WAWI WAUKUBALI USHAURI WA MSAIDZI WA SHERIA UJENZI WA OFISI YA SHEHA

 




NA MWANDISHI WETU, CHAPO@@@@


UONGOZI wa shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake, umesema umeridhia usahuri wa Msaidizi wa sheria wa Jimbo la Wawi, la kutaka kuanzisha ujenzi wa ofisi ya sheha, shehiani humo.


Ulisema, wazo la Msaidizi wa sheria wamelipokea mikono miwili, kwani imekuwa ni usumbufu wanapokuwa na mikutano yao mbali mbali, hasa katika kipindi cha jua au mvua.


Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, leo Juni 16, 2023 Sheha wa shehia hiyo Sharifa Waziri Abdalla, alisema baada ya kulifikisha wazo hilo kwa wajumbe wake, wamelipokea na kusema linawezekana mno kutekelezwa.


Alisema, fikra hiyo imekuja wakati mwafaka, wakati serikali kuu nayo ikihimiza ujenzi wa ofisi za masheha, ili sasa waondokane na kufanyakazi kwenye makaazi yao.


Alieleza kuwa, wazo hilo ambalo aliahidi kulisimamia, linaweza kutekelezwa, hasa kwa umoja na mshikamano, uliopo ndani ya shehia ya Wawi.


‘’Ni kweli tumeupokea na kuukubali ushauri wa Msaidizi wetu wa sheria wa Jimbo la Wawi, la kuomba kuanzishwa kwa ofisi ya sheha, maana inaweza kuwa chachu ya mafanikio,’’alieleza.


Katika hatua nyingine, sheha huyo wa shehia ya Wawi, aliwataka wajumbe wake kuusambaaza ujumbe huo kwa wananchi, ili wakati wa kuataka kuanza ujenzi ukifika wawe na uwelewa.


Aidha sheha huyo alimpongeza Msaidizi huyo wa sheria kwa ujio wa wazo hilo, na kusema amesaidia katika kuleta mabadiliko ya haraka ndani ya shehia.




Akizungumzia kushirikiana na Msaidizi huyo wa sheria, aliwataka wananchi kuendelea kumtumia, kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa masuala mbali mbali ya kisheria.


‘’Kama kuna migogoro kama ya ardhi, matunzo, huduma za mtoto, mipaka, madeni kuendelea kushirikiana nae, ili kufikia sulhu, badala ya kwanza kukimbilia Polisi,’’alieleza.


Mjumbe wa sheha wa kijiji cha Mtemani Nassor Rashid Said, alisema kilichobakia kwa wananchi wa shehia ya Wawi, ni kusimama wima juu ya ujenzi huo.


‘’Hili jambo alilolita Msaidizi wa sheria wa Jimbo la Wawi, ni zuri na linafaa kuungwa mkono, na kwetu sisi ni kufanya ufuatiliaji,’’alishauri.


Nae mjumbe wa sheha Khamis Mwinjaa, aliwata wajumbe wenzake, kuendelea kushirikiana kwa karibu, ili kuijenga shehia yao.


Kwa upande wake Mratibu wa wanawake na watoto shehia ya Wawi Fatma Kassim, alisema ofisi hiyo itakapojengwa, itatoa nafasi pana wakati wa kutoa ushauri nasihi, kwa wahanga wa udhalilishaji.


‘’Hivi sasa inabidi wahanga tunakaa nao barazani kuwapa ushauri nasihi, lakini kama kuna wazo la ujenzi wa ofisi, litasaidia mno, katika kusukuma mbele maendeleo,’’alieleza.




Wakizungumza kwa niaba ya wasaidizi wa sheria wenzake, Haji Nassor Mohamed na  Asha Hilali, walisema ni kweli hivi karibuni, waliishauri Kamati ya sheha wa shehia ya Wawi, juu ya kuanzisha ofisi hiyo.


‘’Tuliona vikao vya sulhu vinafanyika barazani kwa sheha, uwanjani, au wakati mwengine kwenye majengo ya kiimani ya kichama, tukaona sio sahihi,’’walieleza.


Wasaidizi hao wa sheria walisema, wazo hilo wanatarajia litafanyiwa kazi, ili kuona shehia ya Wawi, inakuwa na ofisi yake kwa ajili watendaji, kuendesha kazi zao kwa ufanisi.


Mkurugenzi wa Jumuia ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba, CHAPO Nassor Bilali Ali, alipongeza wazo la wasaidizi hao wa sheria, jimbo la Wawi kwa kufikisha wazo hilo shehiani.




Alieleza kuwa, wasaidizi wa sheria wamepelekwa kwa maksudi shehiani, ili kwenda kusaidia utatuzi wa changamoto mbali mbali za kisheria, pamoja na upatikanaji huduma mbali mbali kwa njia ya mashauriano.


‘’Ni kweli pamoja na majukumu ya msingi ya Msaidizi wa sheria kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria, lakini kama kuna ushauri wa kufanikisha mambo mengine, inakubalika,’’alieleza.


Hata hivyo Mkurugenzi huyo, amewataka wasaidizi wengine wa sheria, kuwa wabunifu katika shehia zao, ili wananchi waendelee kupunguza changamoto.


Katika hatua nyingine Mkurugenzi huyo, aliushauri uongozi wa shehia ya Wawi, kufikiria ikiwa eneo litatosha, kuanzisha chumba cha Msaidizi wa sheria na Mratibu wa wanawake na watoto.


‘’Kwa sasa nguvu ya serikali ni ngazi ya shehia, hivyo napendekeza kwenye ofisi hiyo, kiwemo chumba na Msaidizi wa sheria na Mratibu, ili kutoa nafasi kwa wananchi, kupata ufumbuzi wa changamoto zao kwa ufanisi,’’alipendekeza.

Tayari uongozi wa shehia ya Wawi, umeanza harakati za kutafuta eneo maalum kwa ajili ya ujenzi wa ofisi hiyo, sambamba na kutaka kuteua kamati ya muda ya ujenzi.

                           Mwisho    

 

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’