MKURUGENZI 'CHAPO' AWAVUTIA PUMZI WAJUMBE WATORO WA VIKAO
NA
HAJI NASSOR, PEMBA:::
MKURUGENZI
wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ Nassor
Bilali Ali, ameelezea kusikitishwa kwake na baadhi ya watendaji wa jumuiya
hiyo, kukumbwa na dharura kila panapoitishwa vikao.
Alisema, wapo baadhi ya
watendaji sasa wamekuwa ndio ugonjwa wao usio na tiba wa kutohudhuria vikao,
jambo ambalo kwa baadhi ya wakati, hurejesha nyuma mipango na mikakati yao.
Mkurugenzi huyo ameyasema hayo, Novemba 5, mwaka 2022, ofisini kwake mjini Chake chake, wakati akizungumza na watendaji wake, kwenye kikao cha robo ya nne ya mwaka.
Alisema vikao ni sehemu
muhimu ya kutengeneza, kuunda au kuamua jambo husika kwa maslahi ya wananchi wa
wilaya ya Chake chake, sasa ikiwa kuna wajumbe ni wagonjwa kwa dharura wanaweza
kukwamisha jitahada.
Alisema kuanzia sasa ‘CHAPO’
itakuwa wakali kwa wajumbe watoro na wasiopenda kufuata wakati wa vikao husika,
kwani kinyume chake, wanaweza kukwamisha baadhi ya mambo.
Alieleza kuwa, inafamika
kuwa kila mmoja anayotaasisi anayoifanyia kazi, lakini haina maana kuwa, wanapokuwa
na shughuli zao, iwe vigumu wengine kuhudhuria.
‘’Ni kweli ndani ya
wasaidizi wa sheria, tunao ambao ni watumishi wa umma, lakini tukumbuke
tumebeba mazingo wa jamii wa kuwahudumia kisheria,’’alieleza.
Katika hatua nyingine
Mkurugenzi huyo, aliwasilisha yatokanayo na mkutano uliofanyika Dodoma hivi
karibuni, chini ya ufadhili wa mfuko huru wa msaada wa kisheria ‘LSF’ ambao
umesisitiza uwajibikaji.
‘’Kutakuwa
na ufuatiliaji wa taasisi yetu na hata msaidizi wa sheria mmoja mmoja katika
jimbo, shehia na kijiji, ili wanaofanya ufuatiliaji na tathmini, wajiridhishe.
Nae Mratibu wa Jumuiya hiyo
Mohamed Hassan Abdalla, alisema ni vyema kila mmoja, kuanza kujipanga upya
katika utendaji wake wa kazi, ili kuona ‘CHAPO’ inazidi kupata heshima kwa
jamii.
‘’Sisi kwa Zanzibar ndio
jumuia ya pili kutuma ripoti ya mwaka, sasa lazima tujipange, tushirikiane na
tusaidiane, ili ubora na utendaji wetu upande juu,’’alieleza.
Msaidizi Mratibu wa ‘CHAPO’ Khadija
Said Khalfan, alisema ni vyema kwa wanaopata mafunzo, kuhakikisha wanaporudi
wanawawezesha na wenzao.
‘’Haiwezekani mtu anakwenda
mafunzo akirudi anayaweka kapuni, na kama tukiendelea na utamaduni huu, itakuwa
ndani ya CHAPO wataalamu ni kidogo,’’alishauri.
Nao wasaidizi wa sheria wa
Jimbo la Chake chake Abeda Said na Mashavu Juma Mabroku, walisema lazima mkazo
uwekwe wa kuendelea kushirikiana kama zamani, wakati wa utoaji wa elimu ya
kisheria vijijini.
Kwa upande wake mshika fedha
wa CHAPO Riziki Hamad Ali, alisisitiza suala la ulipaji wa ada na michango kwa
wale wanaopata mikutano kupitia Jumuiya hiyo.
Katika kikao hicho cha robo
ya mwisho wa mwaka, wasaidizi wapya wa sheria watano, wametakiwa kuwa karibu na
wasaidizi waliowatangulia ili kupata uwelewa.
Jumuiya ya wasaidizi wa
sheria wilaya ya Chake chake Pemba, ‘CHAPO’ ambayo shughuli zake kuu ni kutoa
elimu, ushauri na msaada wa kisheria bila ya malipo, inawahudumia wananchi wa
shehia 32 zilizomo kwenye majimbo ya Chake chake, Wawi, Ole, Chonga na Ziwani.
Mwisho
.jpg)






Comments
Post a Comment