CHAPO KUZINDUA MAFUNZO MAALUM YA KISHERIA WAWI MACHI 11, 2023

 

 


NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@


JUMUIYA ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’, asubuhi ya leo, inatarajia kufungua mafunzo maalum ya sheria ngazi ya jamii, kwa lengo la kuwapa uwelewa wanajamii.

Akizungumza na mwandishi wa habari wa hizi ofisini kwake leo Machi 10, 2023 mjini Chake chake, Mkurugenzi wa ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, alisema, tayari kila kitu kimeshakamilika kuelekea mafunzo hayo.

Alisema, mafunzo hayo ya kwanza na maalum kufanywa kwa aina yake, ni miongoni mwa mpango kazi wa ‘CHAPO’ katika kuwaelimisha wananchi masuala ya kisheria.

Alieleza kuwa, ‘CHAPO’ inaamini kila mwananchi anayo haki ya kupata uwelewa wa masuala ya kisheria, na ndio maana ‘CHAPO’ ikabuni mpango huo.

Mkurugenzi huyo alifafanua kuwa, mafunzo hayo kwa kuanzia, yataanzia shehia ya Wawi kama eneo la majaribio, na kisha kusambaa katika majimbo manne ya wilaya ya Chake chake.

‘’Uzinduzi wa mafunzo haya yanatarajiwa kufanyika Machi 11, ukumbi wa Kiwanda cha Mafuta ya Makonyo Wawi wilaya ya Chake chake, na tayari kila kitu kimekaa sawa,’’alieleza.

Aidha Mkurugenzi huyo wa ‘CHAPO’ alisema, ubunifu wa mafunzo hayo, yalitokana na wasaidizi wao wa sheri wa Jimbo la Wawi, ikiwa ni hatua ya kuwafikia wananchi kupata elimu hiyo.

‘’Wazo la wasadizi wa sheria wetu hawa, kwanza tumelipokea mikono miwili, na sasa tumeona liwe la wilaya nzima, ili kuhakikisha kila jimbo, mafunzo hayo yanasambaa,’’alieleza.

Alieleza kuwa, kwa hatua za awali jumla ya wananchi 20 wa shehia ya Wawi, wakiwemo wajumbe 10 wa kamati ya sheha na wananchi wengine 10, ndio watakaoingia kwenye mafunzo,’’alifafanua.

Msaidizi wa sheria Jimbo la Wawi Fatma Hilali, alisema uongozi wa shehia ya Wawi, umeshatoa baraka zote kuelekea mafunzo hayo, ikiwa ni pamoja na kukubali kutoa washiriki.

Hata hivyo, alisema anatamani kuona mfumo huo wa mafunzo, unaendelezwa wilaya yote ya Chake chake na hatimae Zanzibar nzima.




Afisa Sheria kutoka Idara ya Katiba na Msaada wa Kisheria Zanzibar ofisi ya Pemba Bakari Omar Ali, alipongeza hatua hiyo, na kuomba zoezi hilo, lihamie kwenye majimbo na wilaya nyingine.

‘’Ni jukumu la ‘CHAPO’ na jumuia nyingine kuhakikisha wanawaelimisha wananchi, kutambua haki na wajibu wao kisheria, ili waishi kwenye bahari ya haki na kuvua samaki wa uadilifu,’’alieleza.

Hata hivyo, ameonya kuwa, bado jukumu la kutoa elimu, msaada na ushauri wa kisheria, utendelea kubakia mikononi mwa wasaidizi wa sheria wanaotambulika kisheria.

Kwenye uzinduzi wa mafunzo hayo, yanayotarajiwa kuwa ya siku 10, mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Afisa Mdhamini wizara ya nchi, afisi ya rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Halima Khamis Ali.


Miongoni mwa waalikwa ni pamoja na Mwenyekiti wa Madiwani wilaya ya Chake chake, madiwani wa wadi za Wara na Kiboni, Mwenyekiti wa masheha, Katibu, Askari shehia na masheha wa shehia zote zinazounda Jimbo la Wawi.

                                                Mwisho  

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’