MKURUGENZI CHAPO, AWAPA USHAURI WA BURE MASHEHA

 


IMEANDIKWA NA KHADIJA NA HAJI- CHAPO:::


MKURUGENZI wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheri wilaya ya Chake chake Pemba ‘CHAPO’ Nassor Bilali Ali, amewataka masheha, kutayarisha kamati za usuluhishi wa migigoro ya ardhi, zinazokubalika na jamii, ili iwe rahisi wakati wa utendaji wao wa kazi.

Alisema, moja ya jukumu la kamati hizo hapo baadae, ni kusikiliza migogoro ya ardhi, na kuota ushauri kwa ajili ya kupatikana kwa sulhu, hivyo lazima wachugue wajumbe wanaokubalika katika jamii.

Ushauri huo, ameutoa jana wakati akizungumza, kwenye uzinduzi wa mradi wa Kujenga uwelewa kwa jamii, katika kuzuia migogoro itokanayo na matumizi ya ardhi ya uwekezaji, na kufanyika skuli ya Pujini wilaya ya Chake chake.

Alisema, kamati hiyo itaundwa na wajumbe, na kisha kupewa elimu ya utatuzi wa migogoro na hata baada ya mradi huo kukamilika, itatakiwa kuendelea kufanyakazi kwa jamii.

‘’Masheha ni watu wenye uwelewa mkubwa, hivyo natamani sana kuona wakati ukifika, tupate wajumbe wa kamati wanaokubalika ndani ya jamii,’’alishauri.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi huyo wa CHAPO, alisema pamoja na uwepo wa wasaidizi wa sheria karibu kila shehia, lakini CHAPO, iliona vyema kutafuta mradi huo, ili kuwafikia wananchi wengi kielimu.

Mapema akizungumza kwenye ufunguzi wa mafunzo hayo, sheha wa shehia ya Pujini Khamis Uledi Kombo, aliishukuru CHAPO, kwa uamuzi wake wa kuendesha mradi huo katika shehia yake.

‘’Ni kweli migogoro ya ardhi sasa imekuwa kama maji ya kunywa, kila eneo na hata hapa Pujini, sasa CHAPO na wafadhili wao ‘the foundation for Civil society’ kutuletea mradi huu’ utasaidia mno,’’alieleza.

Akieleza malengo la mradi huo, Mratibu wa mradi kutoka ‘CHAPO’ Riziki Hamad Ali, alisema mradi huo wa mwezi mmoja, utakuwa na shughuli tatu kuu, ikiwemo mafunzo ya utatuzi wa migogoro kwa masheh, wajumbe wao na wasaidizi wa sheria.

‘’Shughuli nyingine itakayofanyika ni kuunda mabaraza ya shehia ya usuluhishi wa migogoro na mikutano ya wazi kwa wananchi, ambayo watapata fursa ya elimu,’’alifafanua.

Aidha Mratibu huyo, alisema mradi huo ulitokana na mikutano ya wazi, walioifanya kwa wananchi, na kuelezea uwepo wa uhaba wa elimu ya kukinga na kutatua migogoro ya ardhi.

‘’Sisi pamoja na wafadhili wetu ‘foundation’ tunatarajia baada ya kumalizika kwa mradi huu, kwanza migogoro ya ardhi ipungue na vijana wahamasike kutunza amani na kudumu kwa baraza ya usuluhishi,’’alieleza.

Akiwasilisha mada ya utatuzi wa migogoro, mtoa mada Mohamed Hassan Abdalla, alisema elimu ndogo ya sheria za ardhi, ni moja ya sababu za uwepo wa migogoro ya ardhi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Mkoani Nassor Hakim Haji, alisema moja ya faida ya mabaraza ya usuluhishi wa migogoro ni kupunguza kesi mahakamani.


Wakichangia kwenye mkutano huo, washiriki hao walisema mradi huo ni mzuri, maana unaweza kuwa chachu ya kupungumza migogoro ya radhi.

Sheha wa shehia ya Mfikiwa Bimkubwa Tangwi, alisema jamii imekuwa ikisababisha migogoro ya aradhi, kutokana na kutokujua sheria husika.

Nao washiriki Salim Ali Matta, Abeda Adi Seif, Idrissa Khamis Vuai na Thuheni Talib Thuheni, walisema licha ya muda mfupi wa mradi huo, lakini kama mabaraza yatakayoundwa yatafanyakazi kwa bidii, migogoro ya ardhi itapungua.






Shehia ambazo zinatekeleza mradi huo ni Pujini, Dodo na Mfikiwa, ambapo wajumbe wanne na sheha kila shehia walihudhuria kwenye uzinduzi wa mradi huo.

Jumuiya ya wasaidizi wa sheria wilaya ya Chake chake CHAPO ambayo imeanzishwa mwaka 2016, moja ya majukumu yake ni kutoa elimu, ushauri na msaada wa kisheria bila ya malipo kwa wananchi.

                          Mwisho

Comments

Popular posts from this blog

AFISI YA MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR YAKUSANYA MAONI SHERIA YA MSAADA WA KISHERIA

MKURUGENZI HANIFA, AWAUMA SIKIO WANANCHI WAWI HAKI ZA BINAADAMU

‘WANANCHI HAWANA MAMLAKA YA KUONDOSHA UHAI WA MTU’