BARAZA LA WATOTO WESHA, LAWATUNISHIA MISULI WASHUGHULIKIAJI KESI ZA UDHALILISHAJI

 

 
NA MWANDISHI MAALUM, CHAPO@@@@

BARAZA la watoto wa shehia ya Wesha wilaya ya Chake chake Pemba, wamesema vitendo vya ukatili na udhalilishaji vitaendelea kuwepo na kuwaathiri, kwa vile watendaji, washughulikiaji, watoaji hukumu, wapelelezi na madaktari ni watu wazima na sio katika kundi lao.

Walisema, wapo watoto wenzao wamedhalilishwa na wengine kupata ulemavu wa kudumu na hata kusababisha vifo, ingawa kesi hizo, zinapopelelezwa na kufikishwa mahakamani, watuhumiwa huachiwa huru.

Hayo wameyasema Disemba 17, 2023 kwenye mkutano wa wazi ulioandaliwa na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ na kufanyika uwanja wa mikutano nyumbani kwa sheha wa shehia ya Wesha, wilayani humo.



Wamesema, inashangaaza kuona kesi zinazowahusu watoto kudhalilishwa au kufanyiwa ukatili, zinapelelezwa na kutolewa ushahidi, ingawa kisha hufutwa na kuwaacha wao na maumivu.

Katibu wa Baraza hilo Zainab Kassim Juma, alisema kwa vile watoto ndio wanaodhalilishwa na watu wazima, kisha wanapofika mahkamani, huachiliwa huru na watu wenzao.

‘’Sisi watoto tunadhalilishwa wakati mwengine na wazazi wetu, waalimu na hata watu wingine, lakini kesi hiyo ikifikishwa mahakamani, huachiana na kutuongezea sisi maumivu,’’alisema.




Nae mjumbe wa Baraza hilo Said Mohamed Ali, alisema, lazima wanaotetea haki za watoto wasimame imara, ili udhalilishaji wanaofanyiwa, ulipwe kupitia njia ya mahakama.

‘’Inauma kuona mtoto ameharibiwa mbele na nyuma na mtuhumiwa amepatikana, lakini ikitokea kasoro ndogo kwenye ushahidi, mtuhumiwa anaachiwa na sisi kuishi na kilema na maumivu ya kudumumu,’’alieleza.




Kwa upande wake, mtoto Samir Magessi, alisema watoto wakati mwingine wamekuwa wakitumiwa katika usafirishaji wa dawa za kulevya.


Akifungua mkutano huo, Mratibu wa wanawake na watoto wa shehia ya Wesha Waride Seif Mohamed, alisema suala la kupiga vita vitendo vya ukatili na udhalilishaji, linahitaji nguvu ya pamoja.

‘’Kama walivyofanya wenzetu hawa wasaidizi wa sheria kutoka CHAPO, kufika hapa shehia ya Wesha kuonana na watoto, ni vyema na kila mmoja, kuiga mfano huu,’’alieleza.





Katika hatua nyingine, Mratibu huyo wa wanawake na watoto shehia ya Wesha, aliwataka wazazi na walezi, kuwawekea muda wa kucheza watoto wao, ili ubongo wao upate kukua.

‘’Isiwe kila wakati watoto wanafanyishwa kazi za majumbani, wakati mwingine waachiwe kujichangamsha na wenzao, ili wapate kubadilisha uzoefu na kuendeleza ukuaji wao,’’alifafanua.

Mapema Msaidizi wa sheria wa shehia ya Wesha Khadija Said Khalfan, aliwatahadharisha watoto hao, kuacha mtindo wa kujificha vikani, wanapoamua kutohudhuria masomoni.

Aidha aliwataka watoto hao, kujitenga mbali na kupokea zawadi ovyo ovyo, na kukubali kupanda baiskeli au vyombo vya moto bila ya sababu ya msingi.






‘’Wengine wanaweza kuwapa msaada wa boda boda, kuwaonesha picha chafu au kuwapa pesa na pipi, jihadharini na ikitokezea hivyo kwa mmoja wenu, toweni taarifa,’’alieleza.

Nae Msaidizi wa sheria Jimbo la Wawi Haji Nassor Mohamed, alisema moja ya njia ya kujikinga na vitendo vya ukatili na udhalilishaji, ni kutoa taarifa za awali.

‘’Kama mtamuona mwenzenu ameanza tabia hatarishi, mfano kuchezewa chezewa sehemu zake za siri au anapewa pesa na msaada hata wa basikeli kwa mtu asiyekuwa wa kawaida, msikae kimnya,’’alifafanua.

Katika hatua nyingine, Msaidizi huyo wa sheria, aliwaahidi watoto hao, kushughulikia changamoto yao ya kukatazwa matumizi ya uwanja wa mpira wa miguu na timu kubwa ya Wesha nyakati za jioni.






Huu ni mkutano wa saba, kuendelea kufanywa na timu ya wasaidizi wa sheria kutoka shehia za Wesha, Wawi, Wara na Mgogoni wilaya ya Chake chake, kwa kukutana na makundi tofauti, kutoa elimu ya sheria.

                      Mwisho   

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’