CHAPO: ‘WARIPOTINI WAZAZI, WAALIMU, WAJOMBA WANAOTAKA KUWADHALILISHA''
NA
MWANDISHI WETU, PEMBA
WANAFUNZI
wa chuo cha Kur-an cha Kichangani shehia ya Mgogoni Jimbo la Wawi, wilaya ya
Chake chake Pemba, wamekumbushwa kuwaripoti wazazi, waalimu, walezi na watu wengine,
wanapoona dalili za wao, kutaka kudhalilishwa.
Walieleza kuwa, moja ya dalili hiyo ni mtu huyo kuongeza
mapenzi ya kupindukia, kumpa zawadi zisizotarajiwa na kumshika shika sehemu
nyeti za mwili wake, ikiwemo kifuani na makalio.
Ushauri huo umetolewa na Msaidizi wa sheria, Jimbo la Wawi
Fatma Hilali, wakati akizungumza na wanafunzi hao na waalimu, kwenye mkutano wa
wazi, wa utoaji elimu, juu ya namna ya kujikinga na majanga yakiwemo ya
udhalilishaji.
Aliwaambia wanafunzi hao kuwa, dalili nyingine ni kupigwa
mabusu sehemu tofauti za mwili, kupewa fedha na hasa na mtu asiyemjua pamoja na
kupakatwa.
‘’Wanafunzi mkiona kuna dalili za kawaida, mtu anakushika
kwenye mashavu, makalio, kifuani, mbavuni, anakupa pesa na hasa kwa mtu wa nje,
pipi toweni taarifa kwa waalim au wazazi,’’alisema.
Katika hatua nyingine, Msaidizi huyo wa sheria, alisema moja
ya athari za udhalilishaji kwa watoto, ni kupata athari ya viungo vya uzazi,
kiakili, kupoteza mwelekeo wa masomo.
Kwa upande wake Msaidizi wa sheria wa shehia ya Wawi Haji
Nassor Mohamed, aliwataka wanafunzi hao, kuacha michezo inayopelekea kugusana
sehemu zao nyeti, ikiwemo makalio.
‘’Kuna michezo hasa kwa wanafunzi wa kike, ya kupigana
makofi kwenye makalio na kisha kufukuzana, na kwa wanaume kuchezeana chezeana
ovyo, michezo hii inaweza kuzaa janga, iacheni,’’alieleza,
Akizungumzia haki za watoto kwa mujibu wa sheria ya Mtoto
nambari 6 ya mwaka 2011, alisema ni pamoja na kupewa jina zuri baada ya
kuzaliwa, matibabu, elimu, matunzo, kulindwa pamoja na kusikilizwa.
Aidha aliwaeleza wanafunzi hao kuwa, wajibu wao kwa jamii,
ni kuwatii wazazi, walezi, waalimu, kushiriki kwa mambo yanayowahusu, kushughulikia
masomo na kutoa taarifa zinazoweza kusababisha madhara kwao.
Mapema Mratibu wa wanawake na watoto shehia ya Mgogoni
Khadija Ramadhan Mbwana, aliwataka wanafunzi hao, kuacha tabia ya kujificha
vikachakani.
‘’Wapo wanafunzi wanaondoka nyumbani, lakini wanaishia
vichakani na ikifika wakati wenzao wanarudi madrassa nao huungana pamoja, jambo
sio zuri,’’alikemea.
Katika hatua nyingine, Mratibu huyo alipongeza utaratibu wa ‘CHAPO’
wa kuunda timu ya wasaidizi wa sheria, kupita katika makundi ya jamii, kutoa
elimu ya majanga mbali mbali.
Akifungua mkutano huo, Mwalimu mkuu wa Madrassa hiyo Mohamed
Ali Omar, alisema njia ya ushirikiano katika kuwalinda watoto na majanga,
inaweza kuwasaidia kuwaweka salama.
‘’Kama wazazi, walezi, waalimu, wasaidizi wa sheria na
serikali tukiungana kuwalinda watoto, wahalifu wanaweza kukoma, kwani kwa sasa
mashambulizi yanaelekezwa kwao,’’alieleza.
Mwalimu Zaina Jongo Juma, alisema lazima msisitizo mkali wa
kisheria uwepo, kwa watakaobainika kuwafanyia vitendo vya udhalilishaji watoto.
Wanafunzi katika Madrassa hiyo, wameahidi kuyafanyiakazi
maagizo na makatazo waliyoelezwa, pamoja na kuifikisha elimu hiyo kwa wenzao.
Utafiti
uliofanywa na Chama cha waandishi wa habari Wanawake Tanzania TAMWA-Zanzibar
miaka mitatu iliyopita, umewaibua baba wazazi13, waliowafanyia ubakaji
watoto wao wa kuwazaa, kati ya hao tisa (9) Unguja na watatu (3) kisiwani Pemba.
Ilibainika
pia kuwa, baba walezi na wakambo 25, Unguja wakiwa 13 na Pemba 12 waliowabaka
watoto wao wa kuwalea katika mazingira tofauti.
Mwisho




.jpg)

Comments
Post a Comment