WASAIDIZI WA SHERIA 'CHAPO' WATOA UJUMBE KWA WANAFUNZI

 



Na, Hassan Msellem, Pemba

 

WANAFUNZI skuli ya Sekondari ya Dk. Salim Ahmed Salim iliyopo Wara wilaya ya Chake -chake Pemba, wametakiwa kujiepusha na vitendo vya udhalilishaji na utumiaji wa dawa kulevya, ili kufikia malengo waliojiwekea.

 

Akitoa elimu ya msaada wa kisheria kwa wanafunzi hao  Septemba 11, 2023, Msaidizi wa Sheria shehia ya Wawi Haji Nassor Mohamed, alisema tafiti zinaonesha kuwa, waathirika wakuu wa vitendo hivyo, ikiwemo ubakaji, ulawiti na ukatili wa kijinsia, ni wanafunzi skuli.

 

Aidha amewasihi wanafunzi hao, kuwatumia wasaidizi wa Sheria, ili kupata ufumbuzi juu ya changamoto mbali mbali za kisheria, zinazowakabili.

 

"Udhalilishaji ni kumfanyia mtu kitendo chochote, ambacho kitamuathiri kimwili, kiakili au kisaikolojia, hivyo ni vyema mkajiepusha na hili,’’alieleza.




 

Nae Msaidizi wa Sheria Jimbo la Wawi Fatma Hilal, amesema miongoni mwa sababu zinazochangia baadhi ya wanafunzi kushindwa kuendelea na masomo na kutokutimiza ndoto walizojiwekea ni pamoja utumiaji wa dawa za kulevya.

 

"Kuna athari nyingi sana za utumiaji wa dawa za kulevya na miongoni mwa athari hizo, ni mabadiliko hasi ya kitabia ambayo mabadiliko hayo yanapelekea wizi, ubakiji, ulawiti kama ni mwanafunzi unapotumia tunaweza kushindwa kuendelea na masomo,’’alifafanua.

 



Kwa upande wake Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la Polisi kutoka Shehia za Wawi na Wara Inspekta Issa Ahmada Iddi, amewasihi wanafunzi hao, kuachana na dhana kuwa, mwanafunzi hawezi kuchukuliwa hatua za kisheria, pindi anapofanya kaso, jambo ambalo sio sahihi.

 

Akifunga mkutano huo mwalimu Mkuu wa Skuli hiyo Khamis Said Othman, amewasihi wanafunzi hao kuwa karibu zaidi na walimu wao, ili kufahamu changamoto zinazowakabili na kuweza kupatiwa ufumbuzi wa haraka.

 

"Mimi ni wasihi tu kuwa licha ya kupata elimu hii ya kupinga udhalilishaji na athari za matumizi ya dawa za kulevya, bado muelewa kuwa, mshauri wenu mkuu ni waalimu kabla ya kuzifikisha popote,’’alifafanua.

 


 Sheha wa shehia ya Wara, Massoud Mohamed Khamis aliwakumbusha wanafunzi hao, kuwaripoti kwenye vyombo vya sheria wazazi na walezi, ambao wanajihusisha na vitendo viovu ikiwemo, vya ulevi na udhalilishaji.

 

"Tunafahamu kuwa wapo baadhi ya wazazi na walezi wenye tabia mbaya, ikiwemo ya ulevi, wizi pamoja na kuwadhalilisha watoto kingono, naomba niwaambie kuwa musiwavumilie watu wa aina hii, na msisite kutoa taarifa kwa walimu wenu,’’aliwakumbusha.

 



 

Nao baadhi ya wanafunzi hao wameahidi kuifanyia kazi elimu hiyo, ili kufanya vizuri katika masomo sambamba na kutimiza ndoto walizojiweke.

 

"Kwakweli leo tumejifunza mambo mengi sana, kuhusu udhalilishaji na athari ya matumizi ya dawa za kulevya, na tunaahidi kuitumia elimu hii katika kipindi chote cha maisha yaetu,’’walisema wanafunzi hao.

  

Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria Wilaya ya Chake Chake (CHAPO), kwa sasa imo katika mkakati maalum wa kukutana na makundi kadhaa, kutoa elimu, ambapo hivi karibuni ilikuwa shehia za Mvumoni, Wesha, Kilindi, Ole, Ziwani na Uwandani.  

                   MWISHO

 

 

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’