WANAKONGAMANO: ‘RUSHWA MUHALI ITAENDELEA KUTUTAFUTA MAPAMBANO DHIDI YA UDHALILISHAJI’

 



 NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WAATHIRIKA wa matendo ya ukatili na udhalilishaji kisiwani Pemba, wamesema pamoja na juhudi za serikali kuweka mazingira ya kupungua matendo hayo ikiwemo kuweka adhabu kali, bado rushwa muhali ni kikwazo katika jamii.

Wakizungumza kwenye kongamano la siku moja la kuelekea siku 16 za kupinga ukatili na udhalilishaji, lililoandaliwa na Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba CHAPO, na kufanyika ofisi ya TAMWA Chake chake, washiriki hao walisema bado rushwa muhali ni changamoto.

Walisema bado katika jamii, suala la rushwa muhali linaendelea kujitokeza, hali inayosababisha kuimarika kwa matendo ya ukatili na udhalilishaji.

Hidaya Mjaka Ali kutoka Umoja wa watu wenye Ulemavu UWZ, alisema, serikali imezirekebisha sheria, kwa kuongeza adhabu ya kuanzia miaka 30 na kuendelea.



Alieleza kuwa kama hilo lipo, ni wajibu sasa kwa mahakim na majaji kuzifuata sheria hizo, wakati wa kutoa hukumu, waathirika wapate imani na vyombo vya sheria.

Kwa upande wake, Mratibu wa Jumuia ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake CHAPO, Mohamed Hassan Abdalla, alisema kama sheria ya Mtoto nambari 6 ya mwaka 2011, itatekelezwa ikiwemo ujenzi wa nyumba salama, inaweza kusaidia kupunguza matendo hayo.  



Mshiriki Andikalo Juma Bilali wa Chanjamjawiri, alisema bado katika vyombo vya sheria, kuna dalili ya rushwa na kusababisha wadhalilishaji kurejea makosa.

Aidha mshiriki Bakar Haji Bakar kutoka TAMWA, alishauri kuwa wakati umefika sasa, kuwepo kwa mabadiliko ya sheria, na kusababisha waliobakwa, ikiwa wametengeneza mazingira, nao kupewa hukumu.

‘’Kama sasa na wanawake waliobakwa, itaonekana wamechangia kwa njia moja ama nyingine, basi sheria iwaangalie, ili sasa kupunguza matendo hayo,’’alieleza.

Akifungua kongamano hilo, Mjumbe wa bodi ya wadhamini wa ‘CHAPO’ Zuwena Hamad Ali, alisema kila mmoja ni muathirika wa matendo hayo, hivyo lazima nguvu iwe ya pamoja.

Alieleza, iwe ni wasaidizi wa sheria, wanasheria, jamii, viongozi wa dini na wanaharakati, ni vyema tukaunganisha nguvu za pamoja katika kuzuia viashiria vya udhalilishaji.



‘’Majanga ya ukatili na udhalilishaji yapo kila eneo, sasa ni wajibu wetu sisi jamii, kushirikiana ili kuwashinda wadhalilishaji, maana kwa bahati nzuri, wamo katika jamii zetu,’’alifafanua.

Akizungumzia kuhusu elimu, alisema bado inahitajika hasa suala la ushahidi na haki za watuhumiwa, ikiwemo dhamana jambo ambalo lipo kwa mujibu wa sheria.

Mwanasheria kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Pemba, Asiya Ibrahim Mohamed, aliwashauri wahanga wa matukio ya udhalilishaji, kuendelea kutumia ofisi yao, wanapoona kesi zao, haziendi vyema.

‘’Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, ipo kwa ajili ya kusimama na wahanga wa jinai, hivyo wananchi hawanabudi kuendelea kufikisha malalamiko yao, ili kupatiwa ufumbuzi unaofaa,’’alifafanua.




Kuhusu idadi ya mashahidi, alisema hakuna haja ya kuwa na idadi ya kundi la mashahidi, bali muathirika na mtendaji wakati mwingine inatosha kumaliza kesi.

‘’Wazazi, madaktari, Polisi mpelelezi na watu wa karibu ni kama kuongeza nguvu ya ushahidi, katika mambo mbali mbali, ikiwemo umri, suala la ruhusa na muda wa tukio husika,’’alifafanua.





Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba, CHAPO Nassor Bilali Ali, alisema lengo la siku 16 za kupinga ukatili na udhalilishaji, ni kujadili changamoto na mafanikio katika mapambano hayo.



Alieleza kuwa, CHAPO imekuwa ikikutana na makundi mbali mbali kama wanafunzi, watu wenye ulemavu, viongozi wa dini, wahanga wa matukio ya udhalilishaji na wasaidizi wa sheria.

                                      Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’