‘CHAPO’ YAWAKOSHA WANANCHI KILINDI ELIMU YA SHERIA

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

WANANCHI wa kijiji cha Kuungeni shehia ya Kilindi wilaya ya Chake chake Pemba, wamesema mfumo uliofanywa na Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ kuwafuata kijijini kwao na kuwapa elimu ya kisheria, inafaa kuendelezwa.

Walisema, mfumo huo unafaa kuendelezwa na kuwa imara zaidi, kwani umewasaidia katika kukuza uwelewa wao, hasa masuala la haki na fursa zao kisheria.

Wakizungumza kwenye mkutano wa wazi, uliofanyika Mei 14, 2023 kijijini hapo, walisema wamepata uwelewa wa mambo kadhaa, ikiwa ni pamoja na maana ya wizi kisheria.

Wananchi hao walisema, wamejua njia ambazo mwananchi anaweza kuingia kwenye kosa la wizi, ikiwa ni pamoja na kununua vifaa vya wizi, kuficha taarifa pamoja na kumpa mawasiliano.

Mwananchi Massoud Juma Khamis, alisema ujio huo wa watendaji wa CHAPO, umewaamsha katika ufahamu pia wa masuala ya udhalilishaji, ule ambao sio maarufu kwa jamii.

Alieleza kuwa, kutopeleka huduma za kibinadamu ambazo zinaweza kuwasababishia watoto kubakwa, kudhalilishwaji ni mambo ambayo hawakujua madhara yake.




‘’Tukiona tu kuwa, kama hakuna huduma athari kubwa ni familia kulia njaa, lakini sasa tumeelewa kuwa, kumbe watoto wanaweza kujiingiza kwenye udhalilishaji, kwa kule kutafuta huduma,’’alieleza.

Nae Yussuf Bakar Khamis, alisema mpango huo wa ‘CHAPO’ lazima uwe endelevu kwa vijijini vyengine, ili wananchi wapate uwelewa.

‘’Kwanza, niwapongeza sana wasaidizi hawa wa sheria kutoka CHAPO, maana leo (jana), mmetufumbua macho, na tunawaomba msikae tena sana mje,’’alieleza.

Akifungua mkutano huo, Sheha wa shehia ya Kilindi wilaya ya Chake chake Nassor Mohamed Khamis, alisema ni wajibu wa wananchi, waliopata taaluma ya kisheiria, kuwafikishia wenzao.

‘’Inawezekana, yupo mwanakijiji mwenzetu hapa Kuungeni hakuwahi kufika, sasa ni wajibu wetu kuhakikisha anafikishiwa elimu hii ya kisheria,’alifafanua.




Katika hatua nyingine, sheha huyo aliwataka wananchi kuendelea, kuwaripoti wahalifu na wadhalilishaji mbali mbali, ili serikali kwa upande wake, ichukuwe hatua.

Mapema Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, alisema wamekuwa wakitoa msaada wa kisheria, bila ya malipo.

Alieleza kuwa, ni wajibu wa wananchi sasa kuwatumia wasaidizi wa sheria waliopo shehiani, kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa masuali mbali mbali ya haki zao.



Akizungumzia kuhusu kampeni ya kitaifa ya msaada wa kisheria ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, alisema inalenga kukuza uwelewa kwa jamii, juu ya sheria msaada wa kisheria.

Mratibu wa ‘CHAPO’ Mohamed Hassan Abdalla, alisema moja ya jambo ambalo wananchi wanashindwa kutofautisha, ni kati ya kesi kumalizika na mtuhumiwa kupewa dhamana.

‘’Mkimuona mtuhumiwa ambae mmepeleka Polisi anaranda mtaani, wakati mwengine amepata dhamana, ambayo ni haki ya mtuhumiwa, hili lazima tulijuwe,’’alifafanua.



Msaidizi wa sheria Jimbo la Chonga Juma Seif Haji, alisema jamii isipokuwa makini kwenye dawa za kulevya, vijana wanaweza kupoteza mwelekeo wa maisha yao.

‘’Moja ya jukumu letu, ni kutoa taarifa kwenye mamlaka husika, ikiwemo Jeshi la Polisi, maana athari zake huikumba jamii ikiwemo vitendo vya wizi na udhalilishaji,’’alieleza.



Msaidizi wa sheria Jimbo la Ziwani Khadija Said Khalfan, amewataka wanaume, kutekeleza majukumu yao, kwa kina ili kutowaingiza wanawake kwenye majaribu ya maisha.



CHAPO inaendelea na mpango wake wa kupita katika shehia kadhaa za wilaya ya Chake chake, kwa ajili ya kukutana na wananchi kusikiliza changamoto zao, za kisheria.

                           Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’