MVUMONI CHAKE CHAKE WAOMBA KUONANA NA DK. MWINYI
NA HAJI
NASSOR, PEMBA@@@@
WANANCHI
wa shehia ya Mvumoni wilaya ya Chake chake, wameomba kuonana na Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, ili
kumfikishia kilio chao cha ya kucheleweshewa fidia zao, katika utanuzi wa uwanja
wa ndege Pemba.
Walisema, walifanyia tathmini za nyumba, miti na vipando vyengine
tokea mwaka 2015, juu ya utanuzi wa uwanja wa ndege Pemba, ingawa hadi leo, hawana
taarifa rasmini juu ya tathmini hiyo ilipofikia.
Wakizungumza mbele ya watendaji wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria
wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ waliofika shehiani hapo, kutoa elimu na
msaada wa kisheria, walisema sasa uvumilivu umewashinda.
Wananchi hao walisema, kwa sasa hakuna kiongozi ambae anaweza kuwapa
maelekezo na wakayakubali, isipokuwa awe ni Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Ali
Mwinyi pekee.
Walisema kiongozi huyo amekuwa mkweli na mtendaji kwa vitendo, hivyo
wameziomba mamlaka husika, kuzungumza nae ili awasili shehiani humo, na kumpa
kilio chao.
Mmoja kati ya wananchi hao, Abdalla Seif alisema ni vyema kwa Rais wa
Zanzibar kuwafika, ili kumuelezea changamoto wanazopitia kwa sasa.
‘’Sisi kwa sasa hatujengi, hatuendelezi vipando vya kudumu kwa zaidi
ya miaka saba sasa, tunamuomba sana Rais wa Zanzibar atufike, ili atupe
mrejesho wa tathmini zetu,’’alisema.
Nae mwananchi Alei Seif Said, alisema wamekuwa hawajui hatma ya maisha
yao, baada ya kufanyiwa tathmini zaidi ya mara moja, juu ya utanuzi wa uwanja
wa ndege Pemba.
Kwa upande wao Abdalla Ali Said, Khamis Jama na Yahya Said Seif,
walisema ni vyema sasa kwa serikali ikaanza kuwalipa fidia zao, ili wakaanze
maisha mapya, katika maeneo mengine.
Walieleza kua, wanashindwa kupanda vipando, kuendeleza ujenzi wa
nyumba zao kutokana na kuchelewa malipo ya faidia zao.
Mapema Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake
chake Pemba ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, aliwataka wananchi hao, kushirikiana na
CHAPO, ili kujua changamoto.
‘’Njooni CHAPO tuangalie wapi kuna mkwamo, ili tufuatile kwa pamoja,
suluhisho ya upatikanaji wa fidia zenu kwa haraka,’’alieleza.
Aidha Mkurugenzi huyo, aliwataka wananchi hao kusubiri kwanza, hadi
serikali iingize fidiai zao kwenye akaunti, ambapo kisheria wanaweza kukata
rufaa hapo baadae, ikiwa hakuridhika.
Katika hatua nyingine, Mkurugenzi huyo alisema, tayari tathimi zao,
zimeshakuwa kwa mthamini mkuu wa serikali, kwa ajili ya hatua nyingine ya
malipo yao.
Afisa Mipango wa Shirika la Msaada wa Kisheria na Haki za Binaadamu
Zanzibar ‘ZALHO’ ofisi ya Pemba Siti Habib Mohamed, aliwataka wananchi hao
kurudi, kwao ikiwa kutajitokeza changamoto za fidia zao hapo baadae.
‘’Jamani jambo la serikali lazima lifuate taratibu zote, ili
kuhakikisha hakuna mwananchi amekoseshwa haki yake, na ndio maana ukaona kama
mnacheleweshwa,’’alifafanua.
Mwanasheria kutoka Idara ya Ardhi Pemba, Asha Suleiman Said, alisema hakuna mwananchi atakayehamishwa, pasi na kulipwa fidia yake kisheria.
‘’Serikali haijawahi kufanya hata mara moja, kumuondoa mwananchi
katika eneo husika, pasi na kumlipa fidia, na hataka kama ikiwa ndogo unaweza
kukata rufaa,’’alifafanua.
Tayari Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, imeshasaini Mkataba
wa Ujenzi wa uwanja wa ndege Pemba, kupitia Kampuni ya PROPAV/MECCO JV ya
Hispania.
Ambapo kwa mwaka wa 2022/2023, Mradi ulipangiwa kutumia zaidi ya shilingi
bilioni 134.100, kati ya fedha hizo shilingi bilioni 8,000,000,000 ni kutoka
Serikalini na shilingi bilioni 126.100 ni kutoka kwa mfadhili, ingawa hadi
mwezi Machi, 2023 hakuna fedha iliyopatikana.
Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba, CHAPO imo katika utekelezaji wa mpango
wake kazi, wa kuwafikia wananchi mbali mbali, ili kuwasikiliza changamoto zao
kisheria.
Mwisho







Comments
Post a Comment