MWAKILISHI WAWI ABARIKI CHAPO KUANZISHA DARASA LA SHERIA KWA WANANCHI
NA HAJI NASSOR, PEMBA::
MWAKILISHI wa Jimbo la Wawi Bakar
Hamad Bakar, ameunga mkono, wazo la wasaidizi wa sheria Jimbo la Wawi, la
kutaka kuanzishwa darasa maalum la kutoa elimu ya sheria, kwa wananchi wa
shehia ya Wawi jimboni humo.
Alisema, wazo
la wasaidizi hao wa sheria, kutaka kuanzisha darasa maalum, ni jambo la msingi,
kwani elimu waliyopatiwa wao, itasambaa kwa upana.
Mwakilishi
huyo aliyasema hayo, Febuari 19, 2023 wakati akizungumza na uongozi wa shehia ya Wawi, kwenye
kikao maalum cha maandalizi ya darasa hilo.
Alisema,
wananchi wanahitaji kupata elimu ya kujua haki na wajibu wao kwa jamii, samba
mba na kupata uwelewa wa mambo ya kisheria.
‘’Kwanza
niunge mkono wazo ambalo wenzetu hawa wasaidizi wa sheria Jimbo la Wawi,
wameliwaza na mimi nitaunga mkono kwa hali na mali, ili kufanikisha darasa
hilo,’’alieleza.
Katika hatua
nyingine, Mwakilishi huyo wa Jimbo la Wawi aliwataka wasaidizi hao wa sheria,
kuhakikisha darasa hilo linakuwa endelevu, kwa kundi jingine hapo baadae.
Kwa upande
wake Sheha wa shehia ya Wawi Sharifa Waziri, alisema amelipokea wazo hilo la
kuanzisha darasa maalum la elimu ya sheria, kutoka kwa wasaidizi wa sheria
jimboni humo.
‘’Tayari
tumeshawateua vijana 10 ambao wataungana na wajumbe tisa wa shehia, katika
darasa hilo ambalo linatarajiwa kuanza mwezi ujao,’’alieleza.
Hata hivyo
sheha huyo alisema, atahakikisha darasa hilo linakuwa endelevu, ili makundi
mengine ndani ya shehia hiyo, yaweza kufaidika na elimu hiyo.
Mkurugenzi
wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake ‘CHAPO’ Nassor Bilali
Ali, alisema wameamua kuanzisha darasa hilo, ili elimu ya sheria ifike kwa
upana kwa jamii.
‘’Mikutano yetu
ya kila shehia ya kukutana na makundi mbali mbali ya jamii kuwaelimisha juu ya
mambo ya udhalilishaji, dawa za kulevya na migogoro ya ardhi, ipo kama
kawaida,’’alieleza.
Hata hivyo Mkurugenzi
huyo alisema, gharama za uendeshaji wa mafunzo hayo yanayotarajiwa kuwa ya siku
10, zitabebwa na ‘CHAPO’ kwa kushirikiana na wadau wengine, ili kuhakikisha
jamii, inapata elimu.
Hata hivyo
alisema darasa hilo litakuwa kwa wilaya nzima, ingawa kwa kuanzia litaanzia
shehia ya Wawi Jimbo la Wawi, kama eneo la majaribio.
Kwa upande
wake Msaidizi wa sheria wa jimboni humo Fatma Hilali, alisema baada ya kufikiria
waliona ni vyema sasa kuzaa wazo hilo, ili kuhakikisha elimu inasambaa.
‘’Tuliona
tuanzishe darasa maalum, ambalo litakuwa na wananchi 20 kwa hatua za awali, ili
kuwa nao darasani, kwa lengo la kuwasomesha sheria,’’alieleza.
Mmoja kati
wanafunzi tarajiwa kwenye darasa hilo Issa Omar, alisema watahakikisha wanashiriki
vyema kwenye darasa hilo, mwanzo hadi mwisho.
Nae Afua Ali
Hamad, alisema wamefurahishwa mno na uamuzi wa wasaidizi wao wa sheria wa
kuanzisha darasa maalum.
Mwisho



Comments
Post a Comment