WASAIDIZI WA SHERIA WAWI: 'VIJANA MSICHEZE CHEZE NA WATOTO OVYO OVYO WATAWAUMBUA'
NA MWANDISHI MAALUM, CHAPO
MSAIDIZI wa sheria Jimbo la Wawi Haji
Nassor Mohamed, amewatahadharisha vijana wa shehia ya Wawi, kuacha kucheza
cheza na watoto, kwani huwa rahisi kuwataja mara wanapofanyiwa vitendo vya
udhalilishaji.
Kauli hiyo
ameitoa Febuari 19, 2023 uwanja wa mpira wa miguu Wawi, wakati akizungumza na
wanamichezo kabla ya kuanza kwa michezo ya ligi daraja la pili taifa, mkoa wa
kusini Pemba.
Alisema ule
utamaduni wa kucheza cheza na watoto wa kike na wakati mwengine kuwaita majina
kama mchumba, wauwepuke, kwani wapo vijana ambao umeshawawek pabaya, baadhi ya
watu.
‘’Kama kuna
mtoto wa miaka 12, au 16 hadi 17 umekuwa ukipenda kumtania kwa kumuita mchumba,
hili jambo tuwe makini nalo, maana mtoto akidhalilishaji na mtu asiyemju, huwa
rahisi kumtaja aliyekaribu naye,’’alieleza.
Katika hatua
nyingine, Msaidizi huyo wa sheria Jimbo la Wawi Haji Nassor Mohamed,
amewaelekeza wanamichezo hao, kuwa kisheria mtoto ni mtu yeyote aliyechini ya
miaka 18.
‘’Kwa mujibu
wa sheria zetu, mtoto hana ridhaa, hivyo hata kama yeye atakuita kwao na
kukufungulia mlango, lakini mkifanya tendo, hutafsiriwa kuwa ni ubakaji,’’alieleza.
Katika hatua
nyingine, amewataka wanamichezo hao kushughulika na michezo na kazi nyingine za
kujipatia kipato cha halali, na sio kujiingiza kwenye vitendo vya wizi.
Hata hivyo
amewataka kila mmoja kuwa mlinzi kwa mwenzake, juu ya matumizi, kusambaaza,
kuuza au kuingiza dawa za kulevya, kwani madhara yake ni makubwa.
Amewakumbusha
kuwatumia wasaidizi wa sheria waliomo jimboni humo, ili kupata ufumbuzi wa
mambo yao mbali mbali ya kisheria.
Mapema
Katibu klabu ya mpira wa miguu ya Wawi star Juma Mohamed ‘Mgawaji’ alisema
aliwakumbusha vijana hao, kujiepusha na visharia vyote vinavyowapeleka kwenye
matendo ya kihalifu.
‘’Kama tuna
msaidizi wetu wa sheria tumtumieni tunapokuwa na shida kwenye masuala ya
kisheria, iwe jinai au madai, ili kupata ufumbuzi kabla ya kwenda juu zaidi,’’aleleza.
Kwa upande
wake Msaidizi wa sheria wa Jimbo hilo Fatma Hilali, aliwasisitiza vijana hao,
kujiheshimu na kuheshimiana, ili kulinda haki za binadamu.
‘Inapoishia
haki yao ya bindamu, ndio inapoanzia ya mwenzako, sasa lazima hili tulijue ili
kuhakikisha tunaishi kwa amani,’’alieleza.
Nae Mjumbe
wa sheha wa shehia hiyo kutoka kijiji cha Mtemani shehia humo, Nassor Rashid Said,
alimtaka Masaidizi huyo wa sheria, kuendelea kukutana na vijana kila wakati,
kuwapa elimu kama hiyo.
‘’Sheria ni
jambo pana na kubwa, sasa tukuomba leo isiwe ya mwisho, maana vijana
wanakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwa ni pamoja dawa za kulevya,
udhalilishaji na wizi,’’alifafanua.
Mwisho




Comments
Post a Comment