‘TCACL’: ELIMU IWE NYUNDO YA KUVUNJIA VIKWAZO VYA MTOTO WA KIKE’
NA HAJI NASSOR, PEMBA
MKUU wa Program za Mtandao wa Kupinga Utumikishwaji wa
Watoto Tanzania ‘TCACL’ Adam Matiko Charles, amesema wakati Afrika, ikiadhimisha
siku ya haki za binaadamu, lazima jamii iondokane na mawazo pekee kuwa, elimu
ni haki ya msingi, na waifanye kuwa nyundo ya kuvunja vikwazo kwa mtoto wa
kike.
Alisema, jamii bado inamtazamo wa zamani juu ya elimu, kama
haki ya kawaida ya msingi kwa mtoto, lakini wakati umefika sasa, kuifanya
nyundo yenye kuvunja na kupasua vikwazo, vinavyomzungumka mtoto wa kike.
Mkuu huyo wa Program, aliyasema hayo skuli ya msingi ya Dk. Philipi
Mpango, Gombani Chake chake kisiwani Pemba, wakati akizungumza na wanafunzi,
waalimu, wazazi na watetezi wa haki za binaadamu, kwenye maadhimisho ya siku ya
haki za binaadamu Afrika.
Alisema, siku hiyo ni muhimu kwa jamii, kuangalia ikiwa kuna
vikwazo mbali mbali kwa mtoto wa kike, na kuangalia uwezekano kwa kuviondosha
kupitia elimu wanayoipata.
‘’Kwa sasa, lazima elimu bora na yenye manufaa kwa mtoto wa
kike, isiwe kama anasa, bali iwe msingi mkuu wa kumuwezesha kijinasua na majanga
mbali mbali kama ya udhalilishaji, ukatili wa kingono,’’alieleza.
Kataika hatua nyingine alisema, wakati umefika sasa kwa asasi
za kiraia, mashirika pamoja na serikali kuu, kuunganisha nguvu za pamoja, ili kupinga
utumikishwaji wa watoto Tanzania.
‘’Kwa mfano utumikishwaji, ajira za utotoni, ukatili wa kijinsia,
kukoseshwa haki za elimu, matunzo, afya bora na makuzi na malezi ambayo ndio
msingi mkuu wa maisha yao baadae,’’alieleza.
Kuhusu Mtandao huo, Mkuu huyo wa Program alisema, kuwa wanaowanachama
40 kwa Tanzania bara na Zanzibar, ambapo wamekuwa wakihakikisha watoto wanakuwa
salama, katika nyanja mbali mbali za maisha yao.
Mapema Afisa Elimu na Mafunzo ya Amali wilaya ya Chake chake,
Bur-han Khamis Juma, aliwataka watoto, kuweka pembeni anasa na kushughulikia zaidi
elimu, ambayo ndio mkombozi wao wa baadae.
Alieleza kuwa, wakati huu wizara ya elimu na Mafunzo ya Amali
ikiendelea kuweka miundombinu rafiki ya kujipatia haki ya msingi ya elimu, ni
vyema wanafunzi wakakaza kamba, wanapokuwa masomoni.
‘’Wizara imekuwa ikijenga miundombinu ya kisasa ya elimu,
pamoja na upatikanaji wa vitabu, sasa ni wajibu wenu wanafunzi kusoma kwa bidi,
ili ufaulu uongezeke,’’alieleza.
Akizungumzia kuhusu siku ya haki za binaadamu barani Afrika,
alisema ni siku ya kutafakari juu ya haki za binadamu, zinavyovunjwa na baadhi
ya watu, jambo linahatarisha maendeleo katika sekta mbali mbali.
Kwa upande wake Mwakilishi wa Jumuiya za wasaidizi wa sheria
Pemba ‘JUWASPE’ Nassor Bilali Ali, alisema kama jamii haikuweka mkazo katika
kuzilinda haki za binaadamu, kunaweza kukaendelea kuripotiwa visa kadhaa.
‘’Kila mmoja, na kwa nafasi yake anayonafasi ya kuzilinda
haki za binaadamu, na wala hakuna sheria au kanuni, inayohalalisha watu kujichukulia
sheria mikononi, maana vyombo husika vipo,’’alieleza.
Mwalimu mkuu wa skuli hiyo Halima Khamis Salim, alisema
maadhimisho hayo kufanyika skulini kwake, kumesaidia kuwaasha watoto, namna
bora ya kudai haki zao mbali mbali.
Sheha wa shehia ya Kwale Khamis Salim Ali, alisema vyombo vya
sheria vinawajibu wa kutoa adhabu kali, kwa washtakiwa wa makosa mbali mbali ya
ukatili wa kijinsia.
Hii ni mara ya kwanza kwa Mtandao wa kupinga utumikishwaji wa
mtoto Tanzania ‘TCACL’ kufanya maadhimisho ya siku ya haki za binaadamu Afrika,
ambapo ujumbe wa mwaka huu ‘haki ya elimu bora kwa wote na haki kwa
Afrika’, awali kulitanguliwa na matembezi ya wanafunzi, waalimu na
watetezi wa haki za binaadamu.
Mwisho



.jpg)




.jpg)


Comments
Post a Comment