‘’MLIOPEWA MAFUNZO WA SHERIA WAWI WAHAMASISHENI WANANCHI KUDAI HAKI ZAO’' CHAPO

 


NA MARYAM SALUM, PEMBA@@@@

KAIMU Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba, ‘CHAPO’ Kassim Ali Omar, amewataka wahitimu wa mafunzo ya sheria, kutoka shehia ya Wawi, kuwahamasisha watu kudai haki zao mbali mbali.

Wito huo aliutoa leo Juni 19, 2023 Vikutani shehiani humo, kwenye ufungaji wa mafunzo ya siku ya tano, ya sheria kwa wajumbe wa kamati ya sheha na kamati nyengine, za shehia ya Wawi.

Alisema, anaamini kwa mafunzo hayo, washiriki hao watakuwa waalimu wazuri kwa wenzao, katika kuwahamasisha kudai haki zao mbali mbali badala ya kuwakatisha tamaa.

Alieleza kuwa, ndani ya mafunzo hayo wamejua mambo ambayo yanaweza kusababisha kesi kufutwa, kuondolewa au mtuhumiwa kutumikia kutiwa hatiani.

‘’Mimi naamini kwa mafunzo haya mliopewa ya sheria ngazi ya shehia, mtakuwa na uwezo kuwahamasisha wale waliokata tamaa, kwenda kudai haki zao, mbali mbali,’’alieleza.

Katika hatua nyingine, Kaimu Mwenyekiti huyo wa Bodi ya wadhamini wa CHAPO Kassim Ali Omar, alisema wakati umefika sasa, wa kuunganisha nguvu katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya na udhalilishaji.




 ‘’Jamii yetu inazungumkwa na udhalilishaji, dawa za kulevya, migogoro ya ardhi, ndoa hivyo mafunzo haya sasa, yatuunganishe pamoja kuyashinda majanga hayo,’’alieleza.

Akizungumzia kuhusu uwepo wa wasaidizi wa sheria katika shehia ya Wawi, alisema hiyo ni faraja na kuwataka wananchi kuendelea kuwatumia.

‘’Kwa hakika, hili la wasaidizi wa sheria shehia ya Wawi na uongozi wa ‘CHAPO’ kubuni mafunzo haya, ni jambo linalofaa kuendelezwa, katika shehia nyingine,’’alieleza.

Alisema kuwa, lengo kuu la kuanzishwa kwa wasaidizi wa sheria kwa kila shehia, ni kuona kwamba ile migogoro isiyokuwa ya lazima kwa wananchi, inapungua.

Mapema Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake Chake Pemba ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, alisema mafunzo hayo, wanakusudia kuyasambaaza katika shehia zote 32 za wilaya hiyo.



Alieleza kuwa, lengo la kufanya mafunzo hayo, ni kuona  wanatatua ile migogoro ambayo siyo ya lazima, kwa jamii ili kwenda sambamba na upatikanaji wa haki zao.

“Tunalengo la kuibadilisha jamii katika kutatua migogoro hasa kwa ile isiyokuwa ya lazima, ikiwemo ya mirathi, ardhi, matunzo ya watoto, hivyo ni imani yangu kuwa, mafunzo haya yatazaa matunda,” alieleza.

Hata hivyo aliupongeza uongozi wa shehia ya Wawi wilaya ya Chake chake, kwa kushirikiana vyema na CHAPO, hadi kufanikisha mafunzo hayo ya kwanza kwa Zanzibar.

Kwa upande wake Mratibu wa mafunzo hayo, ambae pia ni Msaidizi wa Sheria Jimbo la Wawi Chake Chake, Haji Nassor Mohamed alisema kuwa mafunzo hayo, yalengo la kuelimisha jamii, juu ya upatikanaji wa haki.

Hivyo aliwataka washiriki hao kuyatumia vyema mafunzo waliyopewa, kwa kuyafanyia kazi, ikiwemo kuwapatia wengine, ili yaweze kuleta matunda hapo baadae.

Sheha wa Shehia ya Wawi Sharifa Waziri Abdalla, alieleza kuwa wanaimani kwamba mafunzo hayo, yatakuwa chachu ya maendeleo katika shehia yao.



‘’Kwa hakika mpango wa kuwepo kwa wasaidizi wa sheria katika shehia, umekuja kuimarisha upatikanaji wa haki na utatuzi wa migogoro, na mfano mzuri ni hapa Wawi,’’alieleza.

Mmoja wa washirikia hao Juma Mohamed Tamimu alisema kuwa, mafunzo hayo yataleta tija katika shehia yao ya Wawi.

“Kuna mambo mengi tulikuwa hatuyafahamu, baada mafunzo haya ya kisheria, tumelewa njia za kutafuta haki, tumeweza kujua mengi na tutahakikisha tutawapatia na wenzetu ili waondokane na migogoro mbali mbali,” alieleza.

Nae Mtama Mohamed Mohamed, alisema kazi iliyobakia mbele yao ni kuyanfanyia kazi mafunzo hayo, ili yalete tija kwa wananchi mbali mbali hasa wasiokuwa na uwezo.

‘’Miongoni mwetu wamo pia wajumbe wa kamati ya sheha ambao wamekuwa wakipokea migogoro kila siku, sasa mafunzo haya yatakuwa chachu ya kufanikisha kazi zetu,’’alieleza.



Nao Fatma Kassim na Khamis Mwinjaa, walisema mafunzo hayo ni vyema, yakawa endelevu kwa makundi mengine ndani ya shehia, ili kuhakikisha kila mmoja amepata uwelewa.

 Mafunzo hayo ya siku tano, yameandaliwa kwa pamoja kati ya Jumuia ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake Chake Pemba ‘CHAPO’ na uongozi wa shehia ya Wawi, ambapo mada 12 zilifundishwa ikiwemo Mirathi, sheria ya mtoto, sheria ya aradhi, sheria ya Ushahidi pamoja na aina za ukamati kisheria.

                                                 MWISHO.

 

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’