria ofisi ya Pemba, Bakar Omar Ali anasema, tena walengwa wakuu wa jambo
hilo ni wananchi maskini, vijana, wanawake, watu wenye ulemavu na wale
wanaoishi katika mazingira magumu.
‘’Idara inaendelea kuwasimamia na
kuwawezesha kimafunzo kila siku wasaidizi wa sheria, ili wakawasaidie wananchi
wasiokuwa na uwezo wa kutafuta Wakili katika kutafuta haki zao,’’anasema.
Hata Mkurugenzi wa Idara hiyo, Zanzibar
Allhajjjat Hanifa Ramadhan Said, anasema Idara ilibaini kuwepo kwa kundi kubwa
la wananchi, wanaokosa haki zao na kisha kushindwa gharama za kuwalipa
Mawakili.
‘’Ndio maana sasa, serikali ililazimika
kuwa na sheria maalum ya Msaada wa Kisheria Zanzibar ya mwaka 2018, ambayo sasa
itawatambua watoa msaada wa kisheria Zanzibar,’’anasema.
Kisha wasaidizi wa sheria, waliamua
kuanzisha Jumuia zao, ili wawe wanafanyakazi kwa nguvu moja, na ndio maana
kuanzia mwaka mwaka 2015 wazo la kuanzisha CHAPO lilianza kuzaliwa.
CHAPO NI IPI
Ni Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilaya ya
Chake chake CHAPO, ambayo yenyewe iliasisiwa na kutiwa roho mwaka 2016, kwa
wakati huo, wakiwa na wanachama (wasaidizi wa sheria) 19.
Mkurugenzi Fedha wa CHAPO Riziki Hamad Ali,
anasema moja ya malengo ya ‘CHAPO’ ni kuhakikisha wananchi na hasa waliokwisha
kata tamaa, wanapata haki zao.
‘’Tukiwa sasa ndani ya miaka saba ya uzawa
wa CHAPO na siku hizi 16 za kupinga ukatili na udhalilishaji, tunayomengi ya
kujivunia, ikiwa ni pamoja na watu kupata haki zao,’’anasema.
Anasema kesi kama ya shehia ya Kichungwani,
ambayo baba wa kambu alimbaka watoto wake, ni moja ambayo wasaidizi wa sheria
kutoka CHAPO waliibua.
Kesi hiyo ilishaanza kutaka kufifia, kwa
vile familia zilishaanza kupasuka pande mbili, moja ikionekana kutokuwa tayari
kesi hiyo kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.
Anasema zipo kesi kadhaa za watoto wenye
ulemavu, ambazo wazazi walishasamehe kutokana na mazingira wanayoyakuta vituo
vya Polisi, ingawa wasaidizi wa sheria walifufua matumaini.
‘’Hivi tunavyozungumza wako washtakiwa
wanatumikia miaka 20 na wengine 25 chuo cha Mafunzo, kwa kesi ambazo sisi
wasaidizi wa sheria tuliziibua na kisha kushirikiana na wahusika, kufikishwa
mahkamani,’’anasema.
‘’Nguvu na umadhubuti wa wasaidizi wa
sheria wa wilaya ya Chake chake, imetokana na ushirikiano tunaoupata kuanzia
Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria, Jeshi la Polisi, wizara husika na
jamii,’’anasema.
Zipo kesi nyingi kama vile eneo la
Vikunguni na Ng’ambwa waathirika na familia zao zilishakata tamaa, kwamba
aliyewadhalilishi ni mtu maarufu, lakini haki mwisho ilipatikana,’’anaeleza.
Msaidizi wa sheria Ali Salim Ali, anasema
ujasiri wa kuziibua kesi za udhalilishaji na kisha kuzifikisha mbele ya vyombo
vya sheria, ni kule Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria pamoja na taasisi ya
LSF kuwawezesha kimafunzo.
‘’Kila baada ya muda, tunapewa mbinu mpya
za mapambano haya na mingine, sasa sisi wasaidizi wa sheria wa ‘CHAPO’ tumekuwa
bora kuliko taasisi nyingine kama hizi,’’anasema.
Anaona ndani ya siku hizi 16 za kupinga
ukatili na udhalilishaji na miaka saba ya CHAPO yapo mafanikio, ambayo wananchi
wameyapata na walishakata tamaa.
Wasaidizi wa sheria Abeida Ali Seif, Mgeni
Kombo Khamis, Khadija Said Khalfan na Mashavu Juma Mabrouk, wanasema hadi kufikia
mafanikio hayo, wameshavuuka mabonde yenye mamba na mashimo.
Wanasema, zipo kesi wanapozifuatilia
hutishiwa hata maisha yao na wakati mwingine, kuonekana kama vile hawafanyi
jambo la maana kwa upande mwingine, laki kazi inaendelea.
‘’Sisi kwa upande wa watu wenye ulemavu,
ndio hasa ambapo CHAPO imekuwa ikitusaidia, maana tunakotokea, ilikuwa hata
kesi moja ya mtu mwenye ulemavu huikuti mahkamani,’’anasema Mashavu.
Ndani ya siku hizi 16 za kampeni ya kupinga
Ukatili na Udhalilishaji zilizoanza Novemba 25 na zikitarajiwa kumalizika
Disemba 10, pamoja na changamoto za watu wenye ulemavu, lakini mafanikio yapo.
Anatoa mfano kuwa, wameshazisimamia kesi kadhaa
ikiwemo ya msichana aliyepwa ujauzito na Askari wa Chuo cha Mafunzo Kengeja,
kwamba ile kufika mahakamani kesi hiyo ni hatua kubwa.
Katika maisha yake, CHAPO ilishahangaika
huku na kule, kuwasaka wafadhili na kujipatia miradi kadhaa, ambayo ilikuwa ya kukoleza
mwendo wa kasi wao.
Kwa mfano, kupitia washirika wao wa The
Foundation for Civil Socity ya Tanzania, iliwahi kuwapa mradi wa ujenzi wa
amani, ambao hapa wanawake wa wilaya ya Chake chake, walijifunza mingi.
Mradi mwingine, ambao nao ulikuja kuinua
ufahamu wa wanawake wa wilaya hiyo ni wa ‘Uwezeshaji wa umiliki ardhi kwa
wanawake’ ambapo ulitoa mwelekeo.
Maana Mkurugenzi wa CHAPO Nassor Bilali
Ali, anasema miradi yote ni muhimu kwao, lakini huo wa ardhi uliwazindua
wanawake kujua haki yao ya kumiliki ardhi.
‘’Hasa ulikuwepo kwenye shehia za eneo la Pujini,
wananchi waliufurahia maana, wengi wanasema hawakuwa wakijua kuwa wana haki
hiyo, kama ilivyo kwa wanaume,’’anafafanua.
Mkurugenzi Fedha wa ‘CHAPO’ Riziki Hamad
Ali, anasema mradi ambao ulikuja hata kuwaamsha wananchi na wasaidizi wao wa
sheria ni wa ‘Upatikanaji haki’ unaofadhiliwa na tasisi ya LSF.
‘’Kwa hakika mradi huu, lazima tuwapongeze
wenzetu wa LSF, maana uliwasaidia mno wasaidizi wa sheria hata kujua wajibu wao
kwa undani na namna ya kuwahudumia wananchi,’’anasema.
WADAU/WASHIRIKA WA CHAPO
Mwakilishi wa taasisi ya LSF, Zanzibar
wakili Alphonce Gura, anasema CHAPO ni moja taasisi zinazofanya vizuri
Tanzania, katika kutetea haki za binaadamu.
Anasema wamekuwa wakijituma hata kama
hakuna maradi wa kusaidia huduma za kifedha kwa wasadizi wa sheria.
Mkuu wa Idara ya Katiba na Msaada wa
Kisheria Pemba Bakar Omar Ali, anasema lazima jumuiya nyingine ziige mfano wa
CHAPO katika mbinu za utendaji kazi.
‘’Kwa mara ya kwanza CHAPO iliandaa mafunzo
ya uwelewa wa sheria ngazi ya shehia, na walianzia shehia ya Wawi, hili ni
jambo jema na ni mafanikio yao ya miaka saba,’’anaeleza.
Mkurgenzi wa Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria
wilaya ya Mkoani Nassor Hakim Haji, anasema kazi zinazofanywa na CHAPO ni njema
na wakati mwingine, wanasoma kutoka kwao.
Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini y
CHAPO Kassim Ali Omar na Mjumbe wa bodi hiyo Zuwena Hamad Ali, wanasema sasa
jumuiya imekuwa daraja la upatikanaji haki.
‘’Watu wengi wenye kesi zao za
udhalilishaji na hata ukatili, wanawatumia wasaidizi wa sheria kupata elimu,
ushauri na msaada wa kisheria, jambo ambalo hapo kabla, ilikuwa shida,’’anasema
Zuwena.
Sheha wa shehia ya Wawi Sahrifa Wazir
Abdalla, anasema sasa CHAPO na wasaidizi wake wa sheria wamezaliwa upya, katika
mampambo dhidi ya udhalilishaji.
‘’Kwa mfano katika shehia yangu, tunao wasaidizi
wa sheria wawili, na wamekuwa masaada mkubwa kwangu, katika kuziibua kesi za
udhalilishaji,’’anasema.
Sheha wa shehia ya Mkoroshoni Khamis Iddi
Songoro na mwenzake wa Wesha Haji Mohamed Ali, wanasema wasaidizi wa sheria
kutoka CHAPO, wamekuwa wakiwasaidia kwa kiwango kikubwa.
‘’Kwa mfano, sasa wanamikutano kwa
ushirikiano kutoka shehia moja hadi nyingine, na hili sasa linawafanya wananchi
waone kuwa, jambo la udhalilishaji ni mapambano ya wengi,’’anasema sheha wa shehia
ya Wesha.
Katibu Mkuu wizara ya Maendeleo ya Jamiii, Jinsia,
Wazee na Watoto Zanzibar, Abeida Rashid Abdalla, anasema asasi za kiraia zimekuwa
na msaada mkubwa, katika mapambano ya ukatili na udhalilishaji.
Mkuu wa wilaya ya Mkoani Khatib Juma Mjaja,
anaeleza kuwa, taasisi za Jumuiya ya wasaidizi wa sheria, kama MDIPAO na CHAPO
zimekuwa mstari wa mbele, kutoa elimu ya kujiepusha na janga hilo.
Mratibu wa Chama cha Waandishi wa habari wanawake Tanzania TAMWA-Zanzibar
Ofisi ya Pemba, Fat-hiya Mussa Said, anaeleza kuwa, lazima taasisi ziongeze
ushirikiano katika mapambano hayo.
CHAPO ambayo ilianza na wasaidizi wa sheria 19, kwa sasa
wanaowanachama 23, ingawa walio hai kwa maana ya kulipa ada na kufanyakazi ni
18, wakizihudumia sheria 32 za wilaya ya Chake chake.
MWISHO.


Comments
Post a Comment