MSAIDIZI WA SHERIA WESHA AWAPA MBINU WANAWAKE MALEZI YA WATOTO

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA:::

WANAWAKE wa kijiji cha Kaole, shehia ya Wesha wilaya ya Chake chake Pemba, wametakiwa kujitathimini aina ya malezi wanayowarithisha watoto wao, ikiwa ni mwafaka, kwa ajili ya kuyamudu mazingira yao, ya kupambana na majanga mbali mbali, kama ya ukatili na udhalilishaji.

 

Ushauri huo umetolewa Novemba 5, mwaka 2022 na Msaidizi wa sheria wa shehia za Wesha na Ndagoni wilayani humo, Khadija Said Khalfan wakati akizungumza na wananchi hao, kwenye mkutano wa wazi wa kutoa elimu, ndani ya siku 16 za kupinga ukatili, mkutano ulioandaliwa na Jamuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake ‘CHAPO’.

 

Alisema, kila utafiti unaofanywa, umekuwa ukiwaangukia wanawake, kuwa wamelengaza kamba katika malezi, na wapo baadhi yao, wamekuwa wakiwarithisha malezi mabovu watoto wao.

 

Alieleza kuwa, kwa mfano wapo wanawake wamekuwa wakiwafichia uovu hasa watoto wa kike, na kujenga uadui kwa baba yao, jambo ambalo halimsaidii mtoto, katika maisha yake ya baadae.

 

‘’Utamskia mama ataka kumrushu mtoto wake kwenda atakako, ingawa anamueleza kuwa baba yake ndio kikwazo,’’huu sio utamaduni mzuri katika malezi.

 

Aidha msaidizi huyo wa sheria, katika shehia za Wesha na Ndagoni, Khadija Said Khalfan alisema, malezi mengine ambayo sio mwafaka kwa maendeleo ya mtoto, ni wazazi walio wengi kuwaachia simu watoto wao.

 

‘’Sasa walezi wakubwa kwa sisi wanawake ni kumfungulia simu mtoto wakati anapolia, aina ya picha na muziki wanaowekewa anajua mama mwenyewe,’’alifafanua.

 

Akizungumzia vitendo vya ukatili na udhalilishaji, alisema namna ya kuviondoa, ni jamii kushirikiana kwa dhati na vyombo vya ulinzi na vya sheria.

 




‘’Njia nyingine, ambayo ni rahisi katika kutokomeza matendo haya, ni kufika mahakamani kutoa ushahidi, kupambana na kushirikiana katika malezi, kati ya baba na mama,’’alifafanua.

 

Hata hivyo amewataka wananchi hao, kuitumia ofisi yao CHAPO, wanapohisi wamewakosa wasaidizi wa sheria waliomo shehiani mwao, ambapo watapewa elimu, ushauri na msaada wa kisheria bila ya malipo.

Akifungua mkutano huo Sheha wa shehia ya Wesha, Haji Mohamed Ali, alisema kazi inayofanywa na wasaidizi wa sheria ni kubwa, na kilichobaki kwa wananchi, ni kubadilika kivitendo.

 





‘’Katika tasisi inayoongoza kwa kuwafikia wananchi, ni wasaidizi wa sheria kutoka ‘CHAPO’ na naamini, kila mwananchi anaefika kwenye mikutano yao, anapa elimu ya kupambana na vitendo hivyo,’’alieleza.

 

Akiwasilisha mada ya njia ya kutokomeza matendo hayo, msaidizi wa sheria kutoka Jimbo la Chake chake, Wahida Kombo Khamis, alisema ni jamii kuyachukia kwa vitendo.

 



Njia nyingine, alisema ni kurudi katika imaani za kidini, ambapo hakuna hata dini moja, inayoruhusu matendo hayo, bali ni mtu mwenyewe tu kwa kule kukosa maadili.

 

‘’Mimi niwashauri, kama nia ya kutokomeza matendo haya ipo, basi kwanza tuanze kwa ngazi ya kijiji, kuyarejesha yale malezi ya zamani, ambayo mtoto mmoja akilelewa na watu wote,’’alishauri.

 

Baadhi wananchi wa kijiji hicho, akiwemo Raya Khamis Abdalla, alisema dhabu nyepesi kwa wanaotiwa hatiani kwa makosa ya udhalilishaji, bado haijawatia woga wengine.

‘’Mpaka leo unaskia kwenye vyombo vya habari kuwa, mshitakiwa wa ubakaji, amefungwa miaka saba, 10 na 20, wakati sheria, tunaambiwa inaekeleza miaka 30 au kifungo cha maisha,’’alisema.

 

Nae Maryam Said Sabour, alisema kama jamii haikushirikiana katika mapambano hayo, itakuwa ndoto kuondoka kwake, maana watendaji wa matukio hayo, wanatoka katika jamii.

 

Kwa upande wao Ali Ghalib Omar, Khamis Said Hamad na Asha Said Ali, walisema bado harufu ya rushwa kwenye vyombo vya sheria, inanukia.

 





Mapema askari kutoka kituo cha Polisi wilaya ya Chake chake anayeshughulikia shehia ya Wesha Khamis Ali Khamis, alisema jamii, ikiamua kupambana na uhalifu, shehia itakuwa salama.

 





Mkutano huo wa wazi shehia ya Wesha, ni muendelezo wa mikutano inayofanywa na ‘CHAPO’ katika siku hizi 16 za kupinga ukatili, ambapo shehia za Ole, Ndagoni, Ziwani tayari mikutano kama huo.

                           Mwisho   

 

  

 

 

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’