CHAPO YAACHA UJUMBE KWA WANAOWAFUNGIA NDANI WATU WENYE ULEMAVU

 

 



NA MWANDISHI MAALUM, CHAPO@@@@

JUMUIYA ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba CHAPO, imewataka wananchi wa kijiji cha Tondooni, shehia ya Wesha wilayani humo, kujua kuwa, kumfungia ndani mtu mwenye ulemavu, ni kosa kisheria kwa vile kumkosesha haki zake za binaadamu.

Wito huo umetolewa na Msaidizi wa sheria jimbo la Wawi Haji Nassor Mohamed, wakati, akiwasilisha mada ya haki za binaadamu, kwa wananchi wenye ulemavu, kwenye mkutano wa wazi, ulioandaliwa na ‘CHAPO’ na kuendeshwa na wasaidizi wa sheria.



Alisema, hakuna sababu ya mzazi, mlezi kumfungia ndani mtoto mwenye ulemavu, kwa sababu ya ulemavu wake, hivyo kisheria anatakiwa kupelekwa kwenye vituo vya elimu, bila ya kujali aina ya ulemavu aliyonao.

Alisema, serikali kwa upande wake imeshaweka mazingira rafiki kiasi, kwa wanafunzi wenye ulemavu na mahitaji maalum, ikiwemo kuanzisha madarasa mjumuishi, kuweka vitengo pamoja na kuanzisha sheria ya kuwalinda.



‘’Kwa mfano ipo sheria mpya ya watu wenye ulemavu Zanzibar nambari 8 ya mwaka 2022, baada ya kufutwa ile ya mwaka 2016, sasa ni wajibu wa wazazi na walezi, kuona wanawapatia elimu na haki zao nyingine kundi hilo,’’alieleza.

Akitaja miongini mwa haki za binaadamu kwa watoto au watu wenye ulemavu alisema ni elimu, matunzo, mavazi, matibabu, kushirikishwa, kuoa na kuolewa, malazi na chakula bora.

Hata hivyo, aliwataka wazazi kuwatoa nje watoto waliowafungia na kuwaandikisha skulini, ili wapate haki zao za elimu, na kuacha visingizio vya hali baya waliyonayo watoto hao.

Kwa upande wake, Msaidizi wa sheria Jimbo la Chake chake Wahida Kombo Khamis, amewatahadharisha watoto, kutokubaliwa kurubuniwa kwa kupewa zawadi au fedha na watu wasiowajua.

Alisema, kwa sasa wadhalilishaji hutumia fedha kidogo au kuwaonesha watoto picha chafu kupitia simu janja, na kisha kupata mwanzo wa kuwadhalilisha kingono, jambo ambalo, huwaharibia maisha yao.




‘’Pendeleeni sana mnapokwenda na kurudi skuli ama madrasaa, muwe mnafuatana kwa kundi na anapopata shida mwenzenu, kimbilieni kutoa taarifa kwa wazazi, walezi, waalimu au watu wengine wa karibu,’’alieleza.

Akieleza lengo la mikutano hiyo ya wazi Msaidizi wa sheria Jimbo la Ziwani Khadija Said Khalfan, alisema CHAPO imekuwa ikiwafikia wananchi katika maeneo yao, ili kuhakikisha wanapa uwelewa wa masuala la kisheria.

Alieleza kuwa, pamoja na kuwa na jukumu la kutoa elimu kwa wananchi wanaofika ofisini kwao mjini Chake chake, lakini wameona ni bora kwenda katika vijiji mbali mbali kuwafuata.

‘’CHAPO ambayo ni taasisi ya kiraia, inawakaribisha kuja ofisini kwetu kupata elimu, ushauri na msaada wa kisheria, kwa kesi yeyote tena bila ya malipo, maana hilo ndio jukumu letu kuu na la msingi,’’alieleza.




Mapema sheha wa shehia ya Wesha Haji Mohamed Ali, alisema mpango ulioandaliwa na CHAPO, unasaidia mno kuwaamsha wananchi hasa wanaozikalia haki za wengine.

‘’Ni kweli wapo wananchi, wamewafungia ndani watoto wenye ulemavu na wamekuwa wakiwakosesha haki zao kama za chanjo, elimu na hata kuwashirikisha, imekuwa ni vigumu,’’alieleza.



Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Tondooni akiwemo Khadija Mohamed Salim, walisema, ipo tabia ya kufungiwa ndani watoto wenye ulemavu, wazazi wakidai kuwa hawana uwezo wa kusoma.

Hata hivyo, alisema bado baadhi ya madrassa za Qur-an zinakabiliwa na ukosefu wa vyoo na maji safi na salama, jambo linalowafanya wanafunzi kujisaidia vichakani.

Mkutano huo wa wazi, ni muendelezo wa watendaji wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake CHAPO, kukutana na wananchi, ili kusikiliza kero zao kisheria.

                      Mwisho  

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’